Matayo 21 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yesu anaingia Yerusalema(Mk 11.1-11; Lk 19.28-40; Yn 12.12-19)

1Yesu na wanafunzi wake wakakaribia kufika Yerusalema upande wa kijiji cha Betefage, karibu na mulima wa Mizeituni. Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake,

2akawaambia: “Mwende katika kijiji kinachokuwa mbele yenu. Wakati mutakapofika kule, mara moja mutaona punda amefungwa na mwana-punda akiwa pamoja naye. Muwafungue na kuwaleta.

3Na kama mutu akiwauliza neno, mumwambie kama Bwana yuko na lazima ya kuwatumia. Na mara moja mutu yule atawaruhusu kuwapeleka.”

4Mambo hayo yote yalitokea, kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii:

5“Muwaambie wakaaji wa muji Sayuni:

‘Angalia, mufalme wenu anakuja kwenu.

Yeye ni munyenyekevu, amepanda juu ya punda,

juu ya mwana-punda, kitoto cha punda.’ ”

6Basi wale wanafunzi wakaenda, nao wakafanya sawa Yesu alivyowaagiza.

7Wakaleta punda pamoja na mwana-punda, wakatandika nguo juu yao na Yesu akaikaa juu ya nguo zile.

8Watu wengi wakatandika nguo zao katika njia, na wengine wakakata matawi ya miti na kuyatandika katika njia vilevile.

9Nalo kundi la watu waliomutangulia Yesu na lile la watu waliofuata nyuma yake, wakaanza kulalamika, wakisema: “Usifiwe wewe Mwana wa Daudi! Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana! Mungu asifiwe juu mbinguni!”

10Yesu alipoingia Yerusalema, muji wote ukavuma. Watu wakaulizana: “Huyu ni nani?”

11Kundi la watu wakajibu: “Huyu ni nabii Yesu wa Nazareti katika Galilaya.”

Yesu anatakasa hekalu(Mk 11.15-19; Lk 19.45-48; Yn 2.13-22)

12Yesu akaingia ndani ya hekalu, naye akawafukuza watu wote waliokuwa wakiuzishia na kununulia vitu vyao ndani yake. Akapindua meza za wale waliobadilisha feza na viti vya wachuuzi wa njiwa.

13Akawaambia: “Imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya maombi.’ Lakini ninyi mumeigeuza kuwa nafasi ya makutano ya wanyanganyi!”

14Vipofu na viwete wakamufikia Yesu kule ndani ya hekalu, naye akawaponyesha.

15Lakini wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria wakachukizwa kwa kuona miujiza aliyoifanya na watoto waliokuwa wakilalamika katika hekalu, wakisema: “Usifiwe wewe, mwana wa Daudi!”

16Basi wakamwuliza Yesu: “Unasikia maneno watoto hawa wanayoyasema?”

Yesu akawajibu: “Ndiyo. Lakini hamujasoma Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Kwa vinywa vya watoto wadogo hata wale wanaokuwa wachanga umetangaza sifa zako.’ ”

17Kisha akawaacha, akatoka inje ya muji wa Yerusalema, naye akaenda Betania na kulala kule.

Yesu analaani muti wa matunda ya tini(Mk 11.12-14,20-24)

18Kesho yake asubui, Yesu alipokuwa akirudia Yerusalema, akasikia njaa.

19Akaona muti wa tini pembeni ya njia, akaenda karibu nao, lakini hakuona kitu juu yake isipokuwa majani matupu. Halafu Yesu akaulaani muti ule akisema: “Wewe usitoe tena matunda tangu leo hata milele!”

Na pale pale muti ule ukakauka.

20Wanafunzi walipoona jambo hilo, wakashangaa sana na kujiuliza: “Namna gani muti huu umekauka mara moja?”

21Yesu akawajibu: “Kweli ninawaambia: mukimwamini Mungu pasipo kuwa na shaka, hamutaweza kufanya tu kama nilivyotendea muti huu, lakini vilevile mutaweza kuuambia mulima huu: ‘Ondoka hapa, ujitupe katika bahari,’ na itakuwa vile.

22Na kitu chochote mutakachoomba, mukiamini, mutakipata.”

Mamlaka ya Yesu yanatoka wapi?(Mk 11.27-33; Lk 20.1-8)

23Yesu akaingia ndani ya hekalu. Alipokuwa akifundisha, wakubwa wa makuhani pamoja na wasimamizi wa watu wakamufikia na kumwuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Ni nani aliyekupa mamlaka yale?”

