Ezekieli 43 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yawe anarudi katika hekalu

1Kisha, yule mutu akanipeleka kwenye mulango unaoelekea upande wa mashariki.

2Utukufu wa Mungu wa Israeli ulitokea upande wa mashariki. Pamoja nao kulikuwa mushindo wa kuja kwake kama mushindo wa maji mengi, inchi ilingaa kwa utukufu wake. Ang. Eze 10.3-4,18-19; 11.22-23; Ufu 1.15

3Maono hayo yalikuwa kama maono niliyoyaona wakati Mungu alipokuja kuuangamiza Yerusalema. Vilevile yalifanana na maono niliyoyaona karibu na muto Kebari. Nikaanguka uso mpaka chini.

4Nao utukufu wa Yawe uliingia katika nyumba ya Yawe kwa njia ya mulango wa mashariki.

5Kisha roho akanitwaa na kunipeleka kwenye kiwanja cha ndani. Nikaona utukufu wa Yawe ukiwa umeijaza nyumba ya Yawe.

6Yule mutu akiwa anasimama karibu nami, nilisikia mutu fulani akisema nami kutoka katika nyumba ya Yawe;

7naye akaniambia: Wewe mwanadamu! Hapa ndipo pahali pa kiti changu cha kifalme, pahali ninapoweka miguu yangu. Nitakaa kati ya watu wa Israeli milele. Na Waisraeli hawatalichafua jina langu, wao wenyewe, wala wafalme wao kwa kuziabudu sanamu au kuzika maiti za wafalme wao pahali hapa.

8Wafalme wao walijenga vizingiti na miimo ya nyumba zao za kifalme karibu na vizingiti vya nguzo za hekalu langu, hivyo kati yangu na wao ulikuwa ni ukuta tu. Walichafua jina langu takatifu kwa machukizo yao waliyotenda, ndiyo maana nimewaangamiza kwa hasira yangu.

9Sasa waache kuziabudu sanamu na waziondoe maiti za wafalme wao mbali nami, nami nitakaa kati yao milele.

10Sasa, ewe mwanadamu, uwaelezee Waisraeli habari za nyumba ya Mungu na wajifunze taswira yake. Wapate haya kutokana na machukizo yao waliyotenda.

11Wakipata haya kutokana na matendo yao, waeleze taswira ya nyumba ya Mungu: taswira yake yenyewe, milango ya kuingilia na kutokea, umbo lake lote, mipango ya kila kitu, kanuni zake na masharti yake. Uwaandikie hayo yote waziwazi kusudi waweze kuona namna yote yalivyopangwa na waweze kuzifuata kanuni na masharti yake.

12Hii ni sheria juu ya nyumba ya Yawe: Eneo lote linalozunguka nyumba ya Yawe juu ya mulima linapaswa kuwa takatifu kabisa.

Mazabahu katika hekalu

13Vipimo vya mazabahu, vitakuwa vilevile kama vipimo vya hekalu. Kutakuwa musingi wenye urefu wa sentimetre makumi tano na upana wa sentimetre makumi tano kuzunguka musingi wa mazabahu, pamoja na ukingo wenye urefu kuenda juu wa sentimetre makumi mbili na tano. Ang. Kut 27.1-2; 2 Sik 4.1

14Sehemu ya mazabahu itakayokuwa chini kabisa tokea juu ya musingi itakuwa na kimo cha metre moja. Sehemu itakayofuata itawekwa nyuma kutoka kwenye ukingo sentimetre makumi tano muzunguko, na kimo cha metre mbili. Sehemu itakayofuata nayo itawekwa nyuma ya ukingo sentimetre makumi tano muzunguko.

15Sehemu hii ya juu, ambayo itatumika kuteketezea sadaka, itakuwa muraba, kila upande metre mbili. Mujengo wa pembe za sehemu hii ya juu zitainuka kuliko sehemu zingine.

16Sehemu ya juu ya mazabahu itakuwa muraba, metre sita kila upande.

17Sehemu ya katikati, itakuwa muraba, sentimetre saba kila upande, nayo itakuwa na ukingo pembeni wenye kimo cha sentimetre makumi mbili na tano. Kutakuwa mufereji wenye upana wa sentimetre makumi tano. Na kutakuwa ngazi za kupandia kwenye mazabahu kila upande.

Kutakaswa kwa mazabahu

18Bwana wetu Yawe akaniambia. Wewe mwanadamu! Yawe anasema hivi: Wakati mazabahu itakapojengwa utaitakasa, kwa kutoa sadaka za kuteketezwa juu yake na kuinyunyizia damu ya nyama waliotolewa. Ang. Kut 29.35-37

19Wale makuhani wanaokuwa wa kabila la Lawi ambao ni wazao wa Zadoki, ndio tu watakaokaribia mbele yangu kwa kunitumikia.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

Utawapa ngombe dume muchanga kuwa sadaka ya kusamehewa zambi.

20Utatwaa damu yake na kuitia juu ya pembe ine za mazabahu na juu ya chongo ine za daraja na juu ya muzunguko wake pande zote. Hivyo ndivyo utakavyoisafisha mazabahu na kuitakasa.

21Utatwaa vilevile ngombe dume aliyetolewa kuwa sadaka ya kusamehewa zambi; watamuteketeza katika pahali palipochaguliwa ndani ya nyumba ya Yawe, lakini inje ya Pahali Patakatifu.

22Kesho yake, utatoa beberu asiyekuwa na kilema, kuwa sadaka ya kusamehewa zambi; mazabahu itatakaswa kama ilivyotakaswa kwa damu ya ngombe dume.

23Utakapokwisha kuitakasa, utatwaa ngombe dume mudogo asiyekuwa na kilema na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema na

24kuwaleta mbele yangu. Makuhani watawapakaa chumvi na kuwatoa kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Yawe.

25Kwa muda wa siku saba, kila siku utatoa beberu mumoja akuwe sadaka ya kusamehewa zambi. Vilevile watatoa ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema.

26Hivyo kwa muda wa siku saba, utafanya upatanisho na kuisafisha, na hivyo utatakasa mazabahu.

27Kisha siku hizo saba, tokea siku ya nane na kuendelea, makuhani watatoa sadaka zenu za kuteketezwa na sadaka zenu za amani. Nami nitawakubali.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help