1Utege sikio, ee mbingu.
Sikiliza, ee dunia, maneno ninayosema.
2Mafundisho yangu yatone kama mvua,
maneno yangu yadondoke kama umande,
kama manyunyu kwenye mimea michanga,
kama mvua nyepesi katika majani mabichi.
3Maana nitatangaza jina la Yawe,
nanyi museme: “Mungu wetu ni Mukubwa”.
4Yawe ni mulima wa usalama.
Kazi zake ni kamilifu,
njia zake zote ni za haki.
Yeye ni Mungu mwaminifu asiyekuwa na kosa,
yeye anafanya mambo ya usawa na ya haki.
5Lakini ninyi mumekosa uaminifu kwake,
ninyi sio watoto wake tena kwa sababu ya uovu,
ninyi ni kizazi kiovu na kipotovu.
6Munaweza namna gani kumulipa hivyo Yawe,
enyi watu wapumbafu na wasiokuwa na akili?
Yeye siye baba yenu aliyewaumba,
aliyewafanya na kuwaimarisha?
7Mukumbuke siku zilizopita,
mufikiri miaka ya vizazi vingi.
Muulize baba zenu nao watawajulisha,
muulize wakubwa wenu nao watawaelezea.
8Mungu Mukubwa alipogawanyia mataifa mali yao,
alipowagawanyia wanadamu,
kila taifa alilipatia mipaka yake,
kulingana na hesabu ya wamalaika,
9lakini alijiwekea watu wa Yakobo kuwa wake,
hao alijichagulia kuwa mali yake.
10Yawe alikuta Waisraeli
katika inchi ya jangwa,
jangwa tupu zenye upepo mukali.
Aliwalinda na kuwatunza.
Aliwakinga kama mboni ya jicho lake.
11Alikuwa kama tai anayelinda chicha yake,
anayeruka karibu ya vitoto vyake,
akitandaza mabawa yake kwa kuwashikilia,
na kuwabeba juu ya mabawa yake.
12Yeye Yawe mwenyewe aliwaongoza
na hakukuwa mungu mwingine wa kumusaidia.
13Aliwapitisha katika inchi za juu za vilima,
nao wakakula mazao ya mashamba.
Akawapa asali kutoka katika mawe waonje
na mafuta kutoka katika jiwe gumu.
14Aliwapa siagi na maziwa ya mifugo,
mafuta ya wana-kondoo na kondoo dume,
makundi ya mifugo ya Basani na mbuzi.
Aliwapa ngano nzuri kabisa
na divai mupya wakakunywa.
15Watu wa usawa walinona,
wakapiga mateke.
Walinenepa sana,
kisha wakamwacha Mungu aliyewaumba,
wakazarau Mulima wa wokovu wao.
16Wakamufanya aone wivu mukali kwa miungu yao,
wakamuchochea akasirike kwa matendo yao ya kuchukiza.
17Wakatambikia pepo ambazo hazikukuwa miungu,
wakaendea miungu ambayo hawakuijua hata kidogo,
miungu mipya iliyotokea kwa siku za karibu,
ambayo wazee wao hawakuiheshimu hata kidogo.
18Hamukumujali Mulima wenu,
yule aliyewapa uzima.
Mulimusahau Mungu aliyewazaa ninyi.
19Yawe aliona jambo hilo akawaacha;
aliwakataa watoto wake, wanaume na wanawake.
20Akasema hivi: Nitawaficha uso wangu
nione mwisho wao utakuwa namna gani.
Maana wao ni kizazi kipotovu,
watoto wasiokuwa na uaminifu wowote.
21Wamenichochea kuona wivu kwa kitu kisichokuwa mungu,
wamenikasirikisha kwa sanamu zao.
Hivyo nitawafanya waone wivu juu ya watu wa bure,
nitawakasirikisha kwa kutumia taifa la wapumbafu.
22Hasira yangu imewaka moto,
inachoma mpaka chini kuzimu,
itateketeza dunia na vinavyokuwa ndani yake,
itaunguza misingi ya milima.
23Nitalundika hasara nyingi juu yao,
nitawamalizia mishale yangu.
24Watakonda kwa njaa,
wataangamizwa kwa homa kali.
Nitaleta nyama wenye meno makali kuwashambulia,
na nyoka wenye sumu wanaotambaa juu ya mavumbi.
25Vita itasababisha vifo vingi inje,
na ndani ya nyumba hofu itawatawala.
Vijana wanaume na wanawake watauawa,
hata wenye kunyonya na wazee wenye imvi.
