1Shuka, uikae katika mavumbi,
ewe bikira, binti wa Babeli!
Ikaa chini pasipo kiti cha kifalme,
ewe binti wa Wakaldea!
Tokea sasa hautaitwa tena murembo wala mwenye kupendeza.
2Utwae mawe ya kusagia, usage unga kama mutumwa!
Vua kitambaa chako, pandisha kanzu yako!
Onyesha miguu yako kwa kuvuka mito.
3Watu watauona uchi wako;
wataona haya yako.
Mimi nitalipiza kisasi,
wala sitamuhurumia mutu yeyote.
4Mukombozi wetu ndiye Mutakatifu wa Israeli;
Yawe wa majeshi ndilo jina lake.
5Ikaa kimya, ingia katika giza,
ewe taifa la Wakaldea.
Maana umepoteza cheo yako
ya kuwa malkia wa falme.
6Niliwakasirikia watu wangu, Israeli,
nikawafanya watu wangu kuwa wanaharamu.
Niliwatia katika mikono yako,
nawe haukuwaonea huruma;
na wazee uliwabebesha nira nzito sana.
7Ulijisemesha ndani ya moyo: “Nitakuwa malkia milele”,
nawe haukufikiri juu ya mambo yanayotokea,
wala kuwaza juu ya mwisho wake.
8Sasa, basi, sikiliza, ewe mupenda raha,
wewe unayezani kuwa katika usalama,
na kujisemesha: Mimi ndiye.
Hakuna mwingine isipokuwa mimi.
Sitakuwa mujane hata kidogo,
wala sitakufiwa na watoto wangu.
9Haya yote mawili yatakupata
kwa rafla katika siku moja:
kupoteza watoto wako na kuwa mujane,
ijapokuwa una wingi wa uchawi wako,
na nguvu nyingi za uganga wako.
10Ulijiona salama katika uovu wako;
ukajisemesha: Hakuna mutu anayeniona.
Hekima na elimu yako vilikupotosha,
ukajisemesha ndani ya moyo wako: Mimi ndiye;
hakuna mwingine isipokuwa mimi.
11Lakini hasara itakupata
ambayo hautaweza kujiepusha nayo.
Magumu yatakutokea
ambayo hautaweza kuyapinga;
maangamizi yatakufikia kwa rafla
ambayo haujapata kuyaona hata kidogo.
12Endelea basi na uganga wako,
tegemea wingi wa uchawi wako.
Wewe uliyashugulikia tangu ujana wako
ukitumainia kwamba utafanikiwa
au kusababisha woga kwa watu!
13Wewe umejichokesha bure na washauri wako.
Basi, wajitokeze hao wenye akili wakuokoe!
Wao wanagawanya mbingu sehemusehemu,
wanachunguza nyota
na kutabiri kila mwezi yatakayokupata.
14Wao ni kama majani yenye kukauka:
moto utayateketeza!
Hawawezi hata kujiokoa wenyewe
mbali na ukali wa moto huo.
Moto huo si wa kujipatia joto,
huo si moto wa kuota!
15Ndivyo watakavyokuwa hao uliowategemea hivyo,
hao uliojishugulisha nao tangu ujana wako.
Watatangatanga kila mumoja njia yake;
hakuna hata mumoja atakayeweza kukuokoa.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.