1Yawe akawaambia Musa na Haruni:
2Ikiwa mutu yeyote atakuwa na kivimba au upele au chunuku juu ya mwili wake, ikionekana kwamba ni ukoma, basi, ataletwa kwa kuhani Haruni au mumoja wa wana wake anayekuwa kuhani.
3Kuhani atachunguza pahali panapokuwa ugonjwa na ikiwa nywele za pahali pale zimebadilika kuwa nyeupe na ugonjwa wenyewe ukionekana kuwa uko ndani zaidi ya ngozi ya mwili wake, basi, huo ni ukoma. Kuhani akimaliza kumuchunguza, hivyo atatangaza kwamba mutu yule ni muchafu.
4Lakini ikiwa kipele hicho, ingawa ni cheupe hakikuingia ndani sana ya ngozi na wala nywele za pahali pale hazikubadilika kuwa nyeupe, basi, kuhani atamutenga mutu yule kwa muda wa siku saba.
5Siku ya saba, kuhani atamwangalia tena mutu yule, na ikiwa, kulingana na uchunguzi wa kuhani, ugonjwa huo haujaenea kwenye ngozi yake, basi, kuhani atamutenga mutu yule kwa siku zingine saba.
6Kuhani atamuchunguza tena mutu yule siku ya saba. Kama kulingana na uchunguzi wake, ile sehemu ya ugonjwa imefifia na ugonjwa haujaenea, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi, huo ni upele tu. Mutu huyo atafua nguo zake, naye atakuwa safi.
7Lakini taka lile likienea kwenye ngozi, nyuma ya mutu yule kujionyesha kwa kuhani kwa ajili ya kutakaswa kwake, basi, atakuja tena kwa kuhani.
8Kuhani atamwangalia tena, na kama ule upele umeenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, huo ni ukoma.
9Kama mutu ameshikwa na ukoma, ataletwa kwa kuhani.
10Kuhani atamwangalia na kama kivimba cheupe ambacho kimefanya nywele zake zikuwe nyeupe na kivimba kile kimegeuka kuwa kidonda kibichi,
11huo ni ukoma wa muda murefu. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu. Hatamutenga mutu yule kwa uchunguzi maana yeye ni muchafu.
12Kama ukoma umemushika na umeenea mwili muzima, toka kwenye kichwa mpaka kwenye miguu kama vile kuhani atakavyoona,
13pale kuhani atamwangalia. Kuhani akiona kwamba ukoma umemwenea mwili muzima, basi, atamutangaza mutu yule kuwa safi kwa sababu mwili umegeuka kuwa mweupe na hivyo mutu yule ni safi.
14Lakini kukionekana juu ya mwili wa mutu yule kidonda kibichi, basi, mutu yule atakuwa muchafu.
15Kuhani ataangalia hicho kidonda kibichi na kumutangaza kuwa ni muchafu kwa sababu huo ni ukoma.
16Lakini hicho kidonda kikigeuka tena kuwa cheupe, mutu yule atarudi kwa kuhani.
17Kuhani atamwangalia na akiona kwamba kimegeuka kuwa cheupe, basi, atamutangaza mutu yule kuwa safi.
18Kama mutu ameshikwa na jipu, nalo limepona,
19lakini pahali pale jipu lilipokuwa pamegeuka kuwa kivimba cheupe au kuwa pekundu lakini peupe, anapaswa kumwonyesha kuhani.
20Kuhani atamwangalia yule mutu. Kuhani akiona pamekuwa shimo na nywele za pahali pale zimegeuka kuwa nyeupe, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu. Huo ni ugonjwa wa ukoma ambao umetokana na jipu.
21Lakini kama kuhani akimwangalia yule mutu na kuona kwamba nywele za pahali pale si nyeupe na wala hakuna shimo, lakini pamefifia, basi, atamutenga huyu mutu kwa muda wa siku saba.
22Kama ugonjwa huo ukienea kwenye ngozi, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, sehemu hiyo ina ugonjwa.
23Lakini, kama ile sehemu haijaenea, basi, lile ni kovu la jipu tu. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi.
24Au, ikiwa kuna pahali palipoungua na ile nyama mbichi imegeuka kuwa nyekundu-nyeupe au ni nyeupe,
25kuhani atapaangalia. Kama akiona kwamba nywele zimegeuka kuwa nyeupe na pana shimo, basi, huo ni ukoma. Ukoma huo umejitokeza kwa njia ya pahali pale palipoungua. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, maana ana ugonjwa wa ukoma.
26Lakini kama kuhani akiona kwamba nywele za pahali pale si nyeupe na hakuna shimo lakini pamefifia, basi, kuhani atamutenga mutu yule kwa muda wa siku saba.
27Siku ya saba kuhani atamwangalia. Kama umeenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, maana ana ugonjwa wa ukoma.
28Lakini, kama ile alama haijaenea, lakini imefifia, hicho ni kivimba kilichotokana na kuungua. Basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi, maana hilo ni kovu la kuungua.
29Kama mutu yeyote mwanaume au mwanamuke, ana kidonda juu ya kichwa au kwenye kidevu,
30kuhani ataangalia ugonjwa huo. Ikiwa kuhani ataona kwamba kuna shimo na nywele ni manjano na nyembamba, basi, atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, maana huo ni upele na ni ukoma wa kichwa au wa kidevu.
