1Kulikuwa kumebaki siku mbili mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka na ya Mukate Usiyotiwa Chachu. Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria walitafuta njia ya kumukamata Yesu kwa werevu kusudi wamwue.
2Kwa maana walijisemesha: “Tusimukamate kwa wakati wa karamu, kusudi fujo isitokee kati ya watu.”
Yesu anamimiwa marasi(Mat 26.6-13; Yn 12.1-8)3Yesu alikuwa Betania katika nyumba ya mutu aliyeitwa Simoni Mukoma. Walipokuwa wakikula, mwanamuke mumoja akaingia ndani ya nyumba. Alikuwa na chupa la jiwe lenye marasi ya bei kali yaliyotengenezwa na maua ya nardo safi. Kisha akavunja mudomo wa lile chupa na kumimia marasi juu ya kichwa cha Yesu.
4Na wamoja kati ya watu waliokuwa pale wakachukizwa na kitendo kile na kusemezana: “Kwa nini kupoteza mali namna hii?
5Marasi hii ingeweza kuuzishwa kwa bei ya vikoroti mia tatu vya feza na kugawanyia wamasikini mali ile.” Na wakamukasirikia yule mwanamuke vikali.
6Lakini Yesu akasema: “Mumwache kimya! Sababu gani munamusumbua? Yeye amenitendea jambo zuri.
7Kwa maana mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, na munaweza kuwasaidia wakati wowote munapotaka, lakini mimi sitakuwa pamoja nanyi siku zote.
8Amefanya sawa alivyoweza. Ameupakaa mwili wangu marasi mbele ya wakati kwa kuutayarisha kwa ajili ya maziko.
9Kweli ninawaambia: kwa ajili ya kukumbuka mwanamuke huyu, tendo lile alilofanya litaelezwa popote Habari Njema itakapohubiriwa katika dunia nzima.”
Yuda anakubali kumutoa Yesu(Mat 26.14-16; Lk 22.3-6)10Yuda Iskariota, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akaenda kwa wakubwa wa makuhani, kusudi amutoe Yesu kwao.
11Waliposikia habari ile wakafurahi sana, nao wakamwahidia kumupa feza. Basi Yuda akaanza kutafuta wakati muzuri kwa kumutoa.
Yesu anakula Pasaka pamoja na wanafunzi wake(Mat 26.17-25; Lk 22.7-14,21-23; Yn 13.21-30)12Siku ya kwanza ya karamu ya sikukuu ya Mukate Usiyotiwa Chachu, wakati ambapo walichinja kondoo wa Pasaka, wanafunzi wa Yesu wakamwuliza: “Unataka tuende wapi kukutayarishia karamu ya Pasaka?”
13Basi Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake akiwaambia: “Mwende katika muji, na kule mutakutana mutu mumoja anayebeba mutungi wenye maji. Mumufuate mutu yule,
14na pahali atakapoingia, mumwambie mwenye nyumba: ‘Mwalimu anauliza kwamba ni wapi kunapokuwa chumba chake ambamo atakulia karamu ya Pasaka pamoja na wanafunzi wake.’
15Naye atawaonyesha chumba kikubwa cha gorofi, kilichokwisha kupangwa vizuri na kuwa tayari. Ni mule mutakapotutayarishia karamu.”
16Halafu wanafunzi wakaondoka, wakaenda katika muji, wakakuta vitu vyote tayari sawa vile Yesu alivyowaambia. Nao wakatayarisha karamu ya Pasaka.
17Ilipokuwa magaribi, Yesu akafika pamoja na wanafunzi wake kumi na wawili.
18Walipokuwa wameikaa kula chakula, Yesu akasema: “Kweli ninawaambia: mumoja kati yenu anayekula pamoja nami atanitoa.”
19Wanafunzi wakaanza kuhuzunika na kumwuliza mumoja kwa mumoja: “Ni mimi?”
20Yesu akawajibu: “Ni mumoja kati yenu ninyi kumi na wawili, anayechovya mukate pamoja nami ndani ya sahani moja.
21Kwa maana Mwana wa Mutu atakufa sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema juu yake, lakini ole kwa yule mutu atakayemutoa! Ingekuwa heri kwake kama asingezaliwa.”
