1Kisha Elihu akaendelea kusema:
2Univumilie kidogo, nami nitakuonyesha kitu;
maana ningali bado na cha kusema kwa ajili ya Mungu.
3Nitaleta hekima yangu kutoka mbali sana,
na kuonyesha kwamba Muumba wangu ni wa haki.
4Kweli maneno yangu si ya uongo;
mwenye elimu kamili yuko hapa nawe.
5Sikia! Mungu ni mwenye nguvu
wala hamuzarau mutu yeyote;
uwezo wa akili yake ni mukubwa sana!
6Hawaachilii waovu waendelee kuishi;
lakini anawapatia wanaoteswa haki zao.
7Haachi kuwalinda watu wa haki;
nao anawaweka kuwa wafalme watawale na kutukuzwa.
8Lakini kama watu wakifungwa minyororo,
wakinaswa katika kamba za mateso,
9Mungu anawaonyesha matendo yao maovu,
na kwamba wao ni watu wenye kiburi.
10Anafungua masikio wasikie mafundisho,
na kuwaamuru warudi na kuacha uovu.
11Wakimutii Mungu na kumutumikia,
wanafanikiwa katika siku zao zote;
miaka yao yote inakuwa ya furaha.
12Lakini wasipomutii, wanaangamia kwa upanga,
na kufa kwa kukosa akili.
13Waovu wanapenda kukasirika;
hawamwombi musaada anapowafunga.
14Wanakufa wangali bado vijana,
maisha yao yanaisha kama ya washerati.
15Lakini Mungu anawaokoa wenye kuteswa kwa mateso yao,
anatumia shida zao kwa kuwafumbua macho.
16Mungu alikutoa katika taabu,
akakuweka pahali pakubwa pasipo shida,
na juu ya meza yako amekutayarishia vyakula vizuri.
17Lakini sasa umehukumiwa kama mwovu,
hukumu ya haki imekupata.
18Angalia kasirani isikuvute kwa kuzarau,
au usiache ukubwa wa mali za kukukomboa ukupotoshe.
19Kilio chako kitafaa kukutoa katika taabu,
au nguvu zako zote zitakusaidia?
20Usitamani usiku ukuje,
ambapo watu wanapotoweka.
21Angalisho! Usielekee uovu
maana umepewa mateso kwa kukuepusha na uovu.
22Kumbuka ukubwa wa uwezo wa Mungu;
nani anayeweza kufundisha kama yeye?
23Nani basi aliyeweza kumupangia njia yake,
au anayeweza kumwambia: “Umekosa”?
24Usisahau kusifu matendo yake
ambayo watu wameyashangilia.
25Watu wote wameona mambo Mungu aliyofanya;
mwanadamu anayaona kutoka mbali.
26Mungu ni mukubwa sana hata hatuwezi kumujua;
muda wa maisha yake hauchunguziki.
27Yeye anayavuta kwake maji ya bahari,
na kutoka ukungu anafanya matone ya mvua.
28Anayafanya mawingu yanyeshe mvua,
na kuwatiririshia wanadamu kwa wingi.
29Nani anayejua jinsi mawingu yanavyotanda,
au jinsi radi inavyonguruma kwake katika anga?
30Yeye anatandaza umeme wake kumuzunguka,
na kuvifunika vilindi vya bahari.
31Kwa mvua anawakulisha watu
na kuwapatia chakula kwa wingi.
32Anaukamata umeme kwa mikono yake,
kisha anapiga nao shabaha.
33Radi inatangaza kuja kwa Mungu;
hata nyama wanajua kwamba anakuja.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.