Matendo ya Mitume 14 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Paulo na Barnaba wanahubiri katika muji Ikonio

1Paulo na Barnaba walipofika katika muji Ikonio, wakaingia vilevile katika nyumba ya kuabudia ya Wayuda. Mule wakahubiri hata kundi kubwa la Wayuda na mataifa mengine wakaamini.

2Lakini Wayuda waliokataa kuamini walishawishi watu wa mataifa mengine na kuwasukuma kuwachukia wandugu waamini.

3Paulo na Barnaba wakakaa Ikonio kwa muda murefu. Walisema kwa uhodari kabisa, wakimutumainia Bwana. Naye aliwapa uwezo wa kufanya maajabu na vitambulisho. Na kwa njia hiyo alihakikisha kwamba ujumbe walioutangaza juu ya neema yake ulikuwa wa kweli.

4Watu wa muji wakatengana: wamoja walikuwa upande wa Wayuda na wengine upande wa mitume.

5Kisha Wayuda wamoja na watu wa mataifa mengine pamoja na wakubwa wao, wakakusudia kuwatendea mitume vibaya na kuwaua kwa kuwatupia mawe.

6Paulo na Barnaba walipotambua jambo lile wakakimbilia katika muji wa Listra na wa Derbe ndani ya wilaya ya Likaonia na katika sehemu za kandokando yake.

7Kule wakaendelea kuhubiri Habari Njema.

Paulo na Barnaba wanahubiri katika muji Listra

8Kule Listra kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa kiwete tangia kuzaliwa. Yeye hakuweza kusimama wala kupima kutembea.

9Yeye alikuwa akisikiliza mahubiri ya Paulo. Paulo akamukazia macho, naye akaona kwamba kiwete yule yuko na imani ya kuweza kuponyeshwa.

10Halafu akamwambia kwa sauti: “Simama wima!”

Mutu yule akaruka akasimama na kuanza kutembea.

11Wakati makundi ya watu walipoona jambo lile Paulo alilofanya, wakasema kwa sauti katika luga yao ya kilikaonia: “Miungu imetushukia ikiwa na sura ya kimutu!”

12Walimupanga Barnaba jina la mungu Zeu, na Paulo jina la mungu Herme, kwa sababu yeye ndiye aliyetoa hotuba.

13Naye kuhani wa hekalu la mungu Zeu, lililokuwa kwenye kiingilio cha muji, akaleta ngombe waliopambwa na mafungu za maua mbele ya mulango. Maana yeye pamoja na kundi la watu walitaka kuwatolea wale mitume sadaka ya nyama wenye kuchinjwa.

14Lakini Barnaba na Paulo waliposikia habari ile, wakapasua nguo zao kwa huzuni, wakaingia haraka katikati ya kundi la watu, na kusema kwa sauti:

15“Wandugu, kwa sababu gani munafanya mambo kama haya? Sisi vilevile ni watu, tuko sawasawa nanyi, na tunawahubiri ninyi Habari Njema kwamba muache kuabudu vitu hivi vya bure na mumugeukie Mungu mwenye uzima; yeye aliyeumba mbingu na dunia, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yao.

16Katika siku zilizopita Mungu aliwaachilia watu wa mataifa yote wafuate njia wanazotaka.

17Ingawa vile hakuacha kujijulisha kwa njia ya kutenda mema. Anawanyeshea mvua toka mbingu, anawapa mavuno kwa wakati wake, anawapa chakula na kuwajaza na furaha.”

18Ijapokuwa mitume walisema maneno haya, ilikuwa vigumu kuzuiza makundi ya watu wasiwatolee sadaka.

19Kisha Wayuda wamoja wakakuja tokea katika muji wa Antiokia na wa Ikonio. Wakashawishi makundi ya watu wajiunge nao. Wakamutupia Paulo mawe na kumukokotea inje ya muji, wakizani kwamba amekwisha kufa.

20Lakini wanafunzi walipokuwa wakimuzunguka, akasimama na kurudi ndani ya muji. Kesho yake yeye pamoja na Barnaba wakaenda katika muji wa Derbe.

Paulo na Barnaba wanarudi katika muji wa Antiokia ya Suria

21Paulo na Barnaba walihubiri Habari Njema katika muji wa Derbe, na kupata wanafunzi wengi. Kisha wakarudi katika muji wa Listra, wa Ikonio na wa Antiokia ya Pisidia.

22Kule waliwajenga wanafunzi moyo na kuwatia nguvu wabakie katika imani wakiwaambia: “Ni sherti tupite katika mateso mengi kwa kuweza kuingia katika Ufalme wa Mungu.”

23Wakawachagua wazee katika kila kanisa. Na kisha kuomba na kufunga kula chakula, wakawaweka chini ya ulinzi wa Bwana waliyemwamini.

24Kisha wakapitia katika jimbo la Pisidia na kufika katika inchi ya Pamfilia.

25Walipokwisha kuhubiri Neno la Mungu kwa watu wa muji Perga, wakaenda katika muji wa Atalia.

26Na kutoka kule wakarudi mpaka Antiokia kwa njia ya chombo. Ni kule walipokuwa wameombewa neema kwa Mungu kwa ajili ya kazi ile waliyotoka kutimiza.

27Walipofika Antiokia, wakafanya mukutano wa kanisa na kuwaelezea mambo yote Mungu aliyofanya kwa njia yao, na namna alivyowafungulia watu wa mataifa mengine mulango kusudi wao vilevile wapate kuamini.

28Nao wakakaa kule Antiokia kwa muda wa siku nyingi pamoja na wanafunzi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help