Waamuzi 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Gideoni anawashinda Wamidiani

1Yerubali, ni kusema Gideoni na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaamuka mapema, wakapiga kambi yao katika bonde karibu na chemichemi ya Harodi. Kambi ya Wamidiani ilikuwa upande wao wa kaskazini katika bonde karibu na mulima More.

2Yawe akamwambia Gideoni: “Watu unaokuwa nao ni wengi sana kwangu mimi kwa kuwatia Wamidiani katika mikono yao. Waisraeli wasipate kujisifu mbele yangu na kusema kwamba wamejiokoa kwa nguvu zao wenyewe.

3Sasa uwatangazie watu wote kwamba mutu yeyote anayekuwa mwoga au anayetetemeka arudi kwake.” Basi, Gideoni akawajaribu, na watu elfu makumi mbili na mbili wakarudi kwao, akabaki na watu elfu kumi.

4Yawe akamwambia Gideoni: “Watu hao wangali wengi sana. Sasa uwapeleke kwenye muto, nami nitawajaribu kule. Mutu yeyote nitakayekuambia: ‘Huyu atakwenda nawe, huyo aende nawe. Lakini mutu yeyote nitakayekuambia hatakwenda nawe, huyo asiende nawe.’ ”

5Basi, Gideoni akawapeleka watu kwenye muto na Yawe akamwambia: “Watu watakaolamba maji kwa ulimi kama imbwa, utawatenganisha na wale watakaopiga magoti kwa kunywa maji.”

6Jumla ya waliokunywa maji kwa kuchota kwa mikono yao na kulamba kama imbwa ilikuwa mia tatu. Lakini wengine wote waliobaki walipiga magoti kwa kunywa maji.

7Yawe akamwambia Gideoni: “Kwa hao watu mia tatu waliokunywa kwa kulamba kama imbwa, nitawaokoa Waisraeli na kuwatia Wamidiani katika mikono yao. Lakini wale wengine wote warudie kwao.”

8Basi, Gideoni akatwaa vyakula vya wale waliokuwa wanaondoka na baragumu, akawaaga waende kwao. Yeye akabaki na wale watu mia tatu. Kambi ya Wamidiani ilikuwa katika bonde upande wao wa chini.

9Usiku ule, Yawe akamwambia Gideoni: “Kwenda uwashambulie katika kambi yao, maana nimewatia katika mikono yako.

10Lakini kama unaogopa, kwenda pamoja na mutumishi wako Pura.

11Kule utasikia wanayosema, nawe utapata nguvu za kuweza kwenda kuwashambulia.” Basi, Gideoni akaenda pamoja na mutumishi wake Pura mpaka kwenye vituo vya walinda zamu wa kambi ya Wamidiani.

12Wamidiani, Waamaleki na watu wote wa mashariki walilala katika bonde, wengi kama nzige, na ngamia wao wasiohesabika, wengi kama muchanga wa bahari.

13Gideoni alipofika, akamusikia mutu mumoja akisimulia na mwenzake juu ya ndoto yake hivi: “Niliota ndoto. Nikaona mukate wa shayiri ukiviringikaviringika mpaka katika kambi ya Wamidiani, ukalipiga hema na kulipindua machali juu. Hema likalala chini.”

14Mwenzake akamujibu; “Hiyo inamaanisha tu upanga wa yule Mwisraeli Gideoni mwana wa Yoasi ambaye Mungu amewatia Wamidiani pamoja na waaskari wote katika mikono yake.”

15Gideoni aliposikia masimulizi hayo ya ndoto na mafasirio yake, akamwabudu Mungu. Kisha akarudi kwenye kambi ya Waisraeli, akasema: “Musimame tuende, maana Yawe amelitia jeshi la Wamidiani katika mikono yenu.”

16Basi akawagawanya wale watu mia tatu katika makundi matatu, akawapa baragumu na mitungi yenye mienge.

17Akawaambia: “Muniangalie na kufanya sawa vile nitakavyofanya wakati nitakapofika katika kambi.

18Nitakapopiga baragumu, mimi pamoja na kundi langu, ninyi wote mupige baragumu kutoka kila upande na kusema kwa sauti kubwa: ‘Kwa ajili ya Yawe na kwa ajili ya Gideoni!’ ”

19Ilipokaribia saa sita za usiku, Gideoni na kundi lake la watu mia moja wakafika kwa mwisho wa kambi, kwa mwanzo wa zamu ya kati. Wakati walipokuwa wamebadilisha wenye zamu, wakakaribia kambi ya waadui. Wakapiga baragumu na kuvunja mitungi waliyokuwa nayo.

20Makundi yote matatu kwa pamoja yakapiga baragumu na kuvunja mitungi yao. Katika mikono yao ya kushoto walishika mienge na kwa mikono yao ya kuume baragumu na kuzipiga, na walikuwa wanasema kwa sauti kubwa: “Upanga kwa ajili ya Yawe na kwa ajili ya Gideoni!”

21Wakasimama kila mumoja kwa nafasi yake kuizunguka kambi. Jeshi lote la waadui likatawanyika nalo likilalamika.

22Watu wa Gideoni walipopiga baragumu zao mia tatu, Yawe akawafanya Wamidiani waanze kuuana wao kwa wao katika kambi. Waliobaki wakatoroka mpaka Zerera, wakafika Beti-Sita, hata kwenye mupaka wa Abeli-Mehola karibu na Tabati.

23Waisraeli wa kabila la Nafutali, Aseri, na Manase, wote waliitwa, wakawafuatilia Wamidiani.

24Gideoni akatuma wajumbe katika inchi yote ya milima ya Efuraimu watangaze: “Muteremuke kwa kuwafuata Wamidiani na kuwazuia kwa kuteka vijito na muto Yordani mpaka Beti-Bara.” Basi, wanaume wote wa Efuraimu wakakuja na kuuteka muto Yordani mpaka Beti-Bara.

25Wakatwaa mateka viongozi wawili wa Midiani, majina yao ni Kibombobombo na Imbwa-wa-Pori. Wakamwua Kibombobombo juu ya jiwe la Kibombobombo, naye Imbwa-wa-Pori wakamwua katika kikamulio cha Imbwa-wa-Pori wakiwa wanawafuatilia Wamidiani. Wakamuletea Gideoni vichwa vya Kibombobombo na Imbwa-wa-Pori, ngambo ya muto Yordani.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help