1Kisha, Yawe akamwambia Musa:
2“Uwaambie Waisraeli warudi nyuma, wapige kambi mbele ya Pi-Hahiroti, kati ya muji wa Migdoli na bahari Nyekundu, mbele ya Bali-Sefoni. Mutapiga kambi mbele yake karibu na bahari.
3Maana, mufalme wa Misri atafikiri: ‘Hao Waisraeli wanatangatanga, nalo jangwa limewazuia wasiweze kutoka.’
4Halafu mimi nitafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye atawafuatilia. Nami nitajipatia utukufu kwa kumwangamiza yeye na jeshi lake. Halafu Wamisri watatambua kwamba mimi ni Yawe.” Basi, Waisraeli wakafanya hivyo.
5Mufalme wa Misri aliposikia kwamba Waisraeli wamekimbia, yeye na wakubwa wake walibadilisha mafikiri yao, wakasema: “Tumefanya nini kwa kuwaachilia Waisraeli waende zao wasitutumikie tena?”
6Basi, mufalme akatayarisha gari lake la vita na jeshi lake.
7Alitwaa magari yake bora ya vita mia sita na magari yote mengine ya kivita ya Misri yakiongozwa na wakubwa wa kijeshi.
8Yawe akafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye akawafuatilia Waisraeli ambao walikuwa wameondoka Misri katika uhuru.
9Wamisri pamoja na farasi wao wote, magari ya vita na wapanda-farasi wake waliwafuata Waisraeli. Wakawakuta wamepiga kambi kando ya bahari, karibu na Pi-Hahiroti, mbele ya Bali-Sefoni.
10Waisraeli walipoinua macho na kumwona mufalme wa Misri akikuja na jeshi lake nyuma yao, wakashikwa na hofu kubwa, wakamulilia Yawe.
11Wakamwambia Musa: “Hakukuwa makaburi ya kutosha katika inchi ya Misri hata ukatuleta tukufie huku katika jangwa? Kwa nini umetufanya tutoke katika inchi ya Misri?
12Hatukukuambia mambo haya tulipokuwa bado Misri? Tulikuambia utuache tuendelee kuwatumikia Wamisri. Ingalikuwa vizuri kuwatumikia Wamisri kuliko kukufia huku katika jangwa.”
13Musa akawaambia Waisraeli: “Musiogope! Musimame imara! Leo mutaona jinsi Yawe atakavyowaokoa. Maana, hawa Wamisri munaowaona leo, hamutawaona tena.
14Yawe atawapigania. Ninyi mutakaa kimya tu.”
15Yawe akamwambia Musa: “Kwa nini munanililia? Uwaambie Waisraeli waendelee mbele.
16Inua fimbo yako na kuielekeza juu ya bahari. Maji yatagawanyika na Waisraeli wataweza kuvuka katikati ya bahari pahali pakavu.
17Mimi nitafanya mioyo ya Wamisri kuwa migumu, nao watawafuatilia katikati ya bahari. Nami nitajipatia utukufu kutokana na kuangamizwa kwa mufalme wa Misri na jeshi lake, magari yake ya vita pamoja na wapanda-farasi wake.
18Hakika, nitatukuzwa kwa kumwangamiza mufalme na jeshi lake, pamoja na magari yake na wapanda-farasi. Nao Wamisri watajua kwamba mimi ni Yawe.”
19Basi, malaika wa Mungu aliyekuwa mbele ya kundi la Waisraeli akaondoka akakaa nyuma yao. Na ule munara wa wingu vilevile ukaondoka mbele ukasimama nyuma yao.
20Ukakaa katikati ya Waisraeli na Wamisri. Lile wingu likawatia Wamisri giza, lakini likawaangazia Waisraeli usiku. Kwa hiyo, makundi hayo mawili, jeshi la mufalme wa Misri na kundi la Waisraeli, hayakukaribiana usiku kucha.
21Musa akanyoosha mukono wake juu ya bahari, naye Yawe akasukuma bahari nyuma kwa upepo mukali toka upande wa mashariki. Upepo ule ulivuma usiku kucha, ukagawanya bahari sehemu mbili na katikati kukatokea inchi kavu.
22Waisraeli wakapita katikati ya bahari pahali pakavu, kuta za maji zikiwa upande wao wa kuume na wa kushoto. Ang. 1 Kor 10.1-2; Ebr 11.29
23Wamisri wakawafuata kwa kupitia inchi kavu iliyokuwa katikati ya bahari pamoja na farasi wao, magari yao ya vita na wapanda-farasi wao wote.
24Karibu na mapambazuko, Yawe akaangalia jeshi la Wamisri kutoka katika ule munara wa moto na ule munara wa wingu, akalitia hofu kubwa.
25Alikwamisha magurudumu ya magari yao, yakakuwa yakienda kwa shida sana. Halafu Wamisri wakasema: “Tuwakimbie Waisraeli! Yawe anawapigania Waisraeli mbele yetu.”
26Kisha Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu ya bahari, kusudi maji yarudie na kuwafunika Wamisri pamoja na magari yao na wapanda-farasi wao.”
27Basi, Musa akanyoosha mukono wake juu ya bahari na kulipopambazuka bahari ikarudilia hali yake ilivyokuwa. Wamisri wakajaribu kukimbia maji lakini Yawe akawasukumizia ndani ya bahari.
28Maji yakafunika magari pamoja na wapanda-farasi. Jeshi lote la mufalme wa Misri lililokuwa limewafuatilia Waisraeli likakufa katika bahari. Hakukuponyoka Mumisri hata mumoja.
29Lakini Waisraeli walipita katikati ya bahari pahali pakavu, kuta za maji zikiwa zimesimama upande wao wa kuume na wa kushoto.
30Siku hiyo Yawe akawaokoa Waisraeli toka mikono ya Wamisri. Waisraeli wakawaona maiti ya Wamisri pembeni ya bahari.
31Waisraeli walipoona tendo hilo la ajabu Yawe alilofanya mbele ya Wamisri, wakamwogopa. Wakamwamini Yawe na Musa mutumishi wake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.