Isaya UTANGULIZI - Swahili Congo Revised Bible 2002
UTANGULIZIIsaya alikuwa mumoja kati ya manabii wakubwa kabisa wa Waisraeli. Alifanya kazi yake ya kinabii kuanzia mwaka wa 750 mpaka 700 mbele ya Kristo. Kitabu chenyewe kinaweza kufikiriwa kuwa na mafungu matatu ya mahubiri.1. Sura 1-39. Sehemu hii kubwa ya kitabu cha Isaya inahusika na utawala wa kaskazini wa Israeli na ule wa kusini, ni kusema Yuda. Zilikuwa zimepatwa na musukosuko mukali wa serikali yenye nguvu, ni kusema Asuria. Isaya alionya, hata wakubwa, kwamba kutakuwa hatari kubwa zaidi. Watu walitegemea kujiunga na Misri pamoja na tawala nyingine juu ya Asuria. Hali hiyo ilimaanisha kwa Isaya kwamba watu walikuwa wamekosa kumutegemea Mungu. Aliwaonya Waisraeli kwamba kwa kufanya hivyo, walikuwa wanajitayarishia maangamizi yao wenyewe.2. Sura 40-55. Yanayozungumuziwa hapa yanaelekea nyakati ambazo watu wengi kutoka Yuda walipelekwa katika uhamisho katika karne ya sita mbele ya Kristo. Wakakuwa huko bila mutawala wala matumaini ya siku zenye kuja. Nabii anatangaza kwamba Mungu atawapa uhuru watu hao waliogandamizwa. Watarudishwa katika muji wao na inchi yao, ambamo watashiriki hali mupya inayokuja. Jambo kubwa katika mahubiri yale ni kwamba Mungu ambaye anaiongoza historia ya ulimwengu ni tofauti na miungu mingine. Yeye ni Muumba wa ulimwengu na mukubwa wa mambo yanayowapata wanadamu. Atatengeneza tena maisha ya Waisraeli kusudi watu wengine wapate fanaka. Hayo yatakamilika kwa kazi ya Mutumishi wa Bwana. Katika Agano Jipya jambo hilo la Mutumishi wa Bwana limekamilika katika nafsi ya Bwana wetu Yesu Kristo.3. Sura 56-66. Labda fungu hili linahusika na ujumbe mbalimbali wa nyakati za nyuma ya kurudi kutoka katika uhamisho. Watu wanaonywa kwamba inafaa kutimiza maagizo ya Mungu. Katika sehemu hii watu wanapewa matumaini ya hali njema zaidi siku zenye kuja. Wanahakikishiwa kwamba Mungu atatimiza yale aliyoahidi. Hiyo ndiyo Habari Njema kwao.