Isaya 63 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Ni nani huyu anayekuja kutoka Edomu,

anayefika kutoka Bosira na nguo ya madoa mekundu?

Ni nani huyo aliyevaa nguo ya utukufu,

anatembea kwa nguvu zake kubwa?

Ni mimi Yawe

ninayetangaza ushindi wangu;

nami ni mwenye nguvu ya kuokoa.

2Lakini mbona nguo yako ni nyekundu,

nyekundu kama ya mutu anayekamua mizabibu?

3Kweli, nimekamua mizabibu peke yangu,

wala hakuna mutu aliyekuja kunisaidia.

Nimeyakanyaga mataifa kwa hasira yangu,

niliyapondaponda kwa kasirani yangu.

Nguo zangu zimejaa madoa ya damu yao,

imechafua kabisa nguo yangu.

4Niliamua kwamba siku ya kulipiza kisasi imefika;

wakati wa kuwakomboa watu wangu umefika.

5Niliangalia, hapakukuwa wa kunisaidia;

nilishangaa, hapakukuwa wa kuniunga mukono.

Lakini nilijipatia ushindi kwa mukono wangu,

kasirani yangu ilinisaidia.

6Kwa hasira yangu niliwaponda watu,

niliwalewesha kwa kasirani yangu;

damu yao niliimwanga chini.

Wema wa Mungu kwa Waisraeli

7Nitakumbusha

mema ya Yawe,

sifa za Yawe,

matendo yake yote kwetu,

mambo mazuri aliyowatendea Waisraeli,

rehema yake,

na wingi wa wema wake.

8Maana alisema juu yao:

Hakika, hawa ni watu wangu;

watoto wangu ambao hawatanidanganya.

Basi yeye akakuwa Mwokozi wao.

9Katika taabu zao zote,

hakumutuma mujumbe mwingine kwa kuwasaidia,

lakini yeye mwenyewe alikuja kuwaokoa;

kwa upendo na huruma yake aliwakomboa.

Aliwabeba na kuwakamata tangu zamani.

10Lakini wao waliasi,

wakaihuzunisha roho yake takatifu.

Basi, Mungu akageuka, akakuwa adui yao;

yeye mwenyewe akapigana nao.

11Halafu walikumbuka siku za zamani,

wakati wa Musa, mutumishi wa Yawe.

Wakauliza: Yuko wapi sasa Yawe,

aliyewaokoa wachungaji wa kundi lake katika bahari?

Yuko wapi yule aliyeweka Roho wake Mutakatifu kati yao,

12ambaye kwa mukono wake wenye nguvu

alifanya maajabu kwa njia ya Musa,

akapasua bahari na kuwaongoza watu wake,

na kujipatia jina la milele?

13Aliwaongoza katikati ya vilindi vya bahari,

wakapita humo kama farasi bila kujikwaa.

14Kama vile ngombe wanavyopelekwa kwa kulishwa katika bonde,

ndivyo Roho wa Mungu alivyowapumzisha watu wake.

Ndivyo, ee Mungu ulivyowaongoza watu wako,

nawe ukajipatia jina tukufu.

Maombi ya kuomba musaada

15Utuchungulie kutoka mbinguni, ee Mungu, uone,

utuangalie kutoka makao yako matakatifu na matukufu.

Iko wapi bidii yako kwa ajili yetu na nguvu yako?

Hatuoni tena upendo na huruma yako.

16Maana wewe ndiwe Baba yetu;

Abrahamu, babu yetu, hatujali,

naye Israeli hatutambui;

lakini wewe, ee Yawe, ni Baba yetu.

Wewe umeitwa tangu zamani: Mukombozi wetu.

17Ee Yawe, mbona unatukosesha njia zako?

Mbona unaifanya mioyo yetu kuwa migumu hata tusikuogope?

Urudie, ee Mungu, kwa ajili ya watumishi wako,

makabila ambayo yalikuwa mali yako siku zote.

18Sisi watakatifu wako tulirizi inchi kwa muda kidogo tu,

lakini waadui zetu wakakuja wakaharibu hekalu lako.

19Tumekuwa kama watu ambao haujawatawala hata kidogo,

kama watu ambao hawakujulikana kwa jina lako.

Heri ungepasua mbingu ushuke chini,

milima ingetetemeka mbele yako!

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help