1Beni-Hadadi mufalme wa Aramu alikusanya waaskari wake wote. Aliungwa mukono na wafalme wengine makumi tatu na wawili pamoja na farasi na magari yao ya vita. Aliuendea muji wa Samaria akauzunguka na kuushambulia.
2Kisha, akatuma wajumbe wake katika muji kwa mufalme Ahabu wa Israeli, wakamwambia: “Mufalme Beni-Hadadi anasema hivi:
3‘Feza na zahabu yako yote ni mali yangu; wake zako wazuri na watoto wako ni wangu vilevile.’ ”
4Naye mufalme wa Israeli akajibu: “Bwana wangu mufalme, ulivyosema ni sawa: mimi ni wako, na vyote ninavyokuwa navyo ni vyako.”
5Nyuma, wajumbe wale wakarudia tena kwa Ahabu, wakamwambia: “Mufalme Beni-Hadadi anasema hivi: ‘Nilikutumia ujumbe kwamba unipe zahabu, feza, wake zako pamoja na watoto wako.
6Sasa, kesho kwa wakati kama huu, nitatuma watumishi wangu wakuje kutafutatafuta ndani ya nyumba yako na nyumba za watumishi wako, watwae na kupeleka kila kitu unachokiona kuwa cha bei kali.’ ”
7Halafu Ahabu mufalme wa Israeli akawaita viongozi wote wa inchi, akawaambia: “Sasa, muone jinsi mutu huyu anavyotaka kutuletea hasara! Ametuma ujumbe kwamba anataka wake zangu, watoto wangu, zahabu na feza yangu. Nami sikumukatalia!”
8Wazee na watu wote wakamwambia: “Usimujali wala usikubali.”
9Basi, Ahabu akawaambia wajumbe wa Beni-Hadadi: “Mumwambie bwana wangu mufalme hivi: ‘Nitafanya yote uliyoomba kwa mara ya kwanza, lakini haya ya pili sikubali hata kidogo.’ ”
Hapo, wajumbe hao wakaenda zao na kumupasha tena mufalme Beni-Hadadi.
10Beni-Hadadi akamutumia Ahabu ujumbe huu: “Miungu iniue ikiwa kule Samaria kutabakia mavumbi ya kutosha kwa kujaza vitanga vya mikono kwa kila mumoja wa watu wangu wengi wanaonifuata!”
11Mufalme Ahabu wa Israeli akajibu: “Mumwambie mufalme Beni-Hadadi kwamba shujaa anajisifu kisha kupigana vita, na si mbele ya vita!”
12Beni-Hadadi alipokea ujumbe huu wa Ahabu wakati yeye na wafalme waliomwunga mukono walipokuwa ndani ya mahema yao wakikunywa. Basi, akaweka waaskari wake tayari kwa kuushambulia muji ule.
13Wakati uleule, nabii mumoja akamwendea Ahabu, mufalme wa Israeli, akamwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Unaona wingi wa waaskari hawa? Leo hii nitawatia katika mikono yako, nawe utatambua kwamba mimi ndimi Yawe.’ ”
14Naye Ahabu akauliza: “Kwa musaada wa nani?”
Nabii akasema: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa musaada wa vijana wanaotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo.’ ”
Naye mufalme akauliza: “Ni nani atakayeanza kupigana?”
Nabii akajibu: “Wewe!”
15Basi, mufalme Ahabu akachunguza vijana waliotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo, jumla yao ilikuwa watu mia mbili makumi tatu na wawili. Kisha akachunguza waaskari wa Israeli, walikuwa waaskari elfu saba.
16Basi, wakati wa saa sita za muchana, Beni-Hadadi na wale wafalme wenzake makumi tatu na wawili waliomwunga mukono walipokuwa katika mahema yao wakikunywa na kulewa, mashambulizi yakaanza.
17Wale vijana waliotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo, wakatangulia. Wakati ule, Beni-Hadadi alikuwa amekwisha kupeleka waaskari wapelelezi, nao wakamupa habari kwamba kulikuwa kundi la watu waliokuja kutoka Samaria.
18Beni-Hadadi akawaambia: “Muwakamate wakiwa wazima. Hata kama wanakuja kwa vita au kwa amani.”
19Basi, wale vijana waliotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo, wakaongoza mashambulizi, na huku nyuma yao, waaskari wa Israeli waliwafuata.
20Kila mumoja wao akamwua adui mumoja. Watu wa Aramu wakakimbia, nao waaskari wa Israeli wakawafuatilia. Lakini Beni-Hadadi mufalme wa Aramu akapanda juu ya farasi, akatoroka na sehemu ya waaskari wapanda-farasi.
21Basi, mufalme wa Israeli akashinda vita, akateka farasi na magari ya vita mengi, na kuwaua Waaramu kwa wingi.
22Kisha, yule nabii akamwendea mufalme wa Israeli, akamwambia: “Uongeze nguvu yako, ufikiri vizuri la kufanya. Mwaka kesho, mufalme wa Aramu atakuja kukushambulia tena.”
Waaramu wanawashambulia tena watu wa Israeli23Watumishi wa mufalme Beni-Hadadi walimushauria hivi: “Miungu ya Waisraeli ni miungu ya juu ya milima; ndiyo maana tulishindwa. Lakini, bila shaka tutawashinda kama tukipigana nao katika bonde.
