Kutoka 36 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Bezaleli na Oholiabu, pamoja na kila mwanaume ambaye Yawe amemujalia uwezo na akili ya kujua namna ya kufanya kazi zote katika majengo ya hema takatifu, atafanya kazi kulingana na yote ambayo Yawe aliamuru.

Matoleo kwa wingi

2Musa akamwita Bezaleli na Oholiabu na kila mutu ambaye alikuwa amejaliwa ujuzi na Yawe na kila mutu ambaye moyo wake ulimusukuma kufanya kazi kwa nia nzuri.

3Hao wakapokea kutoka kwa Musa vitu vyote vilivyotolewa na Waisraeli kwa mapenzi yao kwa ajili ya kazi ya hema takatifu. Watu waliendelea kumuletea michango yao kufuatana na mapenzi yao kila asubui.

4Watu wote wenye ujuzi waliokuwa wanafanya kazi za kila namna za kujenga hema la mukutano walitoka, kila mumoja katika kazi yake, wakamwendea

5Musa na kumwambia: Watu wameleta vitu vingi zaidi ya vile vinavyohitajiwa kwa kazi Yawe aliyotuagiza tufanye.

6Basi, Musa akaagiza: Mutu yeyote, akuwe mwanaume au mwanamuke, asilete muchango zaidi kwa ajili ya hema takatifu. Watu wakazuiwa kuleta vitu,

7maana vile walivyokuwa wameleta vilitosha kwa kazi hiyo na kubaki.

Kutengeneza hema takatifu(Kut 26.1-37)

8Wanaume wote wenye ujuzi wakatengeneza hema takatifu kwa mapazia kumi ya kitani safi iliyosokotwa, na kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kuchora makerubi.

9Urefu wa kila pazia ulikuwa metre kumi na mbili na upana metre mbili. Mapazia yote yalikuwa ya kipimo kimoja.

10Aliyaunga mapazia matano kufanya kipande kimoja na kufanya vile vile na yale mengine matano.

11Alitengeneza kamba za rangi ya samawi kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha kwanza na kamba zingine katika pazia la mwisho la kipande cha pili.

12Alitia kamba makuni tano katika pazia la kwanza la kipande cha kwanza na kamba makuni tano kwenye utepe wa pazia la pili. Kamba zote zilielekeana.

13Kisha akatengeneza vifungio makuni tano vya zahabu kwa kuunganishia vile vipande viwili vya mapazia, hivyo hema likakuwa kitu kimoja.

14Kisha alitengeneza vilevile kifuniko cha hema kwa mapazia kumi na moja ya manyoya ya mbuzi.

15Kila pazia lilikuwa na urefu wa metre kumi na tatu na upana wa metre mbili. Mapazia yote kumi na moja yalikuwa ya kipimo kilekile.

16Basi, akaunganisha mapazia matano pamoja na mapazia sita pamoja.

17Kisha akafanya kamba makuni tano kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha kwanza na kamba makuni tano kwenye upindo wa kipande cha pili.

18Halafu akatengeneza vifungio makuni tano vya shaba kwa kuunganishia vile vipande viwili vya mapazia na hivyo kufanya pazia moja la hema.

19Kisha akatengeneza kifuniko cha ngozi laini ya kondoo dume na juu yake kifuniko kingine cha ngozi laini ya mbuzi.

20Halafu akatengenezea hema mbao za mujohoro za kusimama wima.

21Kila ubao ulikuwa na urefu wa metre ine na upana wa sentimetre makumi sita na sita.

22Kila ubao ulikuwa na ndimi mbili za kuunganishia. Mbao zote za hema alizifanyia ndimi.

23Mbao hizo za hema zilitengenezwa hivi: mbao makumi mbili upande wa kusini,

24na vikalio makumi ine vya feza chini ya hizo mbao makumi mbili, vikalio viwili chini ya kila ubao kwa kushikilia zile ndimi zake mbili.

25Na upande wa pili, ni kusema upande wa kaskazini wa hema, alitengeneza vilevile mbao makumi mbili,

26na vikalio vyake makumi ine vya feza; vikalio viwili chini ya kila ubao.

27Upande wa nyuma, ni kusema upande wa magaribi wa hema, alitengeneza mbao sita.

28Alitengeneza vilevile mbao mbili kwa ajili ya pembe za hema upande wake wa nyuma.

29Mbao hizo mbili za pembeni ziliachana chini lakini zilishikamanishwa kwenye pete ya kwanza. Mbao mbili kwa ajili ya hizo pembe mbili zilitengenezwa namna hiyo.

30Hivyo kulikuwa mbao nane na vikalio vyake vya feza kumi na sita, vikalio viwili chini ya kila ubao.

31Alitengeneza vilevile miti ya mujohoro: miti tano kwa ajili ya mbao za upande mumoja wa hema,

32miti tano kwa ajili ya upande wa pili wa hema, na miti tano kwa ajili ya mbao za upande wa nyuma wa hema uliokuwa upande wa magaribi.

33Alitengeneza muti wa katikati uliofika nusu ya jengo la hema ambao ulipenya katikati kutoka mwisho mpaka mwisho.

34Mbao zote alizipakaa zahabu, akatengeneza na pete za zahabu za kushikilia miti ile ambayo vilevile aliipakaa zahabu.

35Alitengeneza pazia la nyuzi za rangi ya samawi, zambarau na nyekundu na kitani safi iliyosokotwa. Pazia hilo lilipambwa na makerubi kwa ufundi.

36Alitengeneza nguzo ine za mujohoro, akazipakaa zahabu na kuzitilia vifungio vya zahabu. Vilevile alizifanyia vikalio vine vya feza.

37Vilevile, kwa ajili ya mulango wa hema, alitengeneza pazia kwa nyuzi za rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, nalo pazia lilipambwa vizuri,

38na nguzo zake tano zikiwa na vifungio. Chongo zake na vyuma vyake alivipakaa zahabu, lakini vikalio vyake vitano vilikuwa vya shaba.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help