26Ningaliwaangamiza kabisa
na kuwafanya wasikumbukwe tena na mutu yeyote,
27isipokuwa tu kwa sababu ya majivuno ya waadui zao,
kusudi waadui zao wasifikiri kwamba
wamepata kuwaangamiza,
nami Yawe sikufanya kitu katika mambo haya!
28Israeli ni taifa lisilokuwa na akili,
watu wake hawana ufahamu ndani yao.
29Wangekuwa na hekima wangejua kwa nini walishindwa,
wangeweza kuelewa mwisho wao utakuwa namna gani.
30Mutu mumoja anaweza namna gani kuwashinda watu elfu moja,
au watu wawili wanaweza namna gani kuwashinda watu elfu kumi,
isipokuwa kama mulinzi wao amewatupa,
Yawe amewaacha?
31Hata waadui zetu wenyewe wanajua wazi,
mulinzi wao hana nguvu kama mulinzi wetu.
32Maana mizabibu yao ni mizabibu ya Sodoma,
zimetoka katika mashamba ya Gomora.
Zabibu zake ni zabibu zenye sumu,
vishada vyake ni vichungu.
33Divai yao ni kama sumu ya nyoka,
ina sumu kali ya nyoka kubwa.
34Sina njia ya kuwaazibu?
Silaha zangu ziko katika mukono wangu.
35Ni kazi yangu kulipiza kisasi,
mimi nitalipiza,
wakati miguu yao itakapoteleza;
maana siku yao ya hasara imefika
mwisho wao uko karibu sana.
36Yawe atawatetea watu wake,
na kuwahurumia watumishi wake,
wakati atakapoona nguvu zao zimeisha
wala hakuna aliyebaki, mufungwa au mutu huru.
37Ndipo Yawe atakapouliza watu wake:
Iko wapi ile miungu yenu,
mulinzi muliyekimbilia usalama?
38Iko wapi hiyo miungu iliyokula matoleo yenu
na kunywa divai na sadaka zenu za kinywaji?
Basi isimame, iwasaidie;
muache hiyo ikuwe ulinzi wenu sasa!
39Muone kwamba mimi ni Mungu
na wala hakuna mwingine isipokuwa mimi.
Mimi ninaua na kuweka uzima,
ninaumiza na kuponya,
na hakuna anayeweza kumwokoa yeyote toka katika mikono yangu.
40Ninanyoosha mukono wangu mbinguni
na kuapa: Kama vile ninavyoishi milele,
41nitanoa upanga wangu unaometemeta,
nitanyoosha mukono kutoa hukumu,
nitawalipiza kisasi waadui zangu,
nitawaazibu wale wanaonichukia.
42Mishale yangu nitailewesha kwa damu,
upanga wangu utashiba nyama,
utalowana na damu ya vidonda na wafungwa
na waadui wenye nywele ndefu.
43Enyi mataifa, mushangilie watu wake,
maana yeye analipiza kisasi damu ya watumishi wake,
anawalipiza kisasi wapinzani wake,
na kuitakasa inchi ya watu wake.
44Musa alikuja mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, wakarudilia maneno ya wimbo huu, kusudi Waisraeli wote wausikie.
Maagizo ya mwisho ya Musa45Musa alipomaliza kuwaambia watu wa Israeli maneno haya yote,
46akawaambia: “Muweke ndani ya mioyo yenu maneno yote ambayo ninawapa leo. Muwaamuru watoto wenu kusudi wafuate kwa uaminifu maneno yote ya sheria hii.
47Maana sheria hii si maneno matupu lakini ni uzima wenu; kwa njia ya sheria hii, mutaishi maisha marefu katika inchi munayokwenda kurizi, ngambo ya muto Yordani.”
48Siku hiyohiyo, Yawe akamwambia Musa:
49“Panda juu ya mulima huu wa Abarimu, mulima Nebo katika inchi ya Moabu, kuelekea muji wa Yeriko, uiangalie inchi ya Kanana ninayowapa Waisraeli wairizi.
50Kulekule juu ya mulima utakufa na kukutana na wazee wako kama vile kaka yako Haruni alivyokufa katika mulima Hori na kukutana nao,
51kwa sababu ninyi wote wawili mulivunja uaminifu wenu kwangu mbele ya Waisraeli mulipokuwa kwenye maji ya Meriba, karibu na muji wa Kadesi, katika jangwa la Sini. Mukakosa kuhakikisha utakatifu wangu kati ya Waisraeli.
52Utaona inchi inayokuwa mbele yako, lakini hautaingia katika inchi hiyo ninayowapa Waisraeli.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.