2 Samweli 21 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Wazao wa Saulo wanauawa

1Wakati mumoja katika siku za utawala wa Daudi kukatokea njaa kali katika inchi. Njaa hiyo ilidumu miaka mitatu yenye kufuatana. Daudi alimwomba Yawe shauri. Yawe akamwambia: “Saulo na jamaa yake wana makosa ya kumwanga damu kwa sababu aliwaua Wagibeoni.”

2Kwa hiyo, mufalme Daudi akawaita Wagibeoni. Wagibeoni hawakukuwa Waisraeli lakini walikuwa mabaki ya Waamori. Watu wa Israeli walikuwa wameapa kuwaacha wazima, lakini Saulo alijaribu kuwaua wote maana alikuwa na bidii ya upendeleo kwa watu wa Israeli na wa Yuda.

3Daudi akawauliza Wagibeoni: “Niwatendee nini? Nitalipa namna gani maovu muliyotendewa kusudi mupate kuibariki inchi hii na watu wa Yawe?”

4Wagibeoni wakamwambia: “Maneno kati yetu na Saulo pamoja na jamaa yake si jambo la kulipwa feza au zahabu, wala si jambo la kuua mutu yeyote katika inchi ya Israeli.”

Mufalme akawauliza tena: “Sasa munasema niwatendee nini?”

5Wao wakamwambia mufalme: “Saulo alikusudia kutuua sisi na kutuangamiza kusipate kubakia mutu yeyote wetu popote katika eneo lolote la Israeli.

6Basi, utupatie watu saba kati ya wazao wake, nasi tuwatundike mbele ya Yawe juu ya mulima Gibea, kwa Saulo aliyechaguliwa na Yawe.”

Mufalme akasema: “Nitawapatia nao.”

7Mufalme alimwacha Mefiboseti mwana wa Yonatani kwa sababu ya kiapo ambacho Daudi na Yonatani mwana wa Saulo walikuwa wamefanya kati yao kwa jina la Yawe.

8Lakini mufalme aliwatwaa wana wawili ambao Risipa binti ya Ahiya alimuzalia Saulo, nao ni: Armoni na Mefiboseti. Aliwatwaa vilevile watoto wote watano wanaume wa Mikali binti ya Saulo ambao alimuzalia Adrieli mwana wa Barzilayi wa muji Mehola.

9Daudi aliwatoa watoto hao saba wanaume kwa Wagibeoni, nao wakawatundika kwenye mulima mbele ya Yawe, wote saba wakakufa pamoja. Watoto hao waliuawa kwa mwanzo wa mavuno ya Shayiri.

10Kisha, Risipa binti ya Aya alitwaa nguo ya gunia, akajitandikia juu ya jiwe kubwa. Alikaa pale tangu mwanzo wa mavuno mpaka wakati wa mvua ulipofika na kuinyeshea maiti. Wakati huo wote, aliwafukuza ndege na wanyama wa pori, usiku na muchana, kusudi wasifikie maiti hizo.

11Daudi alisikia yale Risipa binti ya Aya, habara ya Saulo aliyofanya.

12Alikwenda na kuitwaa mifupa ya Saulo na ya mwana wake Yonatani kutoka kwa wakaaji wa Yabeshi-Gileadi, waliokuwa wameiiba kutoka kule Beti-Sani, ambako Wafilistini walikuwa wamemutundika Saulo na Yonatani siku ile walipomwua Saulo kwenye mulima Gilboa.

13Daudi akairudisha mifupa ya Saulo na ya mwana wake Yonatani kutoka kule; na kisha wakakusanya mifupa ya vijana saba waliotundikwa.

14Basi, watu wa Daudi wakaizika mifupa ya Saulo na ya mwana wake Yonatani katika inchi ya Benjamina, kule Zela katika kaburi la Kisi baba ya Saulo. Walifanya kila kitu ambacho mufalme aliamuru. Nyuma ya hayo, Yawe akayakubali maombi kwa ajili ya inchi.

Vita kati ya majitu na Wafilistini(1 Sik 20.4-8)

15Kisha Wafilistini walifanya vita tena na Waisraeli. Daudi na watu wake wakaenda kupigana na Wafilistini. Daudi alichoka sana siku ile.

16Isibi-Benobi, mutu mumoja wa wazao wa majitu ambaye mukuki wake wa shaba ulikuwa na uzito wa karibu kilo tatu na nusu na aliyekuwa amejifungia upanga mupya, alisema atamwua Daudi.

17Lakini Abisayi mwana wa Zeruya alikwenda kumusaidia Daudi. Abisayi alimushambulia yule Mufilistini na kumwua. Kwa hiyo, watu wakamwapia Daudi wakisema: “Hautakwenda tena nasi katika vita, kusudi usiizime taa ya ufalme katika Israeli.”

18Nyuma ya hayo, kulitokea tena mapigano na Wafilistini kule Gobu. Kule, Sibekayi wa muji wa Husa alimwua Safu aliyekuwa mutu mumoja wa wazao wa Rafa.

19Kulitokea tena mapigano na Wafilistini kule Gobu. Elihanani mwana wa Yare-Oregimu, wa muji wa Betelehemu, alimwua Goliati wa muji wa Gati, ambaye mupini wa mukuki wake ulikuwa kama muti wa mufumaji wa nguo.

20Kisha kulitokea tena vita kule Gati ambako kulikuwa na mutu mumoja alikuwa murefu sana, na mwenye vidole sita katika kila mukono, na vidole sita katika kila muguu, jumla ya vidole vyake ilikuwa makumi mbili na ine. Yeye vilevile alikuwa wa uzao wa majitu.

21Alipowachekelea Waisraeli, Yonatani mwana wa Simei, ndugu ya Daudi, alimwua.

22Hao wane walikuwa wazao wa majitu kule Gati, nao waliuawa na Daudi pamoja na watumishi wake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help