Ezekieli 39 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kushindwa kwa Gogi

1Bwana wetu Yawe akaniambia: Wewe mwanadamu! Toa unabii juu ya Gogi. Useme:

Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi nitapingana nawe Gogi mutawala mukubwa wa mataifa ya Meseki na Tubali.

2Nitakugeuza na kukuelekezea upande mwingine na kukuongoza kutoka mbali upande wa kaskazini uende kushambulia milima ya Israeli.

3Kisha nitauvunja upinde wako katika mukono wako wa kushoto, na mishale yako katika mukono wako wa kuume nitaiangusha chini.

4Utakufa juu ya milima ya Israeli, wewe pamoja na makundi yako yote ya waaskari na mataifa yanayokuwa pamoja nawe. Nami nitaitoa miili yao ikuliwe na ndege wa kila aina na nyama wakali.

5Utakufia katika pori.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

6Nitawasha moto juu ya inchi ya Magogi na juu ya wote wanaokaa salama katika inchi za kandokando ya bahari. Nao watatambua kwamba mimi ni Yawe.

7Nitajulisha jina langu takatifu kwa watu wangu Waisraeli, wala sitaruhusu tena watu walikufuru jina langu takatifu. Nayo mataifa yatatambua kwamba mimi ni Yawe, Mutakatifu wa Israeli.

8Siku ile ninayosema juu yake, kwa hakika inakuja. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

9Kwa hiyo, watu wanaoishi katika miji ya Israeli watatoka na kukusanya silaha zilizoachwa na kuzichoma kwa moto. Watatumia hizo ngao, pinde, mishale, mikuki na magongo, kama kuni za kuwasha moto kwa muda wa miaka saba.

10Hawatahitaji kuokota kuni katika mashamba, wala kukata miti katika pori, kwa sababu watazitumia hizo silaha kwa kuwasha nazo moto. Watabeba mali za wale walioteka mali zao na kuwanyanganya mali zao. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

11Katika siku ile, nitamupa Gogi pahali pa kufanyia maziko katika inchi ya Israeli, katika Bonde la Wasafiri, upande wa mashariki wa bahari ya Chumvi. Gogi atazikwa huko pamoja na kundi lake lote la waaskari, nao wasafiri watazuizwa kupita kule. Bonde hilo litaitwa, Bonde la Hamoni-Gogi.

12Kwa kuisafisha inchi, Waisraeli watatumia muda wa miezi saba kuzika maiti hizo.

13Watu wote katika inchi watashugulika na kuwazika. Na hilo litakuwa jambo la kuwapatia sifa, siku ile nitakapoonyesha utukufu wangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

14Kisha miezi hiyo saba, watatenga watu watakaopitapita katika inchi kwa kutafuta maiti ambazo zitakuwa bado hazijazikwa, wazizike kwa kuisafisha inchi.

15Wanapoona mufupa wa mutu wataweka kitambulisho juu yake kusudi wale wanaozika wakuje na kuuzika katika Bonde la Hamoni-Gogi.

16Huko kutakuwa vilevile muji utakaoitwa “Muji wa watu wengi”. Ndivyo watakavyoisafisha inchi.

17Sasa, ewe mwanadamu, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Uite ndege wote na nyama wote wa pori wakusanyike toka pande zote na kuja kukula karamu ya sadaka ya nyama ninayowatayarishia, ambayo itakuwa kubwa sana juu ya milima ya Israeli, ambako watakula nyama na kunywa damu. Ang. Ufu 19.17-18

18Watakula nyama ya mashujaa, watakunywa damu ya wakubwa wa dunia watakaochinjwa kama kondoo dume au wana-kondoo, mabeberu au ngombe dume wanono wa Basani.

19Katika karamu hiyo niliyowafanyia watakula mafuta na kushiba. Watakunywa damu na kulewa.

20Kwenye meza yangu, watashibishwa kwa farasi, waaskari wapanda-farasi, mashujaa na watu wote wa vita.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Waisraeli watarudi katika inchi yao

21Yawe akaniambia hivi: Nitaonyesha utukufu wangu kwa mataifa yote, na kuwaonyesha jinsi ninavyotumia nguvu yangu kwa kutimiza hukumu zangu za haki.

22Waisraeli watajua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wao, tangu siku hiyo na itakayokuja.

23Mataifa yatajua kwamba Waisraeli walikwenda katika uhamisho kutokana na makosa yao wenyewe waliyonikosea. Waliniasi, nami nikageuka wasipate kuniona, nikawatoa katika mikono ya waadui zao wakauawa.

24Niligeuka wasipate kuniona nikawatendea kulingana na uchafu na makosa yao.

25Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema hivi: Sasa nitawahurumia Waisraeli wazao wa Yakobo, na kuwarudishia fanaka yao. Ninataka jina langu takatifu liheshimiwe siku zote.

26Watakapokuwa wanaishi kwa usalama katika inchi yao, bila kutishwa, watasahau haya yao na uasi walionitendea.

27Wakati huo, nitakuwa nimewarudisha kutoka kwa mataifa na kuwakusanya kutoka inchi za waadui zao na kuonyesha utakatifu wangu mbele ya mataifa mengi.

28Kisha watatambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wao, kwa sababu mimi niliwapeleka katika uhamisho kati ya mataifa na kuwarudisha tena katika inchi yao. Sitamwacha hata mutu wao mumoja abakie kati ya mataifa.

29Nitakapowajaza Waisraeli Roho yangu, sitageuka tena wasipate kuniona.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help