24Yesu akawajibu: “Nitawauliza ulizo moja tu. Kama mukinijibu, mimi vilevile nitawaambia ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.

25Yoane alipata mamlaka ya kubatiza kutoka kwa nani? Kwa Mungu au kwa watu?”

Nao wakaanza kupiga mafikiri pamoja na kusema: “Kama tukijibu kwamba mamlaka yake yalitoka kwa Mungu, atatuuliza: ‘Kwa sababu gani basi hamukumwamini?’

26Lakini vilevile kwa kuwa tunaogopa watu hawa, hatuwezi kusema kwamba yalitoka kwa mutu; kwa maana watu hawa wote wanasadiki kwamba Yoane alikuwa nabii.”

27Basi wakamujibu Yesu: “Hatujui.”

Naye akawaambia: “Nami vilevile sitawaambia ninyi ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.”

Mufano wa watoto wawili

28Yesu akaongeza kusema: “Ninyi munafikiri nini juu ya habari hii? Kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa na watoto wawili. Yeye akamwambia mutoto wa kwanza: ‘Mutoto wangu, ninataka uende leo kutumika katika shamba langu la mizabibu.’

29Naye akamujibu: ‘Sitaki.’ Lakini kisha akageuza nia yake na kwenda kutumika.

30Halafu yule baba akamwambia mutoto wa pili sawa vile alivyomwambia yule wa kwanza. Naye akamujibu: ‘Ndiyo, baba,’ lakini hakwenda.

31Kati ya hawa wawili ni nani aliyefanya sawa na mapenzi ya baba yake?”

Wale wakubwa wakajibu: “Ni yule wa kwanza.”

Na Yesu akawaambia: “Kweli ninawaambia: Walipishaji wa kodi pamoja na makahaba wataingia mbele yenu katika Ufalme wa Mungu.

32Kwa maana Yoane alikuja kwenu kuwaonyesha njia ya haki, nanyi hamukumusadiki. Lakini walipishaji wa kodi na makahaba walimusadiki. Na ijapokuwa muliona mambo hayo yote, hamukugeuka toka zambi zenu na kumusadiki.”

Mufano wa walimaji wabaya(Mk 12.1-12; Lk 20.9-19)

33“Musikilize mufano mwingine. Mutu mumoja alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha upango, akatengeneza nafasi ya kukamulia matunda ya mizabibu na kujenga munara kwa ajili ya walinzi wa shamba. Kisha kupatana kwa kugawanyana mavuno na walimaji wamoja watakaobaki wakitunza shamba lake, akaenda safari katika inchi ingine.

34Wakati siku za mavuno zilipotimia, akawatuma watumishi wake kwa wale walimaji kusudi wamupatie sehemu yake ya mavuno.

35Lakini wale walimaji wakawakamata wale watumishi. Wakamupiga mumoja, wakamwua mwingine na kumutupia mwingine mawe hata akakufa.

36Halafu mwenye shamba akatuma tena watumishi wengine wengi zaidi kuliko wale wa kwanza, lakini wale walimaji wakawatendea namna ile ile.

37Kwa mwisho, akamutuma mwana wake kwao, akisema: ‘Ninajua kwamba watamuheshimu mwana wangu.’

38Lakini wakati walimaji walipomwona yule mwana, wakasemezana: ‘Musimame! Huyu ndiye atakayerizi shamba hili. Basi tumwue, na shamba hili litakuwa urizi wetu!’

39Basi wakamukamata, wakamwua na kutupa maiti yake inje ya shamba.”

40Kisha Yesu akauliza: “Basi wakati mwenye shamba la mizabibu atakapokuja, atafanya nini na wale walimaji?”

41Nao wakamujibu: “Atawaua hao watu wabaya pasipo huruma, naye atapatana na walimaji wengine kwa kutunza shamba lake na kumupatia sehemu yake ya matunda kwa wakati wa mavuno.”

42Na Yesu akawaambia: “Hamujasoma bado Maandiko Matakatifu yanayosema:

‘Jiwe lililokataliwa na wajengaji

limekuwa jiwe kubwa la musingi.

Ni Bwana aliyefanya jambo hili,

nalo ni ajabu sana kwetu.’

43Kwa sababu hii ninawaambia: Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu na kupewa kwa watu watakaotoa matunda yanayostahili ufalme ule.”

45Wakubwa wa makuhani na Wafarisayo waliposikia mifano hiyo Yesu aliyoitumia, wakatambua kwamba alisema juu yao.

46Kwa hiyo wakatafuta kumukamata, lakini waliogopa makundi ya watu kwa sababu wao walisadiki kwamba yeye ni nabii.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help