1Watu wakaanza kunungunika mbele ya Yawe juu ya taabu zao. Yawe akasikia, na hasira yake ikawaka. Moto toka kwa Yawe ukawaka kati yao na kuchoma upande mumoja wa kambi.
2Watu wakamulilia Musa, naye akamwomba Yawe na moto huo ukazimika.
3Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa Tabera, ni kusema “Kuchoma”, kwa sababu pale moto wa Yawe uliwaka kati ya watu.
Musa anachagua viongozi makumi saba4Kati ya Waisraeli kulikuwa kundi fulani lililoandamana nao ambalo lilikuwa na hamu kubwa ya kula nyama. Waisraeli wenyewe wakalia, wakisema: Heri kama tungeweza kupata nyama ya kula!
5Tunakumbuka, samaki tuliokula katika Misri bila malipo, maboga, matikiti, mboga, vitunguu na vitunguu sumu!
6Lakini sasa nguvu zimetuishia na hakuna chakula kingine isipokuwa hii mana tu!
7Mana ilikuwa kama mbegu ndogo zenye rangi ya kimanjano.
8Watu walizungukazunguka na kuikusanya, kisha waliisaga kwa mawe ya kusagia au waliitwanga katika vinu, halafu waliitokotesha ndani ya vyungu na kutengeneza maandazi. Onjo yake ilikuwa kama ya maandazi yaliyokaangwa kwa mafuta.
9(Umande ulipoanguka katika kambi wakati wa usiku, mana vilevile ilianguka pamoja na huo umande).
10Musa akasikia watu wakilia katika jamaa zote, kila mutu kwenye mulango wa hema lake. Basi, hasira ya Yawe ikawaka sana; naye Musa akachukizwa.
11Halafu Musa akamwambia Yawe: Kwa nini unanitendea vibaya mimi mutumishi wako? Mbona sikupata kukubaliwa mbele yako? Kwa nini umenibebesha muzigo wa kuwatunza watu hawa wote?
12Ni mimi ndiye niliyewazaa, hata ukaniambia niwabebe kwenye kifua changu kama mulezi anavyobeba mutoto muchanga, na kuwapeleka mpaka katika inchi uliyoapa kuwapa babu zao?
13Nitapata wapi nyama ya kuwakulisha watu hawa wote? Maana wanalia mbele yangu wakisema: Utupatie nyama tukule!
14Siwezi kuwatunza watu wote hawa peke yangu; kwa sababu ni muzigo muzito kwangu!
15Ikiwa hivi ndivyo utakavyonitendea, afazali uniue mara moja! Kama ninapata kukubaliwa mbele yako, usiniache kuendelea katika taabu yangu.
16Basi, Yawe akamwambia Musa: Uwakusanye wazee makumi saba wa Israeli, ambao wewe unajua wanaheshimiwa na kukubaliwa na watu kuwa viongozi, uwalete kwenye hema la mukutano, wasimame karibu nawe.
17Nitashuka kule na kuzungumuza nawe; nitatwaa sehemu ya roho niliyokupa, niwape watu hao. Nao watabeba muzigo wa kuwatunza watu hawa pamoja nawe, kusudi usibebe muzigo huo peke yako.
18Sasa uwaambie watu hivi: Mujitakase kwa ajili ya kesho; mutakula nyama. Yawe amesikia mukilia na kusema kwamba hakuna wa kuwapa nyama, na kwamba hali yenu ilikuwa nzuri zaidi mulipokuwa Misri. Sasa Yawe atawapa nyama, nanyi sherti mutaikula.
19Mutakula nyama si kwa muda wa siku moja tu, au mbili, au tano, au kumi au makumi mbili,
20lakini kwa muda wa mwezi muzima! Mutaikula mpaka iwatoke ndani ya pua, mpaka muichukie. Yote hayo ni kwa sababu mumemukataa Yawe anayekuwa hapahapa kati yenu, na kulia mbele yake mukisema: Kwa nini tulitoka Misri?
21Lakini Musa akamwambia Yawe: Hesabu ya watu ninaowaongoza hapa ni elfu mia sita wanaoenda kwa miguu, nawe unasema: Nitawapa nyama ya kuwatosha mwezi muzima!
22Kunaweza kuchinjwa kondoo na ngombe wa kuwatosheleza? Samaki wote bahari wavuliwe kwa ajili yao?
23Yawe akamujibu Musa: Uwezo wangu umepunguka? Utaona basi kama neno langu litakuwa la kweli kwako au hapana.
24Basi, Musa akaenda na kuwajulisha watu yale Yawe aliyosema. Kisha, akakusanya wazee makumi saba kutoka kati ya wazee viongozi nao akawaweka kandokando kuzunguka hema.
25Hapo, Yawe akashuka katika wingu na kuzungumuza naye. Halafu akatwaa sehemu ya roho aliyokuwa amemupa Musa, akawapa kila mumoja wa wale wazee makumi saba. Walipoingiwa na roho huyo, wazee hao wakaanza kutoa unabii, lakini hawakurudia kufanya hivyo.
26Wazee wawili kati ya wale makumi saba waliochaguliwa, Eldadi na Medadi, walikuwa wamebaki katika kambi wenzao walipokwenda kwenye hema. Roho iliwafikia humohumo ndani ya kambi, wakaanza kutoa unabii pahali walipokuwa.
27Kijana mumoja akatoka mbio na kumwambia Musa: Eldadi na Medadi wanatoa unabii ndani ya kambi.
28Hapo, Yoshua mwana wa Nuni, ambaye alikuwa musaidizi wa Musa tangu ujana wake, akamwambia Musa: Bwana wangu, uwakataze!
29Lakini Musa akamujibu: Unaona wivu kwa ajili yangu? Heri Yawe angewapa watu wake wote roho yake nao wapate kuwa manabii!
30Kisha Musa akarudi katika kambi pamoja na wale wazee makumi saba wa Israeli.
Yawe anatuma kwale31Nyuma ya pale, Yawe akavumisha upepo kwa rafla, ukaleta kwale kutoka katika bahari na kuwafanya watue kando ya kambi, mwendo wa siku moja hivi kila upande kuzunguka kambi, wakalundikana chini karibu metre moja hivi kwenda juu.
32Basi, siku hiyo yote, usiku kucha, na siku iliyofuata watu walikusanya kwale; hakuna mutu aliyekusanya chini ya kilo elfu moja. Wakawaanika kila pahali kandokando ya kambi kwa kuwakausha.
33Kulikuwa kungali nyama kwa wingi na mbele watu hawajawamaliza kula, Yawe akawakasirikia watu, akawapiga watu kwa pigo kubwa sana.
34Kwa hiyo pahali pale pakapewa jina Kibroti-Hatawa, ni kusema “Makaburi ya Hamu”, kwa sababu huko ndiko walikozika watu waliokuwa na hamu ya kula nyama.
35Kutoka hapo Kibroti-Hatawa watu wakasafiri mpaka Haseroti, wakapiga kambi yao na kukaa kule.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.