1 Wafalme 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Daudi anamupa Solomono maagizo

1Daudi alipokaribia kufa, alimwita mwana wake Solomono, akamupa maagizo akisema:

2“Mwana wangu, kama inavyokuwa kawaida kwa viumbe vyote kufa, siku zangu zimekwisha. Ukuwe imara na hodari.

3Timiza maagizo ya Yawe, Mungu wako, ufuate njia zake na kushika masharti yake, amri zake, maagizo yake na maamuzi yake kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa. Kwa hiyo, utafanikiwa katika kila jambo unalofanya na kokote unakoenda.

4Naye Yawe atatimiza ahadi yake aliyotoa aliponiambia kwamba, ikiwa wazao wangu watatii amri zake na kumutumikia kwa uaminifu na kwa moyo wote, hakutakosekana mumoja wao kwa kutawala Israeli nyakati zote.

5“Zaidi ya hayo, unajua vilevile yale Yoabu mwana wa Zeruya aliyonitendea, jinsi alivyowatendea majemadari wawili wa waaskari wa Israeli, Abeneri mwana wa Neri, na Amasa mwana wa Yeteri. Aliwaua wakati wa amani akitaka kulipiza kisasi kwa mauaji waliyofanya wakati wa vita. Aliwaua watu wasiokuwa na kosa, nami nikabeba lazima ya kifo cha watu wale kwa ajili ya vitendo vyake.

6Basi, wewe fanya kadiri ya hekima yako, lakini tu usimwache akufe kwa amani.

7“Lakini uwatendee mema wana wa Barzilayi, yule Mugileadi, wakuwe kati ya wale wanaokula kwenye meza yako, kwa sababu walinitendea mema wakati nilipomukimbia ndugu yako Abusaloma.

8Vilevile, kuko Simei mwana wa Gera, wa kabila la Benjamina wa muji wa Bahurimu, ambaye aliniapiza na kunilaani vikali nilipokwenda kule Mahanaimu; lakini alipokuja kunipokea kwenye muto Yordani, nilimwapia kwa jina la Yawe nikimwambia: ‘Sitakuua kwa upanga.’

9Lakini wewe usimwache bila kumwazibu. Una hekima, utajua utakalomufanyia. Ingawa yeye ana imvi, usimwache. Umwue ingawa ni muzee.”

Kifo cha Daudi

10Daudi akakufa na kuzikwa katika muji wake.

11Alikuwa ametawala inchi ya Israeli kwa muda wa miaka makumi ine; miaka saba akiwa Hebroni, na miaka makumi tatu na mitatu akiwa Yerusalema.

12Basi, Solomono akaikaa katika kiti cha kifalme kwa pahali pa baba yake Daudi, na ufalme wake ukaimarika.

13Nyuma, Adonia mwana wa Hagiti, alimwendea Batiseba, mama ya Solomono. Batiseba akamwuliza: “Unaleta habari ya amani?”

Adonia akamujibu: “Ndiyo, ninaleta habari ya amani.

14Lakini, nina jambo moja tu la kukuambia.”

Batiseba akamwambia: “Sema tu.”

15Adonia akamwambia: “Unajua kwamba ni mimi ndiye ningalikuwa mufalme, na hata Israeli yote ilikuwa inanitazamia nikuwe mufalme. Lakini, mambo yakageuka na ndugu yangu akanipindua, kwa sababu hayo ndiyo yaliyokuwa mapenzi ya Yawe.

16Sasa, nina ombi moja tu ambalo ninakusihi usinikatalie.”

Batiseba akamwambia: “Sema tu.”

17Naye akasema: “Tafazali, ninakusihi umwombe mufalme Solomono aniruhusu nimukamate Abisagi, yule Musunami, akuwe muke wangu, kwa maana ninajua hatakukatalia wewe.”

18Batiseba akamwambia: “Sawa; nitazungumuza na mufalme kwa jina lako.”

19Basi, Batiseba akamwendea mufalme Solomono kwa kumwelezea ombi la Adonia. Mufalme akasimama kwenda kumupokea mama yake, akainama mbele yake. Halafu, akaikaa katika kiti chake cha kifalme, akaagiza mama yake aletewe kiti, naye akaikaa kwa upande wa kuume wa mufalme.

20Batiseba akasema: “Nina ombi dogo tafazali ulikubali, na ninakuomba usinikatalie.”

Mufalme akamwambia: “Sema ombi lako mama yangu, kwa sababu sitakukatalia.”

21Naye akasema: “Umuruhusu ndugu yako Adonia amwoe Abisagi, yule Musunami.”

22Mufalme Solomono akamwuliza mama yake: “Kwa nini unataka nimupe Abisagi? Hii ni sawa kabisa na kumutakia ufalme wangu! Kumbuka kwamba yeye ni mukubwa yangu, na si ile tu, kuhani Abiatari na jemadari Yoabu mwana wa Zeruya, wako upande wake!”

23Hapo mufalme Solomono akaapa kwa jina la Yawe, akisema: “Mungu aniue ikiwa Adonia hatakufa kwa sababu ya kutoa ombi hili!

