1Basi Daudi akasema: “Hapa ndipo pahali ambapo nyumba ya Yawe itakuwa, na hii ndiyo mazabahu ambapo watu wa Israeli watatolea sadaka ya kuteketezwa kwa moto.”
Matayarisho ya kujenga hekalu2Daudi akatoa amri kwamba wageni wote waliokuwa katika inchi ya Israeli wakusanyike, naye akawapangia kazi. Akaweka wamoja wachonge vizuri mawe ya kujenga nyumba ya Mungu.
3Daudi akaweka vilevile akiba tele ya chuma cha kutengeneza misumari na vifungio vya milango ya nyumba, na akiba tele ya shaba isiyopimika.
4Mbao za mierezi ambazo Daudi aliletewa na Wasidoni na Watiro zilikuwa hazihesabiki.
5Daudi akajisemesha: “Nyumba ambayo mwana wangu Solomono atakayomujengea Yawe itakuwa nzuri sana, ya kusifiwa na tukufu katika dunia yote. Lakini kwa vile yeye bado angali kijana na bado hana maarifa mengi, afazali nimufanyie matayarisho.” Hivyo basi, Daudi akaweka akiba kubwa sana ya vitu vya kujenga mbele ya kufa kwake.
6Halafu Daudi akamwita mwana wake Solomono, akamwagiza amujengee Yawe, Mungu wa Israeli, nyumba.
7Daudi akamwambia Solomono: “Mwana wangu, nilikusudia ndani ya moyo wangu kumujengea Yawe, Mungu wangu, nyumba kwa kumutukuza. Ang. 2 Sam 7.1-16; 1 Sik 17.1-14
8Lakini neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: ‘Wewe umemwanga damu nyingi na kupigana vita kubwa. Kwa sababu ya damu nyingi ambayo umemwanga mbele yangu hapa katika dunia, hautanijengea nyumba.
9Hata hivyo, utapata mwana ambaye atatawala kwa amani kwa sababu nitamupa amani na waadui zake wote wa jirani. Jina lake litakuwa Solomono, kwa maana katika siku za utawala wake, atailetea inchi ya Israeli amani na utulivu.
10Hivyo, yeye ndiye atakayenijengea nyumba. Atakuwa mwana wangu nami nitakuwa baba yake, na wazao wake watatawala Israeli milele.’
11“Sasa, mwana wangu, Yawe, Mungu wako, akuwe pamoja nawe kusudi uweze kumujengea nyumba kama vile alivyosema.
12Yawe akupe hekima na akili kusudi atakapokupa uongozi juu ya Israeli, ushike sheria za Yawe, Mungu wako.
13Ukiwa mwangalifu, na ukitii masharti na maagizo ambayo Yawe alimwagiza Musa juu ya Israeli, utastawi. Ujipe moyo, ukuwe imara. Usiogope wala usifazaike. Ang. Yos 1.6-9
14Kwa juhudi kubwa, nimeiwekea akiba nyumba ya Yawe zaidi ya toni elfu tatu za zahabu, zaidi ya toni elfu moja za feza pamoja na shaba na chuma visivyoweza kupimwa maana ni vingi sana. Nimetayarisha mbao na mawe. Lakini utaweza kuongeza.
15Uko na watumishi wengi: kuna wachongaji wa mawe, wajengaji, waseremala na wafundi wa kila aina wenye ujuzi mwingi
16wa kufua zahabu, feza, shaba na chuma. Basi sasa, anza kazi! Yawe akuwe pamoja nawe!”
17Zaidi ya hayo, Daudi akawaamuru viongozi wote wa Waisraeli wamusaidie mwana wake Solomono, akisema:
18“Yawe, Mungu wenu hayuko pamoja nanyi? Hajawapa amani katika pande zote? Yeye aliwatia wakaaji wa inchi hii katika mikono yangu na sasa wako chini ya Yawe na watu wake.
19Sasa, mumutumikie Yawe, Mungu wenu, kwa nia na moyo wote. Basi mujitayarishe kumujengea Yawe pahali patakatifu kusudi Sanduku la Agano la Yawe pamoja na vyombo vyote vitakatifu vinavyotumiwa katika ibada, viwekwe ndani ya nyumba iliyojengwa kwa ajili ya Yawe.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.