ZAKARIA 14 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yerusalema na watu wa mataifa mengine

1Angalia, siku ya kasirani ya Yawe inakuja. Siku hiyo, enyi watu wa Yerusalema, mali yenu itagawanywa mbele ya macho yenu.

2Yawe atayakusanya mataifa yote kwa kuushambulia Yerusalema. Muji utakamatwa, nyumba zenu zitatekwa, na wanawake wenu watakamatwa kwa kinguvu. Nusu ya wakaaji wa muji watapelekwa katika uhamisho, lakini nusu itakayobaki haitaondoshwa inje ya muji.

3Kisha Yawe atatoka na kuyapiga vita mataifa hayo, kama vile anavyofanya siku zote wakati wa vita.

4Siku hiyo, atasimama kwenye mulima wa Mizeituni unaokuwa upande wa mashariki wa Yerusalema. Mulima ule utagawanywa kwa sehemu mbili na bonde pana litatokea toka upande wa mashariki mpaka wa magaribi. Nusu moja itaelekea upande wa kaskazini na nusu ingine kusini.

5Ninyi mutakimbia kupitia bonde lile, katikati ya milima miwili ya Yawe. Mutakimbia kama vile babu zenu walivyokimbia tetemeko la inchi wakati wa utawala wa mufalme Uzia wa Yuda. Kisha Yawe, Mungu wangu, atakuja na watakatifu wote pamoja naye.

6Wakati ule hakutakuwa baridi wala baridi kali.

7Muchana utaendelea bila giza kuingia. Wakati huo unajulikana kwa Yawe peke yake. Hakutakuwa muchana wala usiku, kwa maana hata saa za magaribi mwangaza utaendelea kuwa.

8Wakati ule, maji ya uzima yatabubujika kutoka Yerusalema, na nusu ya maji yale yatatiririkia kwenye bahari ya mashariki, na nusu ingine kwenye bahari ya magaribi. Maji yale yataendelea kububujika wakati wa kipwa kama yanavyokuwa wakati wa mvua.

9Wakati huo, Yawe atakuwa ndiye mufalme pekee wa dunia yote; naye atakuwa ndiye Yawe pekee, mumoja tu, na jina lake litakuwa ndilo jina pekee.

10Inchi yote, tangu Geba mpaka Rimoni, upande wa kusini wa Yerusalema, itageuzwa kuwa mbuga yenye kunyooka kabisa. Lakini Yerusalema utabaki juu pahali pake tokea mulango wa Benjamina mpaka kwenye mulango wa zamani, hata kwenye mulango wa Konani, tangu munara wa Hanameli mpaka kwenye kikamulio cha mufalme.

11Muji Yerusalema utakaliwa na watu maana ndani yake hakutakuwa laana tena; watu watakaa kule kwa usalama.

12Lakini juu ya wale watu ambao walikuja kupigana na Yerusalema, hizi ndizo hasara ambazo Yawe atawaletea: Miili yao itaoza wangali wazima; macho yao yataoza yakiwa kwenye matundu yake na ndimi zao zitaoza zikiwa katika vinywa vyao.

13Siku ile, hofu kutoka kwa Yawe itawapata watu, na kila mutu atamushambulia mwenzake.

14Watu wa Yuda watapigana kwa kuulinda Yerusalema; utajiri wa mataifa yote yanayoizunguka inchi ya Yuda utakusanywa: watakusanya zahabu, feza na nguo kwa wingi sana.

15Hasara kubwa zitapata farasi, nyumbu, ngamia, punda na nyama wote watakaokuwa katika kambi zile za waadui.

16Kisha, kila mutu aliyebaki kati ya mataifa yote yaliyokuja kuushambulia Yerusalema, atakuwa akikuja Yerusalema mwaka kwa mwaka, kwa kumwabudu Yawe wa majeshi anayekuwa mufalme, na kushiriki kwa sikukuu ya Vibanda.

17Ikiwa kuna taifa lolote katika dunia ambalo halitakwenda Yerusalema kumwabudu Yawe wa majeshi anayekuwa mufalme, basi, mvua haitanyesha katika inchi yao.

18Ikiwa Wamisri watakataa kushiriki kwa sikukuu ya Vibanda, basi, Yawe atawapiga kwa ugonjwa uleule atakaowapiga nao mataifa yote yanayokataa kushiriki kwa sikukuu hiyo.

19Hiyo itakuwa ndiyo azabu itakayolipata taifa la Misri pamoja na mataifa yote yasiyoshiriki kwa sikukuu ya Vibanda.

20Wakati ule, kwenye kengele za farasi kutaandikwa maandiko haya: “Vimetolewa kwa Yawe.” Vyungu vinavyokuwa katika hekalu la Yawe vitakuwa kama mabakuli yanayokuwa mbele ya mazabahu.

21Kila chungu katika Yerusalema na inchi ya Yuda kitatolewa kwa Yawe wa majeshi, kusudi wote wanaotoa sadaka waweze kuvitumia kwa kupikia nyama ya sadaka. Wakati ule, hakutakuwa muchuuzi yeyote katika hekalu la Yawe wa majeshi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help