1Mufalme Solomono alipomaliza kujenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme na majengo mengine yote aliyokusudia kujenga,
2Yawe alimutokea tena kama alivyomutokea kule Gibeoni.
3Yawe alimwambia: “Nimesikiliza wakati uliponiomba na kunisihi. Nimeitakasa nyumba hii ambayo umenijengea kusudi watu waabudu jina langu hapa milele. Nitaichunga na kuipenda wakati wote.
4Nawe kama ukinitumikia kwa ukamilifu wa moyo na usawa kama baba yako Daudi alivyofanya, ukitii amri zangu na kutimiza yale yote niliyokuamuru, ukifuata masharti yangu na maagizo yangu,
5basi, mimi nitakiimarisha kiti chako cha kifalme juu ya Israeli milele, kama nilivyomwahidi baba yako Daudi, nikisema: Hautakosa mutu wa kuikaa juu ya kiti cha kifalme cha Israeli.
6Lakini wewe au watoto wako mukigeuka na kuacha kunifuata, musiposhika amri zangu na masharti niliyowapa, mukienda kutumikia miungu mingine na kuiabudu,
7basi, nitawahamisha watu wangu, Waisraeli, kutoka inchi hii ambayo nimewapa; vilevile na nyumba hii ambayo niliyoitakasa kwa ajili ya jina langu, nitaitupilia mbali nami, na kuifanya kitu cha kuchekelewa na kuzarauliwa kati ya watu wa mataifa yote.
8Na nyumba hii itaharibiwa na kuwa mabomoko. Kila mutu atakayepita karibu atashituka na kutikisa kichwa, na kuuliza: ‘Kwa nini Yawe amefanya hivyo kwa inchi hii na kwa nyumba hii?’
9Watu wengine watajibu: ‘Ni kwa sababu walimwacha Yawe, Mungu wao, aliyewatoa babu zao katika inchi ya Misri, wakashikamana na miungu mingine, wakaiabudu na kuitumikia; kwa hiyo, Yawe amewaletea hasara hizi zote.’ ”
Solomono anamupa Hiramu miji makumi mbili(2 Sik 8.1-2)10Kisha miaka makumi mbili ambayo Solomono alipitisha kwa kuzijenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme,
11mufalme Solomono alimupa Hiramu mufalme wa Tiro miji makumi mbili katika jimbo la Galilaya kwa sababu yule Hiramu alikuwa amemupelekea Solomono mbao za mierezi na miberoshi, na zahabu vilevile, kadiri alivyohitaji kwa majengo.
12Lakini Hiramu alipofika kutoka Tiro na kuiona miji hiyo aliyokuwa amepewa na Solomono hakupendezwa nayo.
13Basi, akamwuliza Solomono: “Ndugu yangu, ni miji gani hii ambayo umenipa?” Ndiyo sababu miji hiyo inaitwa “Inchi ya Kabure” hata leo.
14Hiramu alikuwa amemupelekea mufalme Solomono zahabu kilo elfu tatu na mia sita.
Shuguli zingine za Solomono(2 Sik 8.3-18)15Haya ni maelezo juu ya mufalme Solomono, jinsi alivyowatumikisha watu kazi za kulazimishwa katika kujenga nyumba ya Yawe, nyumba yake ya kifalme, uwanja wa Milo, na ukuta wa Yerusalema, na vilevile katika kujenga upya miji ya Hazori, Megido na Gezeri.
16Gezeri ndio muji ambao mufalme wa Misri alikuwa ameuteka, akauchoma kwa moto na kuwaua Wakanana, wakaaji wake. Nyuma, binti wa mufalme wa Misri alipoolewa na Solomono, mufalme wa Misri alimupa binti yake muji ule wa Gezeri ukuwe zawadi ya arusi.
17Basi, Solomono aliujenga upya muji wa Gezeri. Vilevile alijenga Beti-Horoni wa chini;
18tena miji hii: Balati, na Tamari, muji unaokuwa katika mbuga katika inchi ya Yuda,
19na miji yake yote ya kuwekea akiba, magari yake ya vita, na waaskari wapanda-farasi wake; vilevile na chochote alichotaka kujenga katika Yerusalema, Lebanoni au nafasi ingine katika ufalme wake.
20Watu wengine wote waliobaki kati ya Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, maana yake wote hao ambao hawakukuwa wa taifa la Israeli,
21pamoja na wazao wao ambao Waisraeli hawakuweza kuwaangamiza kabisa, Solomono aliwatumikisha kazi za kulazimishwa hata leo.
22Lakini kati ya Waisraeli, Solomono hakumufanya mutu hata mumoja kuwa mutumwa. Waisraeli walimutumikia kwa kuwa waaskari, waongozi, majemadari, wakubwa, wasimamizi wa magari yake ya vita, na waaskari wapanda-farasi.
23Hii ndiyo jumla ya wakubwa waliohusika na uangalizi wa kazi ya Solomono: watu mia tano na makumi tano, hao ndio waliosimamia watu waliofanya kazi.
24Kisha binti ya mufalme wa Misri alihama katika muji wa Daudi, akaenda kukaa katika nyumba yake mwenyewe ambayo Solomono alimujengea. Kisha Solomono akajenga uwanja wa Milo.
25Mara tatu kila mwaka, Solomono alitoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani juu ya mazabahu aliyokuwa amemujengea Yawe, akamufukizia Yawe ubani. Akafanya vile ilivyofaa kwa nyumba ya Yawe.
26Mufalme Solomono alitengeneza mashua nyingi kule Ezioni-Geberi, karibu na Eloti kwa kivuko cha bahari Nyekundu, katika inchi ya Edomu.
27Naye mufalme Hiramu akawatuma wafundi wake wenye kujua bahari pamoja na watumishi wa Solomono.
28Walisafiri kwenda katika inchi ya Ofiri, na kuleta toka kule zahabu, wakamuletea mufalme Solomono yapata kilo elfu kumi na ine.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.