Yeremia 29 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Barua ya Yeremia kwa Wayuda kule Babeli

1Hii ni barua ambayo nabii Yeremia aliyotuma kutoka Yerusalema kwa wasimamizi wa watu waliopelekwa katika uhamisho Babeli pamoja na makuhani, manabii, na watu wote wengine ambao Nebukadneza alikuwa amewachukua kutoka Yerusalema na kuwapeleka kule.

2Wakati huu ulikuwa nyuma ya kuondoka Yerusalema kwa mufalme Yekonia na malkia mama wa mufalme, matowashi wa mufalme, wakubwa wa inchi ya Yuda na wa Yerusalema, wafundi na wafua vyuma.

3Barua hii ilitumwa kwa mukono wa Elasa mwana wa Safamu, na Gemaria mwana wa Hilkia, ambao Zedekia mufalme wa Yuda, aliowatuma kwa Nebukadneza mufalme wa Babeli. Nayo iliandikwa hivi:

4Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi juu ya watu wote aliowatoa wapelekwe katika uhamisho kutoka Yerusalema na kwenda Babeli:

5Mujijengee nyumba za kukaa. Mulime mashamba, mupande mbegu na kula mazao yake.

6Muoe, mupate watoto. Muwaoee wana wenu na kuowesha wabinti zenu, nao vilevile wapate watoto. Muongezeke kule wala musipunguke.

7Mushugulike na kuleta ustawi katika muji ule ambamo nimewahamishia. Muuombee muji huo kwa Yawe, maana ukistawi ninyi vilevile mutastawi.

8Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Musikubali kudanganywa na manabii wenu na waaguzi wanaokuwa katikati yenu, wala musisikilize ndoto wanazoota.

9Maana wanawatabiria uongo kwa kutumia jina langu. Mimi sikuwatuma.

–Ni ujumbe wa Yawe.

10Yawe anasema hivi: Mutakapopitisha miaka makumi saba huko Babeli, nitawashugulikia na kuitimiza ahadi yangu ya kuwarudisha kwa nafasi hii.

11Maana, mimi ninajua mupango ninaokuwa nao juu yenu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nayo mipango yangu ni ya kuwatendea mema wala si mabaya, kusudi mupate kuwa na tumaini katika siku zinazokuja.

12Kwa hiyo mutakapokuja kunililia na kuniomba, nitawasikiliza.

13Mutanitafuta mimi na kuniona. Mutakaponitafuta kwa moyo wote,

14mutaniona. Nitatengeneza upya maisha yenu na kuwakusanya kutoka mataifa yote na pahali pote nilipowasambaza. Nitawarudisha pahali nilipowaondoa wakati nilipowapeleka katika uhamisho.

–Ni ujumbe wa Yawe.

15Ninyi munasema: Yawe ametuinulia manabii huko Babeli.

16Yawe anasema hivi juu ya mufalme anayetawala katika kiti cha kifalme cha Daudi, na juu ya watu wote wanaokaa katika muji huu, ndio wandugu zenu ambao hawakuondoka kwenda pamoja nanyi katika uhamisho:

17Nitawatumia vita, njaa na magonjwa makali. Nitawafanya kuwa kama matunda mabaya sana ya tini zisizoweza hata kukuliwa.

18Nitawashambulia kwa vita, njaa na magonjwa makali. Nitawafanya kuwa kitu cha kuchukiza kwa falme zote za dunia; nitawafanya kuwa mufano wa kutumia kwa kutoa laana. Mutakuwa kitu cha kushangaza, cha kuzarauliwa na cha kuzomewa kati ya mataifa yote nitakapowasambaza.

19Nitafanya hivyo kwa sababu hamukusikiliza maneno yangu niliyowaambia kila mara kwa njia ya watumishi wangu, manabii, nanyi mukakataa kusikiliza.

–Ni ujumbe wa Yawe.

20Enyi wote niliowaondoa kutoka Yerusalema na kuwapeleka katika uhamisho kule Babeli, musikilize neno langu mimi Yawe.

21Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi juu ya Ahabu, mwana wa Kolaya na juu ya Zedekia mwana wa Masea, ambao wanawatabiria uongo kwa jina lake: Nitawatoa katika mikono ya Nebukadneza, mufalme wa Babeli, naye atawaua waziwazi mbele ya macho yenu.

22Kwa sababu jambo hilo litakalowapata, watu wote waliohamishiwa Babeli kutoka Yuda, watatumia mufano huu kwa kutoa laana: Yawe akufanye kama Zedekia na Ahabu, ambao mufalme wa Babeli aliwachoma katika moto.

23Jambo hili litawafikia kwa sababu wametenda katika Israeli mambo yasiyofanyika. Walizini na wake za jirani zao, na kusema maneno ya uongo kwa jina langu, jambo ambalo mimi sikuwaamuru wafanye. Mimi ninajua hayo. Nimeyashuhudia.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Barua ya Semaya

24Yawe akaniagiza kumwambia Semaya wa Nehelamu hivi:

25Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Umejiruhusu kutuma barua kwa wakaaji wote wa Yerusalema na kwa kuhani Zefania, mwana wa Masea na kwa makuhani wengine wote. Katika barua hiyo, ulimwambia Zefania hivi:

26Yawe amekufanya wewe Zefania kuwa kuhani kwa pahali pa kuhani Yehoyada, kusudi ukuwe mukubwa wa nyumba ya Yawe. Wewe utashugulika na kumutia katika kifungo na kumufunga kwa minyororo mwenda-wazimu yeyote anayetabiri.

27Kwa nini basi, haukukaripia Yeremia wa muji wa Anatoti ambaye anakutabiria?

28Maana yeye alituma habari huko Babeli, akisema: Mutabaki katika uhamisho kwa muda murefu, mujenge nyumba za kukalia, mulime mashamba, mupande mbegu na kula mazao yake!

29Kuhani Zefania akamusomea nabii Yeremia barua hiyo.

30Neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi:

31Utume ujumbe huu kwa watu wote wanaokuwa katika uhamisho:

Yawe anasema hivi juu ya Semaya wa Nehelamu: Semaya amewatabiria ninyi ingawa mimi sikumutuma na kuwasukuma musadikie uongo.

32Kwa hiyo nitamwazibu Semaya wa Nehelamu pamoja na wazao wake. Hakuna hata mumoja wa watu wake atakayebaki muzima na kupata kuona mema nitakayowafanyia watu wangu, kwa sababu amesema maneno ya uasi juu ya Yawe.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help