31Kama kuhani ataona kwamba hakuna shimo na nywele si nyeusi, basi kuhani atamutenga mutu yule kwa muda wa siku saba.
32Siku ya saba kuhani ataangalia kile kidonda. Kama kidonda hicho hakijaenea na hakuna nywele zenye rangi ya manjano wala hakuna vipele vyovyote pahali pale, basi,
33mutu yule atanyoa nywele au ndevu zake. Lakini pahali pale penye vipele hatapanyoa. Kisha kuhani atamutenga mutu yule kwa muda mwingine wa siku saba.
34Siku ya saba, kuhani ataangalia vile vipele. Ikiwa kuhani ataona kwamba vipele hivyo havikuenea kwenye ngozi na wala havikuingia ndani ya ngozi, basi, atamutangaza mutu yule kuwa safi. Mutu huyo atafua nguo zake, naye atakuwa safi.
35Lakini ikiwa vipele hivyo vimeenea kisha kutakaswa,
36mutu yule ataangaliwa na kuhani na ikiwa vimeenea kwenye ngozi, kuhani hatahitaji kutafuta nywele zenye rangi manjano. Mutu yule atakuwa muchafu.
37Lakini ikiwa kuhani ataona kwamba vile vipele vimepona na nywele nyeusi zimeota pahali pale, basi, vidonda vimepona, basi, mutu yule ni safi. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi.
38Kama mutu yeyote, akuwe mwanaume au mwanamuke, ana alama nyeupe juu ya mwili wake,
39kuhani atamwangalia mutu yule. Ikiwa kuhani ataona kwamba alama hizo ni nyeupe kidogo, huo ni upele wa kawaida, mutu yule ni safi.
40Kama mwanaume amepata upaa, yeye ni safi maana ana upaa tu.
41Ikiwa upaa huo umetanda tangu nyuma mpaka mbele mutu yule ana upaa tu na yuko safi.
42Lakini kama kwenye kichwa penye upaa au kwenye paji la uso kwenye upaa kuna alama nyekundu-nyeupe, huo ni ukoma unaotokea kwenye upaa wake juu ya kichwa au kwenye paji lake.
43Kuhani atamwangalia. Ikiwa kuhani ataona kwamba hicho kivimba ni chekundu-cheupe kwenye upaa au kwenye paji lake na unaonekana kama ukoma kwenye ngozi yake,
44basi, mutu yule ana ukoma, yeye ni muchafu. Kuhani atamutangaza mutu huyo kuwa muchafu. Ugonjwa wake uko kwenye kichwa chake.
45Mwenye ukoma yeyote atavaa nguo zilizochanika, nywele zake hatazichanuliwa, na mudomo wake wa juu ataufunika na atalalamika akisema: Mimi ni muchafu, mimi ni muchafu.
46Ataendelea kuwa muchafu kwa muda wote anaokuwa na ugonjwa ule. Yeye ni muchafu, naye atakaa peke yake inje ya kambi.
47Kama kuna namna ya taka la ukoma kwenye nguo, ikuwe ya sufu au kitani,
48nguo ile ikuwe imefumwa au imesokotwa kwa kitani au sufu au ni nguo ya ngozi ya aina yoyote,
49ikiwa taka lile lina rangi ya kijani au nyekundu katika nguo ile, basi, nguo ile ina ukoma. Kwa hiyo ni lazima kumwonyesha kuhani.
50Kuhani ataangalia taka lile na kuweka nguo ile kando kwa muda wa siku saba.
51Siku ya saba ataangalia taka lile. Ikiwa taka lile limeenea katika nguo hiyo, ikuwe ni ya kufuma au kusokotwa au ya ngozi au ya ngozi ya aina yoyote, nguo ile ina ukoma. Hivyo nguo ile ni chafu.
52Kuhani atachoma kwa moto nguo ile maana ina namna ya ukoma wenye kuenea.
53Kama kuhani ataona kwamba taka halikuenea katika nguo, basi,
54ataamuru nguo ile ifuliwe na kuwekwa pembeni kwa muda mwingine wa siku saba.
55Kuhani ataangalia nguo ile kisha kufuliwa. Ikiwa ile alama haijabadilika rangi yake hata ingawa taka halikuenea, basi, nguo ile ni chafu. Nguo ile utaichoma kwa moto, ikuwe alama ile iko nyuma au mbele ya nguo ile.
56Kama kuhani ataona kwamba ile alama imefifia kisha kufuliwa, basi atakata ile sehemu inayokuwa na namna ya ukoma.
57Kisha, ikiwa hiyo alama inaonekana tena kisha katika nguo iliyofumwa au iliyosokotwa au katika kitu chochote cha ngozi, basi ukoma umeenea. Kwa hiyo nguo ile utaichoma kwa moto.
58Lakini nguo ambayo taka limetokea kisha kufuliwa, itafuliwa kwa mara ya pili na hivyo itapata kuwa safi.
59Hiyo ni sheria juu ya taka la ukoma linalotokea katika nguo ya sufu au kitani au iliyofumwa au iliyosokotwa au ya ngozi. Kwa njia hiyo mutaweza kutia tofauti kati ya nguo isiyokuwa chafu na ile inayokuwa chafu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.