Yesu anasimika karamu ya Bwana(Mat 26.26-30; Lk 22.14-20; 1 Kor 11.23-25)22Walipokuwa wakikula, akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema: “Mutwae, huu ni mwili wangu.”
23Kisha akatwaa kikombe, akakibariki na kuwapa, nao wote wakakikunywa.
24Na Yesu akawaambia: “Hii ni damu yangu; damu inayomwangika kwa ajili ya watu wengi kwa kuhakikisha agano la Mungu.
25Kweli ninawaambia: Tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka siku ile nitakapoikunywa kwa upya katika Ufalme wa Mungu.”
26Na walipokwisha kuimba wimbo, wakaondoka kwenda kwa mulima wa Mizeituni.
Yesu anatabiri kwamba Petro atamukana(Mat 26.31-35; Lk 22.31-34; Yn 13.36-38)27Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ninyi wote mutaanguka, kwa maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nitamwua muchungaji, na kondoo watasambazwa.’
28Lakini nitakapokwisha kufufuka, nitawatangulia Galilaya.”
29Petro akamwambia: “Hata wote wengine wakianguka, mimi sitaanguka.”
30Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia kwamba usiku huu, mbele jogoo hajawika mara mbili, utakuwa umenikana mara tatu.”
31Lakini Petro akazidi kusema kwa nguvu: “Hata ikinipasa kufa pamoja nawe, sitakukana hata kidogo.” Na wote wengine wakasema sawasawa naye.
Yesu anaomba katika Getesemane(Mat 26.36-46; Lk 22.39-46)32Wakafika katika bustani inayoitwa Getesemane, na Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Muikae hapa kwa wakati mimi nitakapokuwa nikiomba.”
33Kisha akatwaa Petro, Yakobo na Yoane na kwenda nao. Akaanza kuwa na hofu na mahangaiko.
34Akawaambia: “Ninahuzunika sana, karibu kufa! Mubakie hapa na mukeshe.”
35Kisha akajitenga mbali kidogo nao, akajitupa chini. Akaomba kwamba ikiwezekana, saa ile ya mateso imuondokee mbali.
36Akasema: “Ee baba! Yote yanawezekana kwako; ninakuomba uniondolee mbali hiki kikombe cha mateso. Lakini isikuwe kama vile mimi ninavyotaka, lakini kama vile wewe unavyotaka.”
37Aliporudi akawakuta wamelala usingizi. Akamwambia Petro: “Simoni, umelala? Haukuweza kukesha hata kwa saa moja tu?
38Mukeshe na kuomba, kusudi musianguke katika majaribu; kwa maana roho ni hodari, lakini mwili ni zaifu.”
39Mara tena akawaacha, akaomba akirudilia maneno yale yale.
40Aliporudi tena, akawakuta wanafunzi wale wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa yamewezwa sana na usingizi. Nao hawakujua wamujibu nini.
41Aliporudi kwa mara ya tatu, akawaambia: “Mungali munalala na kupumzika? Inatosha! Saa imetimia. Sasa Mwana wa Mutu anatolewa katika mikono ya wenye zambi.
42Musimame, tuende! Yule anayenitoa, amefika karibu!”
Kukamatwa kwa Yesu(Mat 26.47-56; Lk 22.47-53; Yn 18.3-12)43Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, mara moja Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akafika pamoja na kundi kubwa la watu wenye panga na magongo. Hawa wote walikuwa wametumwa na wakubwa wa makuhani, walimu wa Sheria, na wasimamizi wa watu.
44Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, alikuwa amekwisha kuwapa kitambulisho hiki: “Yule nitakayemubusu, ndiye yeye. Mumukamate na mumupeleke, mukimulinda vizuri.”
45Yuda alipofika, mara moja akamujongelea Yesu na kumwambia: “Mwalimu!” Kisha akamubusu.
46Basi wale watu wakamukamata Yesu na kumufunga.
47Lakini mumoja kati ya wale waliokuwa pale, akachomoa upanga wake na kumukata mutumishi wa Kuhani Mukubwa sikio.
48Kisha Yesu akawaambia: “Mumekuja na panga na magongo kwa kunikamata kama watu wanavyokwenda kumukamata munyanganyi?
