1Roho wa Bwana wetu Yawe yuko pamoja nami,
maana Yawe amenichagua,
akanituma niwahubirie wanaoteswa habari njema,
niwatunze waliovunjika moyo,
niwatangazie waliohamishwa kwamba watapata uhuru,
na wafungwa kwamba watafunguliwa.
2Amenituma kutangaza mwaka wake wa neema,
na siku ya Mungu wetu ya kulipiza kisasi
kusudi niwafariji wote wanaoomboleza.
3na kuwapa wale wanaoomboleza katika Sayuni
taji la maua pahali pa majivu juu ya kichwa,
mafuta ya kuangarisha kwa furaha pahali pa maombolezo,
nguo ya sifa pahali pa moyo muzito.
Nao wataitwa miti ya mialo ya haki,
Yawe aliyopanda kuonyesha utukufu wake.
4Watayajenga upya mabomoko ya zamani,
wataisimika miji iliyoharibika tangu mbele;
wataitengeneza miji iliyobomolewa,
uharibifu wa vizazi vingi vilivyopita.
5Wageni watakuwa hapo kuwachungia makundi yenu ya nyama;
watawalimia na kuwatunzia mizabibu yenu.
6Nanyi mutaitwa: “Makuhani wa Yawe”,
Mutaitwa: “Watumishi wa Mungu wetu”.
Mutafaidika kwa utajiri wa mataifa,
mutatukuzwa kwa mali zao.
7Kwa vile mulipata haya mara mbili,
watu wakaona kwamba mazarau ni majaliwa yenu,
sasa mutapata sehemu mara mbili kuwa mali yenu,
na furaha yenu itadumu milele.
8Mimi Yawe ninapenda watu wafuate sheria yangu;
ninachukia unyanganyi na uovu.
Nitawatunza watu wangu kwa uaminifu,
nitafanya nao agano la milele.
9Wazao wao watajulikana kati ya mataifa;
watajulikana kati ya watu wengine.
Kila mutu atakayewaona atakubali kwamba
wao ni watu waliobarikiwa na Yawe.
10Nitafurahi sana kwa sababu ya Yawe,
nafsi yangu itashangilia kwa sababu ya Mungu wangu.
Maana amenivalisha nguo ya wokovu,
amenifunika kanzu ya haki,
kama bwana arusi anavyojipamba kwa shada la maua,
kama bibi arusi anavyojipamba kwa ushanga wake.
11Hivyo, kama vile udongo unavyootesha mimea,
na shamba linavyochipukiza mbegu zilizopandwa humo,
Yawe atasababisha haki na sifa
kuonekana mbele ya mataifa yote.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.