1Nyuma ya siku chache, Yesu akarudi Kapernaumu, na watu wakasikia kwamba yuko ndani ya nyumba.
2Watu wengi wakakusanyika pale mpaka hapakukuwa tena nafasi ndani ya nyumba, hata inje mbele ya mulango. Yesu alipokuwa akiwahubiri Neno la Mungu,
3wakamuletea mugonjwa mwenye kupooza, akibebwa na watu wane.
4Lakini kwa kuona hawakuweza kumufikisha mbele ya Yesu kwa sababu ya uwingi wa watu, wakabomoa dari juu ya pahali Yesu alipokuwa. Kisha wakamushusha yule mwenye kupooza kwenye nafasi ile walipobomoa, akilala juu ya kipoyi chake.
5Yesu alipoona namna walivyomwaminia, akamwambia yule mwenye kupooza: “Mutoto wangu, zambi zako zimesamehewa.”
6Walimu wamoja wa Sheria walioikaa pale wakajiuliza:
7“Namna gani mutu huyu anasubutu kumutukana Mungu? Ni nani anayeweza kusamehe zambi isipokuwa Mungu peke yake?”
8Mara moja Yesu akitambua mafikiri yao, akawauliza: “Sababu gani munajiuliza mambo hayo yote?
9Kitu gani kinachokuwa chepesi: kumwambia mutu mwenye kupooza ‘Zambi zako zimesamehewa’ au kumwambia ‘Simama, utwae kipoyi chako na utembee?’
10Basi, ninataka mujue kwamba Mwana wa Mutu yuko na mamlaka ya kusamehe zambi hapa katika dunia.”
Kwa hiyo akamwambia yule mutu mwenye kupooza:
11“Ninakuamuru, simama, utwae kipoyi chako na uende kwako!”
12Na watu wote walipokuwa wakimwangalia mutu yule, pale pale akasimama, akatwaa kipoyi chake na kujiendea. Wote wakashangaa, wakamusifu Mungu, wakisema: “Hatujaona mambo kama haya hata mara moja!”
Yesu anamwita Lawi amufuate(Mat 9.9-13; Lk 5.27-32)13Yesu akaenda tena pembeni ya ziwa la Galilaya. Kundi kubwa la watu wakamufikia, naye akawafundisha.
14Kisha alipokuwa akipita, akamwona Lawi mwana wa Alfayo, akiikaa katika nyumba ya kulipishia kodi. Yesu akamwambia: “Unifuate!”
Naye Lawi akasimama na kumufuata.
15Nyuma Yesu akaikaa kula chakula ndani ya nyumba ya Lawi. Walipishaji wengi wa kodi na watenda mabaya wengine waliikaa kula pamoja na Yesu na wanafunzi wake, kwa maana watu wengi wa namna ile walikuwa wamemufuata.
16Na wakati walimu wa Sheria wa kikundi cha Wafarisayo walipomwona Yesu akikula pamoja na watu wale, wakawauliza wanafunzi wake: “Kwa sababu gani anakula pamoja na walipishaji wa kodi na watenda mabaya?”
17Yesu alisikia vile walivyosema, na kwa hiyo akawaambia: “Wenye afya nzuri hawahitaji muganga, ni wale wanaokuwa wagonjwa tu. Sikukuja kuwaita wenye haki kunifuata, lakini watenda mabaya.”
Ulizo juu ya kafunga kula chakula(Mat 9.14-17; Lk 5.33-39)18Wanafunzi wa Yoane Mubatizaji na Wafarisayo walikuwa wakifunga kula chakula. Hivi watu wakakuja kumwuliza Yesu: “Sababu gani wanafunzi wa Yoane Mubatizaji na wanafunzi wa Wafarisayo wanafunga kula chakula, lakini wanafunzi wako hawafungi?”
19Yesu akawajibu: “Munafikiri kwamba wanaoalikwa kwa arusi wanaweza kujizuiza kula chakula cha karamu wakati bwana-arusi angali pamoja nao? Hapana! Wakati bwana-arusi angali pamoja nao hawawezi kujizuiza kula.
20Lakini kutakuwa siku bwana-arusi atakapoondoshwa kati yao; ni katika siku zile ndipo watafunga kula.
21“Hakuna mutu anayeshonea kiraka kipya juu ya nguo ya zamani. Kama akifanya vile, kile kiraka kipya kinapasua nguo ya zamani, nako kupasuka kwake kunaongezeka zaidi.
22Vilevile hakuna mutu anayetia divai mupya ndani ya machupa ya ngozi yenye kuzeeka. Kama akifanya vile, ile divai mupya itapasua machupa yale yenye kuzeeka, nayo divai na machupa vyote vinapotea bure. Lakini inafaa kutia divai mupya ndani ya machupa mapya ya ngozi.”
Yesu ni Bwana wa siku ya Sabato(Mat 12.1-18; Lk 6.1-5)23Siku moja ya Sabato Yesu akapita katika mashamba ya ngano. Wanafunzi wake wakaanza kuchumachuma masuke ya ngano kwa kadiri walivyoendelea katika njia.
24Basi Wafarisayo wakamwambia Yesu: “Sababu gani wanafunzi wako wanafanya jambo linalokatazwa kwa siku ya Sabato?”
25Yesu akawajibu: “Hamujasoma bado vile Daudi alivyofanya wakati alipohitaji chakula, kwa sababu yeye mwenyewe na watu wake walisikia njaa?
26Si aliingia ndani ya nyumba ya Mungu na kula mikate mitakatifu iliyotolewa kwa Mungu? Jambo hili lilifanyika wakati Abiatari alipokuwa Kuhani Mukubwa. Ni makuhani tu walioruhusiwa kula mikate ile, lakini Daudi alikula na kuwapa watu wake vilevile.”
27Yesu akaongeza kuwaambia: “Siku ya Sabato iliwekwa kwa ajili ya mafaa ya mutu, lakini mutu hakuumbwa kwa ajili ya siku ya Sabato.
28Ni kwa sababu hii, Mwana wa Mutu ndiye Bwana hata wa siku ya Sabato.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.