1Uwakumbushe watu wajinyenyekeze mbele ya watawala na wakubwa. Wanapaswa kuwatii na kuwa tayari kwa kufanya kila tendo zuri.
2Uwaambie wasiseme mabaya juu ya mutu, lakini wakuwe wenye kupenda amani na wema, na wenye kuonyesha upole mbele ya kila mutu.
3Kwa maana zamani sisi vilevile tulikuwa wajinga, waasi na wapotovu. Tulikuwa tumetawaliwa na kila namna ya tamaa mbaya na ya vitu mbalimbali vilivyotuvuta sana. Tuliishi katika uovu na wivu, tuliwachukiza watu nao walituchukia.
4Lakini wakati Mungu Mwokozi wetu alipoonyesha wema wake na upendo wake kwa watu,
5alituokoa sisi. Hakufanya vile kwa sababu ya matendo yetu ya haki, lakini alituokoa kwa sababu ya huruma yake kwa njia ya Roho Mutakatifu aliyetuwezesha kuzaliwa mara ya pili na kuwa na maisha mapya kwa kutusafisha kwa maji.
6Kwa maana Mungu amemimia Roho Mutakatifu kwa uwingi juu yetu kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi wetu.
7Ilifanyika vile, kusudi kwa neema yake tupate kuhesabiwa haki mbele ya Mungu na kuupata uzima wa milele tunaotumainia.
8Neno hilo ni la kuaminiwa.
Ninataka uyatilie maneno hayo mukazo, kusudi watu walioamini Mungu wajitolee kwa kuzidi kutenda mema. Jambo hilo ni zuri na lenye mafaa kwa watu.
9Lakini uepuke mabishano ya upumbafu, hadisi za vizazi vya babu, na magomvi pamoja na mapingano juu ya Sheria, kwa sababu mambo hayo hayana mafaa, nayo ni ya bure.
10Ujiepushe na mutu anayeleta matengano unapokwisha kumwonya mara mbili.
11Kwa maana unajua kwamba mutu kama huyo amepotoka, na zambi zake zinamuhukumu yeye mwenyewe.
12Wakati nitakapokutumia Artema au Tikiko, ufanye bidii sana kuja kukutana nami kule Nikopoli, kwa maana nimekusudia kukaa kule wakati wa baridi kali.
13Ujikaze upate kumusafirisha vizuri mwanasheria Zenasi pamoja na Apolo, kusudi wasikose kitu chochote wanachohitaji katika safari yao.
14Inafaa watu wetu vilevile wajifunze kuzidi kutenda mema kusudi wapate kutoa musaada kwa ajili ya mahitaji ya kweli. Na hivi maisha yao yatakuwa yenye mafaa.
15Watu wote wanaokuwa pamoja nami wanakusalimia. Unisalimie wapendwa wetu katika imani.
Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Mungu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.