24Sasa, ufanye hivi: Uwaondoe wale wafalme makumi tatu na wawili katika madaraka yao na kwa pahali pao uweke majemadari.
25Ukusanye waaskari kama walewale uliopoteza, farasi na magari ya vita kama yale uliyopoteza. Kisha, tutapigana nao katika bonde na bila shaka tutawashinda.” Mufalme Beni-Hadadi akasikia shauri lao, akafanya hivyo.
26Halafu kwa mwaka uliofuata, mufalme Beni-Hadadi akawakusanya watu wake, akaenda katika muji wa Afeki kwa kupigana na watu wa Israeli.
27Nao watu wa Israeli walikusanywa na kupewa silaha, wakaenda kupigana na Waaramu. Watu wa Israeli walipiga kambi, wakaonekana kama vikundi vidogovidogo vya mbuzi, lakini Waaramu walijaa katika inchi.
28Halafu, mutu mumoja wa Mungu akamukaribia mufalme wa Israeli, akamwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa sababu Waaramu wamesema kwamba mimi Yawe ni Mungu wa milima wala si Mungu wa inchi ya bonde, nitakupa ushindi juu ya kundi hili kubwa, nawe utatambua kwamba mimi ni Yawe.’ ”
29Watu wa Israeli na Waaramu walipiga kambi kwa muda wa siku saba, wakielekeana. Siku ya saba, mapigano yakaanza. Siku hiyohiyo, watu wa Israeli wakaua waaskari wa miguu elfu mia moja.
30Waliobaki, walikimbilia katika muji wa Afeki. Kule, kuta za muji ziliwaangukia na kuwaua watu elfu makumi mbili na saba waliobakia. Beni-Hadadi vilevile alikimbia na kujificha katika chumba fulani cha ndani, katika muji.
31Watumishi wake wakamwendea, wakamwambia: “Tumesikia kwamba wafalme wa Israeli ni wema. Basi, uturuhusu tujifunge magunia kwenye viuno na kamba katika shingo, tumwendee mufalme wa Israeli. Labda atayaokoa maisha yako.”
32Basi, wakajifungia magunia kwenye viuno na kamba katika shingo yao, wakamwendea mufalme wa Israeli, wakamwambia: “Mutumishi wako, Beni-Hadadi, anakusihi akisema: ‘Tafazali, uniache nipate kuishi.’ ”
Ahabu akasema: “Kumbe angali anaishi? Yeye ni ndugu yangu.”
33Watumishi wa Beni-Hadadi walitambua kwamba masemi yake yalikuwa kitambulisho kizuri. Kwa hiyo wakasema: “Ndiyo, Ben-hadadi ni ndugu yako!”
Ahabu akawaambia: “Mwende mumulete kwangu.”
Basi, Beni-Hadadi alipofika, Ahabu akamuruhusu kuikaa pamoja naye katika gari lake la vita.
34Kisha, Beni-Hadadi akamwambia: “Miji yote ambayo baba yangu alimunyanganya baba yako, nitakurudishia. Unaweza kuanzisha masoko kule Damasiki kama vile baba yangu alivyofanya kule Samaria.”
Ahabu akajibu: “Nitakuachilia kwa masharti hayo.” Hapo, akafanya mapatano naye na kumwacha huru.
Nabii anamulaani Ahabu35Kwa amri ya Yawe, mumoja wa wanafunzi wa manabii akamwambia mwenzake: “Unipige, tafazali.” Lakini mwenzake akakataa kumupiga.
36Naye akamwambia: “Kwa sababu umekataa kutii amri ya Yawe, basi, mara tu utakapoachana nami, simba atakuua.” Na kweli, mara tu alipoachana naye, akakutana na simba, akamwua.
37Kisha, yule mwanafunzi akamukuta mutu mwingine, akamwambia: “Unipige, tafazali.” Mutu yule akamupiga na kumwumiza.
38Basi, nabii akajifunga kitambaa kwenye uso kusudi asitambuliwe, akaenda, akakaa pembeni ya njia kwa kumungojea mufalme wa Israeli.
39Mufalme alipokuwa anapita, nabii akamulilia akisema: “Bwana, mimi mutumishi wako nilikuwa kwa mustari wa mbele katika vita. Kukakuja askari mumoja, akaniletea mateka mumoja na kuniambia: ‘Umulinde mutu huyu. Akitoroka utalipa kwa maisha yako wewe peke yako, au kwa bei ya vikoroti elfu tatu vya feza.’
40Lakini nilipokuwa nikishugulikashugulika, mutu yule akatoroka.”
Mufalme wa Israeli akamwambia: “Ndivyo hukumu yako itakavyokuwa. Umejihukumu mwenyewe.”
41Hapo, nabii akaondoa harakaharaka kitambaa kwenye uso wake, naye mufalme akamutambua kuwa mumoja wa manabii.
42Basi, nabii akamwambia mufalme: “Yawe anasema hivi: ‘Umemwachilia akuponyoke mutu ambaye niliamuru auawe. Basi, maisha yake utalipa kwa maisha yako, na watu wake kwa watu wako.’ ”
43Basi, mufalme wa Israeli akaenda zake kwake Samaria, akijaa chuki na huzuni nyingi.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.