24Sasa basi, kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyeniweka na kuniimarisha katika ufalme wa baba yangu Daudi na kutimiza ahadi yake ya kunipa kiti cha kifalme mimi na wazao wangu, Adonia atakufa leo!”

25Halafu mufalme Solomono akatoa amri kwa Benaya mwana wa Yehoyada; naye akamwendea Adonia, akamwua.

Abiatari anafukuzwa; Yoabu anauawa

26Mufalme Solomono akamwambia kuhani Abiatari: “Ondoka uende katika shamba lako, kule Anatoti. Unastahili kufa wewe. Lakini sasa, sitakuua kwa sababu ulilishugulikia Sanduku la Agano la Yawe ulipokuwa na baba yangu Daudi, ukateswa pamoja naye.”

27Basi, mufalme Solomono akamufukuza Abiatari, asikuwe kuhani wa Yawe. Hivyo likatimia neno alilosema Yawe kule Shilo, juu ya Eli na ukoo wake.

28Yoabu alipopata habari, alikimbilia katika hema ya Mungu na kushikilia pembe za mazabahu kwa maana alikuwa amemwunga Adonia mukono ingawa mbele hakukuwa na Abusaloma.

29Mufalme Solomono aliposikia kwamba Yoabu yuko katika hema la Mungu na kwamba amesimama kwenye mazabahu, alimutuma Benaya mwana wa Yehoyada, akisema: “Kwenda umupige.”

30Basi, Benaya akaenda katika hema la Mungu, akamwambia Yoabu: “Mufalme ameamuru utoke inje.”

Yoabu akajibu: “Mimi sitatoka; nitakufia hapahapa.”

Benaya akarudi kwa mufalme na kumwelezea jinsi Yoabu alivyojibu.

31Solomono akasema: “Fanya sawa alivyosema. Umwue na kumuzika. Hivyo, mimi na wazao wengine wote wa Daudi hatutabeba lazima ya vitendo vya Yoabu vya kuwaua watu wasiokuwa na kosa.

32Mungu atamwazibu Yoabu kwa mauaji hayo aliyoyafanya bila baba yangu kuwa na habari. Yeye aliwaua watu wawili ambao walikuwa wa maana zaidi kuliko yeye, tena walimupita kwa wema; aliwaua Abeneri mwana wa Neri, jemadari wa kundi la waaskari Waisraeli, na Amasa mwana wa Yeteri, jemadari wa waaskari wa Yuda.

33Azabu ya mauaji hayo itakuwa juu ya Yoabu na wazao wake milele. Lakini Yawe atawabariki siku zote Daudi na wazao wake watakaoikalia kiti chake cha kifalme.”

34Basi, Benaya mwana wa Yehoyada akaenda katika hema, akamwua Yoabu ambaye alizikwa katika shamba lake, katika mbuga.

35Mufalme akamuweka Benaya mwana wa Yehoyada kuwa jemadari wa kundi la waaskari kwa pahali pa Yoabu, na Zadoki akakuwa kuhani pahali pa Abiatari.

Kifo cha Simei

36Halafu mufalme akaagiza Simei aitwe, akamwambia: “Ujijengee nyumba humu Yerusalema, ukae hapa bila kwenda pahali pengine popote.

37Maana siku utakapotoka na kuvuka kijito Kidroni, ninakuambia kweli utakufa na kubeba lazima ya kifo chako wewe mwenyewe.”

38Simei akajibu: “Ni vizuri, mufalme. Nitafanya kama ulivyosema.” Basi, akakaa Yerusalema kwa muda murefu.

39Lakini kwa mwisho wa mwaka wa tatu, watumwa wawili wa Simei walitoroka, wakaenda kwa Akisi mwana wa Maka, mufalme wa Gati. Habari zilipomufikia kwamba wako Gati,

40Simei alipanda juu ya punda wake, akaenda kule kwa kuwatafuta, kwa mufalme Akisi. Basi, akafika, akawapata, akawarudisha kwake.

41Mufalme Solomono alipopata habari kwamba Simei alikuwa ametoka Yerusalema, akaenda Gati na kurudi,

42alimwita Simei na kumwambia: “Si wewe ndiwe uliniapia kwa jina la Yawe kwamba hautatoka Yerusalema? Nami si nilikuonya kwamba hakika utakufa kama ukisubutu kwenda inje? Nawe ulikubali, ukaniambia: ‘Ni vizuri, nitatii’.

43Mbona basi, umevunja kiapo chako kwa Yawe na kutojali amri niliyokupa?”

44Mufalme aliendelea kumwambia Simei: “Unayajua wazi maovu uliyomutendea baba yangu Daudi. Sasa, kwa sababu ya hayo, Yawe atakuazibu.

45Lakini mimi atanibariki, na kiti cha kifalme cha Daudi kitaimarishwa mbele ya Yawe milele.”

46Hapo, mufalme akamwamuru Benaya mwana wa Yehoyada, naye akatoka, akamupiga na kumwua Simei. Basi, ufalme ukaimarika chini ya Solomono.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help