Yobu 18 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kisha Bildadi, wa inchi ya Suhi, akajibu:

2Utawinda maneno ya kusema mpaka wakati gani?

Fikiri vizuri nasi tutasema.

3Kwa nini unatufanya kama ngombe?

Mbona unatuona sisi kuwa wapumbafu?

4Wewe unajirarua mwenyewe kwa hasira zako.

Dunia itaachwa tupu kwa ajili yako

au mawe yahamishwe toka pahali pake?

5Kweli, mwangaza wa mutu mwovu utazimishwa;

ulimi wa moto wake hautaangaa.

6Katika nyumba yake mwangaza ni giza,

taa inayomwangazia itazimishwa.

7Hatua zake ndefu zitafupishwa;

mipango yake itamwangusha chini.

8Miguu yake mwenyewe itamutia katika mutego;

kila mara anatembea juu ya shimo.

9Mutego unamukamata kwenye kisigino,

kamba inamunasa kabisa.

10Amefichiwa kamba ya kumunasa ndani ya udongo,

ametegewa mutego katika njia yake.

11Hofu kubwa inamutisha kila upande,

inamufuata katika kila hatua yake.

12Alikuwa na nguvu, lakini sasa njaa imemubana;

hasara ziko tayari kumwangusha.

13Ugonjwa mukali unakula ngozi yake,

ugonjwa wa kifo unaharibu viungo vyake.

14Anaongolewa katika nyumba aliyotegemea,

na kupelekwa kwa mufalme wa vitisho.

15Nyumba yake tupu, wengine wataishi ndani;

kiberiti kimetawanywa katika makao yake.

16Yeye ni kama muti uliokauka mizizi,

matawi yake juu yamenyauka.

17Katika inchi hakuna atakayemukumbuka;

jina lake halitatamkwa tena katika barabara.

18Ameondolewa toka katika mwangaza, akatupwa katika giza;

amefukuzwa mbali kutoka katika dunia.

19Hana watoto wala wajukuu;

hakuna aliyebaki katika makao yake.

20Watu wa upande wa magaribi wameshangazwa na yaliyomupata;

hofu imewapata watu wa upande wa mashariki.

21Hayo ndiyo yanayowapata wasiomujali Mungu;

pale ndipo pahali pa wasiomujua Mungu.

Jibu la Yobu
Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help