1Haya ni maneno ya mwisho ya Daudi. Ni ujumbe wa Daudi mwana wa Yese, ujumbe wa mutu ambaye Mungu alimufanya akuwe mukubwa, muchaguliwa wa Mungu wa Yakobo, mwimbaji muzuri wa zaburi wa Israeli:
2Roho wa Yawe amesema kwa njia yangu,
aliyaweka maneno yake katika kinywa changu.
3Mungu wa Israeli amesema,
Yeye Jiwe la Kufichamia la Israeli ameniambia:
Mutu anayetawala watu kwa haki,
anayewatawala akimwogopa Mungu,
4yeye ni kama mwangaza wa asubui,
jua linapochomoza asubui isiyokuwa na mawingu.
Yeye ni kama mvua inayootesha majani juu ya udongo.
5Hivi ndivyo jamaa yangu inavyokuwa mbele ya Mungu.
Maana amefanya nami agano la kudumu milele;
agano kamili na lenye kuwa imara.
Naye atanifanikisha katika mahitaji yangu yote.
6Lakini watu waovu
wote ni kama miiba inayotupwa tu,
maana haiwezi kukamatwa kwa mukono;
7kwa kuigusa, sherti kutumia chuma au mupini wa mukuki.
Watu hao wataangamizwa kabisa kwa moto.
Mashujaa wa Daudi(1 Sik 11.10-47)8Haya ni majina ya mashujaa Daudi aliokuwa nao:
Yosebu-Basebeti, wa muji wa Takemoni ndiye aliyekuwa kiongozi wa wale watatu. Yeye alipigana kwa mukuki wake, akaua watu mia nane mara moja katika vita.
9Halafu aliyefuata kati ya wale mashujaa watatu alikuwa Eleazari mwana wa Dodayi, wa ukoo wa Muahoa. Siku moja, Eleazari alikuwa pamoja na Daudi walipowatukana Wafilistini waliokuwa wamekusanyika kwa kupigana vita. Waisraeli waliwakimbia Wafilistini.
10Lakini Eleazari alisimama imara na kupigana na Wafilistini mpaka mukono wake uliposhindwa kupindika, ukabaki umebania upanga wake. Siku hiyo, Yawe alijipatia ushindi mukubwa. Nyuma ya ushindi ule, Waisraeli walirudi pahali Eleazari alipokuwa na kuteka vitu kutoka kwa Wafilistini waliouawa.
11Shujaa wa tatu alikuwa Sama mwana wa Age, wa muji wa Harari. Wafilistini walikusanyika kule Lehi, pahali palipokuwa shamba la manjegere nyingi. Kule Waisraeli waliwakimbia Wafilistini.
12Lakini alisimama imara katikati ya shamba lile kwa kulikinga, naye akawaua Wafilistini. Kwa hiyo, Yawe akajipatia ushindi mukubwa.
13Kisha, mashujaa watatu kati ya wakubwa makumi tatu waliteremuka wakati wa mavuno, wakamufikia Daudi kwenye pango kule Adulamu. Wakati ule kundi la waaskari wa Wafilistini lilikuwa limepiga kambi katika bonde la Refaimu.
14Naye Daudi wakati ule alikuwa katika maficho, nalo kundi la Wafilistini lilikuwa katika muji Betelehemu.
15Daudi akasema kwa hamu kubwa: “Ni nani atakayeweza kunipa maji ya kunywa kutoka katika kisima cha Betelehemu, kinachokuwa karibu na mulango wa muji!”
16Wale mashujaa wake watatu walitoka, wakapenya katikati ya kambi ya kundi la waaskari wa Wafilistini, wakaenda na kuchota maji katika kisima cha Betelehemu, karibu na mulango wa muji, wakamuletea Daudi. Lakini Daudi alikataa kuyakunywa, na pahali pa kuyakunywa, akayamwanga chini kama vile sadaka kwa Yawe,
17akisema: “Sina haki hata kidogo ya kunywa maji haya, ee Yawe. Maji haya si ni kama damu ya wale walioyahatarisha maisha yao kwa kuyaleta?” Kwa hiyo, Daudi hakuyakunywa maji hayo. Hayo ndiyo mambo waliyotenda wale mashujaa watatu.
18Abisayi mwana wa Zeruya na ndugu ya Yoabu alikuwa mukubwa wa mashujaa makumi tatu. Yeye alipigana kwa mukuki wake na watu mia tatu, akawaua, akajipatia sifa pamoja na wale mashujaa watatu.
19Alikuwa na heshima zaidi kati ya wale mashujaa makumi tatu. Kwa hiyo akakuwa jemadari wao, lakini hakukuwa shujaa kama wale mashujaa watatu.
20Naye Benaya mwana wa Yehoyada wa muji Kabuseli, alikuwa askari shujaa ambaye alifanya mambo mengi ya ajabu. Aliwaua mashujaa wawili kutoka Moabu, na siku moja wakati wa teluji, alishuka katika shimo na kuua simba.
21Vilevile, aliua mutu mumoja jitu wa Misri. Mumisri yule alikuwa na mukuki, lakini Benaya alimwendea akiwa na fimbo tu, akamunyanganya mukuki ule, na kumwua Mumisri yule kwa mukuki wake mwenyewe.
22Benaya mwana wa Yehoyada alifanya mambo haya, akajipatia sifa pamoja na wale mashujaa watatu.
23Akakuwa na heshima pamoja na wale mashujaa makumi tatu, ingawa hakukuwa kama wale mashujaa watatu. Na Daudi akamupa cheo cha mukubwa wa waaskari walinzi wake.
24Asaeli ndugu ya Yoabu, alikuwa mumoja wa mashujaa makumi tatu.
Mashujaa wengine wa Daudi walikuwa: Elihanani, mwana wa Dodo wa Betelehemu;
25Sama na Elika, wote wa muji Harodi;
26Helesi wa muji Palti; Ira mwana wa Ikesi wa muji Tekoa;
27Abiezeri wa muji Anatoti; Mebunayi wa muji Husa:
28Zalmoni wa muji Ahoa; Maharai wa muji Netofa;
29Helebu mwana wa Bana wa muji Netofa; Itayi mwana wa Ribayi toka Gibea katika kabila la Benjamina;
30Benaya wa muji Piratoni; Hidayi wa vijito vya Gasi;
31Abialboni wa muji Araba; Azimaweti wa muji Bahurimu;
32Eliabu wa muji Salaboni; wana wa Yaseni; Yonatani;
33na Sama wa muji Harari; Ahiamu mwana wa Sarari wa muji Arari;
34Elifeleti mwana wa Ahasibayi wa Maka; Eliamu mwana wa Ahitofeli wa Gilo;
35Hesiro wa muji Karmeli: Parayi wa muji Araba;
36Igali mwana wa Natani wa inchi ya Zoba; Bani wa muji Gadi;
37Zeleki wa inchi ya Waamoni; Naharayi wa muji Beroti aliyekuwa mubebaji wa silaha wa Yoabu mwana wa Zeruya;
38Ira na Garebu wa ukoo wa Yeteri;
39na Uria wa inchi ya Wahiti. Wote pamoja walikuwa mashujaa makumi tatu na saba.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.