1Heri ningepata kibanda cha wasafiri katika jangwa,
ningewaacha watu wangu na kujiendea.
Wote ni wazinzi,
ni kundi la watu waasi.
2Ndimi zao ni hatari kama pinde;
wameimarika kwa ajili ya uongo na si kwa ajili ya haki.
Wanaendelea kutenda uovu kisha uovu,
wala hawanitambui mimi.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
3Kila mutu ajiepushe na jirani yake,
wala asimwaminie ndugu yake!
Maana ndugu ni mudanganyifu
na kila jirani ni musingiziaji.
4Kila mutu anadanganya jirani yake,
hakuna hata mumoja anayesema ukweli.
Wamezifundisha ndimi zao kusema uongo;
anatenda uovu kwa kadiri ya kushindwa kabisa kunigeukia.
5Wanalundika matendo ya kuzulumu juu ya mengine,
nao udanganyifu juu ya udanganyifu.
Wanakataa kunitambua mimi.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
6Kwa hiyo, Yawe wa majeshi anasema hivi:
Nitawasafisha na kuwapima kwa moto
kama vile chuma.
Ni namna gani zaidi ya kuwatendea hawa watu wangu waovu?
7Ndimi zao ni kama mishale yenye sumu,
hawachoki kudanganya;
kila mutu anaongea vema na jirani yake,
lakini anafanya mipango ya kumushambulia ndani ya moyo wake.
8Nisiwaazibu kwa sababu ya mambo haya?
–Ni ujumbe wa Yawe.–
Nisililipize kisasi taifa kama hili?
Nyakati za kulia na kuomboleza9Nitalia na kuomboleza juu ya milima;
nitaomboleza juu ya mashamba ya nyama katika jangwa,
kwa sababu yamekauka kabisa,
hakuna mutu anayepita pahali pale.
Hakusikiliki tena sauti za ngombe;
ndege na nyama wamekimbia na kutoweka.
10Yawe anasema:
Nitaifanya Yerusalema kuwa mabomoko matupu,
nitaifanya kuwa pango la mbweha;
na miji ya Yuda nitaifanya kuwa jangwa,
pahali pasipokaliwa na mutu yeyote.
11Nami nikauliza: Kuna mutu anayekuwa na hekima apate kueleza mambo haya? Ni nani aliyeongea na Yawe hata aweze kutangaza kwa nini inchi imeharibiwa na kufanywa tupu kama jangwa hata hakuna mutu anayepita humo?
12Yawe akajibu na kusema hivi: Ni kwa sababu wamekataa kushika sheria yangu niliyowapa, wamekataa kutii sauti yangu na kufuata mapenzi yangu.
13Wamefuata ugumu wa mioyo yao, wakaenda kuabudu miungu inayoitwa Mabali kama walivyofundishwa na babu zao.
14Basi, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitawakulisha watu hawa uchungu na kuwapa maji yenye sumu wakunywe.
15Nitawatawanya kati ya mataifa ambayo wao wenyewe wala babu zao hawakupata kuyajua; na kisha nitatuma vita nyuma yao mpaka hapo nitakapowaangamiza wote.
16Yawe wa majeshi anasema hivi:
Mufikiri na kuwaita wanawake waombolezaji;
muwaite wanawake wanaoelewa nyimbo za kilio.
17Muwaambie hivi: Mukuje upesi muomboleze juu yetu,
macho yetu yapate kutiririka machozi,
na kope zetu zibubujike machozi kama maji.
18Kilio hiki kinasikilika Sayuni:
Tumeangamia kabisa!
Tumefezeheshwa kabisa,
kwa maana sherti tuiache inchi yetu,
nazo nyumba zetu zibomolewe!
19Enyi wanawake, musikilize neno la Yawe!
Mutege masikio musikie jambo analosema.
Muwafundishe wabinti zenu kuomboleza,
na kila mutu amufundishe jirani yake wimbo huu wa maziko:
20Kifo kimetuingilia katika madirisha yetu,
kimetupangia katika nyumba zetu nzuri;
kimewaangukia watoto wetu katika barabara,
nao vijana wetu katika viwanja vya makutano.
21Sema:
Huu ni ujumbe wa Yawe:
Maiti za watu zinalala chini kila pahali
kama malundo ya mboleo katika mashamba,
kama miganda iliyoachwa na muvunaji,
wala hakuna anayeikusanya.
22Yawe anasema hivi:
Mwenye hekima asijivunie hekima yake,
mwenye nguvu asijivunie nguvu yake;
wala tajiri asijivunie utajiri wake.
23Anayetaka kujivuna,
ajivune kwamba ananifahamu mimi,
kwamba anajua kwamba mimi Yawe ninatenda mema,
ninafanya mambo ya haki kufuatana na sheria yangu katika dunia.
Watu wa namna hiyo ndio wanaonipendeza.
–Ni ujumbe wa Yawe.
24Siku zinakuja ambapo nitawaazibu wote waliotahiriwa kimwili tu.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
Ni kusema nitawaazibu:
25Wamisri, Wayuda, Waedomu, Waamoni, Wamoabu na wakaaji wote wa jangwa wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa. Maana watu hawa wote na Waisraeli wote hawajatahiriwa mioyo yao.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.