Matayo 16 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Wafarisayo na Wasadukayo wanataka kitambulisho(Mk 8.11-13; Lk 12.54-56)

1Wafarisayo na Wasadukayo wakamufikia Yesu. Nao wakamupima wakimwomba awaonyeshe kitambulisho kinachohakikisha kwamba uwezo wake unatoka kwa Mungu.

2Lakini akawajibu: “Kwa wakati wa magaribi munapoona kwamba mawingu ni meupe, munasema kwamba hali ya hewa itakuwa nzuri kesho yake.

3Na asubui munapoona kwamba mawingu ni meusi munasema kwamba mvua itanyesha. Munajua kutambua hali ya mawingu, lakini hamuwezi kujua vitambulisho vya nyakati hizi.

4Watu wa kizazi kibaya na kinachokosa uaminifu mbele ya Mungu wanataka kuona kitambulisho. Lakini hawataonyeshwa kitambulisho isipokuwa kitambulisho cha nabii Yona.” Kisha Yesu akawaacha na kujiendea.

Chachu ya Wafarisayo na Wasadukayo(Mk 8.14-21)

5Wakati wanafunzi walipovuka ziwa kwenda ngambo ingine, walikuwa wamesahau kupeleka mikate.

6Yesu akawaambia: “Muangalie vizuri, mujiepushe na chachu ya Wafarisayo na Wasadukayo.”

7Wanafunzi wakaanza kusemezana hivi wao kwa wao: “Anasema hivi kwa sababu hatuna mikate.”

8Yesu akatambua maneno waliyosema, basi akawauliza: “Ee ninyi wenye imani ndogo, sababu gani munasemezana kati yenu juu ya kukosa mikate?

9Hamujaelewa bado? Hamukumbuki ile mikate mitano niliyoshibisha nayo watu elfu tano, nayo ile hesabu ya vitunga mulivyojaza?

10Hamukumbuki vilevile ile mikate saba niliyoshibisha nayo watu elfu ine, na ile hesabu ya vitunga mulivyojaza?

11Namna gani hamwelewi kwamba sisemi nanyi juu ya mikate, nilipowaambia kwamba mujiepushe na chachu ya Wafarisayo na Wasadukayo.”

12Halafu wanafunzi wakafahamu kwamba Yesu hakuwaambia kwamba wafanye angalisho na chachu ya mikate, lakini na mafundisho ya Wafarisayo na Wasadukayo.

Petro anajulisha kwamba Yesu ni Kristo(Mk 8.27-30; Lk 9.18-21)

13Yesu alipofika pande za muji Kaisaria Filipi, akawauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema kwamba Mwana wa Mutu ni nani?”

14Nao wakamujibu: “Wamoja wanasema kwamba yeye ni Yoane Mubatizaji; wengine wanasema kwamba yeye ni Elia, na wengine wanasema ni Yeremia au mumoja wa manabii wengine.”

15Halafu Yesu akawauliza: “Na ninyi munasema kwamba mimi ni nani?”

16Simoni Petro akamujibu: “Wewe ni Kristo, Mwana wa Mungu Mwenye Uzima.”

17Halafu Yesu akamwambia: “Heri kwako, wewe Simoni mwana wa Yona, kwa maana hakuna mutu aliyekufunulia neno hili isipokuwa Baba yangu anayekuwa mbinguni.

18Nami sasa ninakuambia: ewe Petro, wewe ni jiwe, na juu ya jiwe hili, nitajenga musingi wa kanisa langu, na hata uwezo wa lufu hautaweza kulishinda.

19Nitakupa funguo za Ufalme wa mbinguni; chochote utakachokikataza katika dunia, kitakatazwa mbinguni vilevile, na chochote utakachokiruhusu katika dunia, kitaruhusiwa mbinguni vilevile.”

20Kisha Yesu akawakataza sana wanafunzi wake wasimwambie mutu kwamba yeye ndiye Kristo.

Yesu anajulisha habari za kufa na kufufuka kwake(Mk 8.31–9.1; Lk 9.22-27)

21Tangia wakati ule Yesu akaanza kuwaambia wanafunzi wake waziwazi kwamba ni sherti kwake kwenda Yerusalema, ateswe kule na wasimamizi wa watu, wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria, auawe, na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.

22Basi Petro akamwita Yesu pembeni na kuanza kumukaripia, akisema: “Ee Bwana, isikuwe vile! Mambo yale hayatakufikia hata kidogo!”

23Lakini Yesu akageuka na kumwambia: “Ondoka hapa karibu nami, wewe Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa maana mawazo yako si ya Mungu, lakini ni ya kimutu.”

24Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kama mutu akitaka kunifuata, ajikane yeye mwenyewe, lakini ajitolee kwa kubeba musalaba wake na kunifuata.

25Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu, ataupata tena.

26Ni faida gani kwa mutu kupata utajiri wote wa dunia, lakini anapoteza uzima wake? Hakuna kitu mutu anachoweza kutoa kwa kukomboa uzima wake.

27Kwa maana Mwana wa Mutu atakuja na wamalaika akitukuzwa na Baba yake, halafu atamulipa kila mutu kufuatana na matendo yake.

28Kweli ninawaambia: wamoja kati ya watu wanaokuwa hapa hawatakufa mbele hawajamwona Mwana wa Mutu akikuja katika Ufalme wake.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help