49Siku zote nilikuwa pamoja nanyi, nami nilifundisha ndani ya hekalu, nanyi hamukunikamata. Lakini mambo haya yamefanyika kusudi Maandiko Matakatifu yatimizwe.”
50Wanafunzi wake wote wakamwacha na kukimbia.
51Lakini kijana mumoja aliyevaa shuka akaendelea kumufuata Yesu. Walijaribu kumukamata,
52lakini akaachilia shuka ile na kukimbia uchi.
Yesu mbele ya Baraza Kubwa(Mat 26.57-68; Lk 22.54-55,63-71; Yn 18.13-14,19-24)53Wakamupeleka Yesu mbele ya Kuhani Mukubwa, nao wakubwa wote wa makuhani, na wasimamizi wa watu pamoja na walimu wa Sheria wakakusanyika pale.
54Petro akamufuata Yesu kwa mbali, hata akaingia ndani ya upango wa nyumba ya Kuhani Mukubwa. Pale akaikaa pamoja na walinzi, akiota moto.
55Wakubwa wa makuhani na wakubwa wote wa Baraza Kubwa walitafuta mashitaki juu ya Yesu kusudi wapate kumwua, lakini hawakupata neno.
56Watu wengi walimushuhudia uongo, lakini ushuhuda wao haukupatana.
57Hata wengine wakasimama kwa kutoa ushuhuda huu wa uongo juu yake wakisema:
58“Sisi tulimusikia akisema: ‘Mimi nitabomoa hekalu hili lililojengwa na watu, na katika siku tatu nitajenga lingine lisilojengwa na watu.’ ”
59Lakini hata hivi ushuhuda wao haukupatana.
60Basi Kuhani Mukubwa akasimama katikati ya watu na kumwuliza Yesu: “Haujibu hata neno? Watu hawa wanakushitakia nini?”
61Lakini Yesu akanyamaza, wala hakujibu neno. Kuhani Mukubwa akamwuliza tena: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu mwenye sifa?”
62Yesu akajibu: “Mimi Ndiye! Nanyi mutamwona Mwana wa Mutu akiikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu Mwenye Uwezo. Mutamwona vilevile akikuja katika mbingu katikati ya mawingu!”
63Wakati Kuhani Mukubwa aliposikia maneno haya, akapasua nguo zake, na kusema: “Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu ya mutu huyu.
64Mumesikia wenyewe jinsi alivyomutukana Mungu. Munawaza nini?”
Wote wakamuhukumu kwamba anastahili kufa.
65Wengine katikati yao wakaanza kumutemea Yesu mate, wakamufunika uso na kumupiga ngumi, wakimwambia: “Tambua sasa ni nani aliyekupiga!” Nao waaskari walinzi wakamukamata Yesu na kumupiga makofi.
Petro anamukana Yesu(Mat 26.69-75; Lk 22.56-62; Yn 18.15-18,25-27)66Petro alipokuwa angali chini ndani ya upango, mumoja wa watumishi wanawake wa Kuhani Mukubwa akafika pale.
67Alipomwona Petro akiota moto, akamwangalia, na kumwambia: “Wewe vilevile ulikuwa pamoja na Yesu wa Nazareti.”
68Lakini Petro akakana, akisema: “Sijui wala sifahamu maneno unayotaka kusema.” Kisha akatoka inje ya upango na kwenda kwenye kiingilio cha mulango.
69Yule mutumishi mwanamuke akamwona pale, akaanza tena kuwaambia wale waliokuwa pale: “Huyu mutu ni mumoja wao!”
70Lakini Petro akakana tena.
Nyuma kidogo, watu wale wakamwambia Petro tena: “Hakika wewe ni mumoja wao, kwa sababu wewe vilevile ni wa Galilaya.”
71Basi Petro akaanza kusema: “Nilaaniwe ikiwa ninasema uongo! Ninaapa kwamba simujui mutu huyu munayemutaja.”
72Mara moja jogoo akawika kwa mara ya pili, na Petro akakumbuka maneno yale Yesu aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika mara mbili, atakuwa amemukana mara tatu. Basi akaanza kulia.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.