1Kuna muda kwa kila kitu, na wakati kwa kila jambo katika dunia:
2wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa,
wakati wa kupanda na wakati wa kuvuna kilichopandwa,
3wakati wa kuua na wakati wa kuponyesha,
wakati wa kubomoa na wakati wa kujenga,
4wakati wa kulia na wakati wa kucheka,
wakati wa kuomboleza na wakati wa kucheza,
5wakati wa kutupa mawe na wakati wa kukusanya mawe pamoja,
wakati wa kukumbatia na wakati wa kutokumbatia,
6wakati wa kutafuta na wakati wa kupoteza,
wakati wa kuchunga na wakati wa kutupa,
7wakati wa kupasua na wakati wa kushona,
wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema,
8wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia,
wakati wa vita na wakati wa amani.
9Mufanya kazi anafaidia nini kutokana na jasho aliyotoa?
10Mimi nimeiona kazi ambayo mwanadamu amepewa na Mungu.
11Mungu amefanya kila kitu kikuwe kizuri kwa wakati wake. Ameweka ndani ya moyo wa mwanadamu mawazo juu ya muda usiokuwa na mwisho, lakini mutu hawezi kuelewa mwanzo na mwisho wa matendo ya Mungu.
12Ninajua kwamba, kwa mwanadamu, kuna jambo moja tu la kumufalia: kufurahi na kujifurahisha kwa muda wote anapoishi.
13Kama mwanadamu anakula na kunywa na kufurahia matunda ya jasho yake, hayo ni majaliwa ya Mungu.
14Ninajua kwamba jambo lolote Mungu analotenda linadumu milele. Hakuna kinachoweza kuongezwa wala kupunguzwa. Mungu amefanya mambo yakuwe hivyo kusudi wanadamu wamwogope yeye.
15Kinachotukia sasa, kilikwisha tukia; kitakachotukia nyuma kilikwisha kutukia. Mungu anafanya kitu kitukie tena na tena.
Ukosefu wa haki chini ya jua16Zaidi ya hayo, nimegundua chini ya jua kwamba uovu unatawala kwa pahali pa haki na sheria.
17Basi, nikasema ndani ya moyo wangu: “Mungu atawahukumu watu wa haki hata vilevile na waovu, maana amepanga wakati kwa kila jambo na kwa kila kazi.”
18Nikasema ndani ya moyo wangu: “Mungu anawajaribu wanadamu, kwa kuwaonyesha kwamba wao ni sawa tu na nyama.”
19Mwisho wa mwanadamu na mwisho wa nyama ni mumoja. Jinsi mwanadamu anavyokufa ndivyo nyama anavyokufa. Wote wanapumua namna ileile; mwanadamu si bora kuliko nyama. Yote ni bure.
20Wote wanakufa na kwenda kwa nafasi moja. Wote wametoka katika mavumbi na wote watarudi katika mavumbi.
21Nani anayejua, basi, kama kweli roho ya mutu inapanda juu, na roho ya nyama inashuka chini ndani ya udongo?
22Basi, nikatambua kwamba hakuna jambo linalokuwa bora zaidi kwa mwanadamu kufanya kuliko kufurahia kazi yake, kwa sababu amepangiwa hivyo. Nani anayeweza kumujulisha mwanadamu yale yatakayokuwa kisha kufa kwake?
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.