Yeremia 46 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Yawe akamutolea Yeremia ujumbe juu ya watu wa mataifa.

Neno la Yawe juu ya Misri

2Juu ya Misri na jeshi la Neko mufalme wa Misri, lililokuwa huko Karkemisi karibu na muto Furati ambalo Nebukadneza mufalme wa Babeli alilishambulia katika mwaka wa ine wa utawala wa Yoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda:

3Mutayarishe ngao ndogo na kubwa

musonge mbele kwa kupigana vita.

4Mutandike farasi na kupanda juu yao.

Mushike nafasi zenu, na muvae kofia za chuma.

Munoe mikuki yenu, muvae nguo zenu za chuma.

5Lakini mbona ninawaona wametishwa?

Wamerudi nyuma.

Mashujaa wao wamepigwa,

wamekimbia mbio,

bila hata kuangalia nyuma.

Kuna kitisho kila upande.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

6Wanaokuwa wepesi hawawezi kutoroka,

mashujaa hawawezi kukwepa;

huko kaskazini kwenye muto Furati

wamejikwaa na kuanguka.

7Nani huyo anayekuwa kama muto Nili uliofurika,

kama mito inayovumisha mawimbi?

8Misri ni kama muto Nili uliofurika,

kama mito inayovumisha mawimbi.

Ilisema: Nitajaa, nitaifunika inchi,

nitaiharibu miji na wakaaji wake.

9Musonge mbele, enyi farasi;

mushambulie, enyi magari ya vita.

Mashujaa wasonge mbele:

watu wa Etiopia na Puti wanaoshika ngao,

watu wa Ludi, wafundi wa kutumia pinde.

10Lakini siku hiyo ni siku ya Bwana wetu Yawe wa majeshi.

Ni siku ya kulipiza kisasi,

siku ya kuwaazibu waadui zake.

Upanga utawamaliza hao na kutosheka,

utaikunywa damu yao na kushiba.

Maana Bwana wetu Yawe wa majeshi yuko na sadaka

huko kaskazini karibu na muto Furati.

11Mupande Gileadi, enyi watu wa Misri,

kwa kutafuta dawa.

Mumetumia dawa nyingi bure;

hakuna kitakachowaponyesha ninyi.

12Mataifa yamesikia jinsi mulivyopata haya,

kilio chenu kimeenea katika dunia yote;

mashujaa wamegongana wenyewe kwa wenyewe,

wote pamoja wameanguka.

13Hili ndilo neno ambalo Yawe alimwambia Yeremia wakati Nebukadneza mufalme wa Babeli alipofika kuishambulia inchi ya Misri:

14Tangaza katika inchi ya Misri,

uijulishe huko Migidoli,

uijulishe huko Nofi na Tapanesi.

Uwaambie: Mukae tayari kabisa

maana upanga utawaangamiza kila nafasi.

15Kwa nini shujaa wako amekimbia?

Mbona ngombe dume wako hakuweza kuvumilia?

Kwa sababu mimi Yawe nilimwangusha chini!

16Wengi walijikwaa, wakaanguka,

kisha wakaambiana wao kwa wao:

Musimame, tuwaendee watu wetu,

turudi katika inchi yetu,

tuukimbie upanga wa adui.

17Naye Mufalme wa Misri, mumupange jina hili:

Mwenye domo ya bure!

18Kama vile ninavyoishi,

–ni ujumbe wa mufalme, jina lake Yawe wa majeshi–

kweli adui anakuja kuwashambulia:

ni hakika kama vile Tabori unavyokuwa mulima,

kama vile mulima Karmeli unavyoonekana kutoka katika bahari.

19Enyi wakaaji wa Misri,

mujitayarishe na mizigo kwenda katika uhamisho!

Maana muji wa Nofi utaharibiwa kabisa,

utakuwa mabomoko yasiyokaliwa na watu.

20Misri ni kama mwana-ngombe muzuri,

lakini uharibifu kutoka kaskazini umekuja juu yake.

21Hata waaskari wake wa mushahara ni kama wana-ngombe wanono;

nao tena wamegeuka, wakakimbia pamoja,

wala hawakuweza kuvumilia,

kwa maana siku yao ya kuangamizwa imefika,

wakati wao wa kuazibiwa umetimia.

22Misri anatoroka bila fujo kama nyoka anayekimbia;

maana waadui zake wanamufikia kwa nguvu,

wanamufikia kwa mashoka kama wakata miti.

23Watakata kabisa pori lake, ingawa halipenyeki.

–Ni ujumbe wa Yawe–

maana wao ni wengi kuliko nzige wasiohesabika.

24Watu wa Misri watapata haya,

watatiwa katika mikono ya watu kutoka kaskazini.

25Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, alisema: Mimi nitamwazibu Amoni mungu wa muji wa Tebesi, nitaiazibu Misri na miungu yake na wafalme wake, nitamwazibu Mufalme wa Misri na wote wanaomutegemea.

26Nitawatia katika mikono ya wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao, ni kusema Nebukadneza mufalme wa Babeli na wakubwa wake. Kisha, inchi ya Misri itakaliwa na watu kama ilivyokuwa hapo zamani.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Yawe atawaokoa watu wake

27Lakini wewe usiogope, ee Yakobo mutumishi wangu,

usifazaike, ee Israeli,

maana nitakuokoa kutoka mbali,

nitakuja kuwaokoa wazao wako

kutoka inchi walimohamishiwa.

Yakobo utarudi na kutulia na kustarehe,

wala hakuna yeyote atakayekutia hofu.

28Usiogope, ee Yakobo mutumishi wangu,

kwa maana mimi niko pamoja nawe.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Nitayaangamiza kabisa mataifa yote

ambayo nimekutawanya kati yao,

lakini wewe sitakuangamiza.

Nitakuazibu kadiri unavyostahili,

sitakuacha bila kukuazibu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help