1 Samweli 18 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Saulo alipomaliza kuzungumuza na Daudi, Yonatani mwana wa Saulo alivutwa sana na Daudi, akamupenda kwa moyo wake wote kama alivyojipenda yeye mwenyewe.

2Tangu siku ile, Saulo akamutwaa Daudi katika nyumba yake, hakumuruhusu kurudi kwenye nyumba ya baba yake.

3Kwa sababu Yonatani alimupenda Daudi kama roho yake, alifanya agano naye.

4Alivua nguo aliyovaa na kumupa Daudi pamoja na silaha zake, hata upanga, upinde na mukaba wake.

5Kokote Daudi alikotumwa na Saulo, Daudi alifanikiwa. Hivyo, Saulo akamufanya kuwa mukubwa wa waaskari wake. Jambo hilo liliwafurahisha watu wote hata watumishi wa Saulo.

Saulo anamusikilia Daudi wivu

6Waaskari walipokuwa wanarudi kwenye nyumba, pamoja na Daudi kisha kumwua yule Mufilistini, wanawake kutoka kila muji katika Israeli walitoka kwenda kumupokea mufalme Saulo. Wanawake nao walikuwa wanaimba nyimbo za furaha, wakipiga matari na vinubi.

7Vilevile walikuwa wanacheza na kuimba nyimbo za kuitikiana hivi:

“Saulo ameua maelfu yake,

na Daudi ameua elfu yake makumi.”

8Saulo hakupendezwa na maneno ya wimbo huo. Akakasirika sana. Akasema: “Wamemupa Daudi elfu makumi, lakini mimi wamenipa maelfu tu. Linalobakia ni kumupa Daudi ufalme.”

9Tangu siku hiyo, Saulo akakuwa anamusikilia Daudi wivu.

10Kesho yake, pepo muchafu kutoka kwa Mungu akamushambulia Saulo kwa rafla, akakuwa anapayukapayuka kama mwenda-wazimu katika nyumba yake. Daudi alikuwa anapiga kinubi kama alivyofanya siku zote. Saulo alikuwa na mukuki katika mukono wake.

11Basi, alimutupia Daudi mukuki mara mbili maana alifikiri: “Nitamubanisha Daudi kwenye ukuta.” Lakini Daudi aliepa mara zote mbili.

12Saulo alikuwa anamwogopa Daudi kwa sababu Yawe alikuwa pamoja naye, lakini Yawe alikuwa amemwacha Saulo.

13Hivyo, Saulo akamwondoa na kumufanya kiongozi wa waaskari elfu moja. Naye Daudi akawaongoza vyema katika vita.

14Daudi alifanikiwa katika kila kitu alichofanya, maana Yawe alikuwa pamoja naye.

15Saulo alipoona kufanikiwa kwa Daudi, akakuwa anamwogopa.

16Lakini watu wote wa Israeli na Yuda walimupenda Daudi, maana ndiye aliwaongoza vizuri katika vita na kuwarudisha na mafanikio.

Daudi anamwoa binti ya Saulo

17Saulo akamwambia Daudi: “Huyu ni Merabu, binti yangu mukubwa, nitamutoa kwako kusudi umwoe kwa masharti mawili: Ukuwe askari wangu shujaa na mutiifu, upigane vita ya Yawe.” Saulo alizani kwa njia hiyo Wafilistini watamwua Daudi, kusudi kitendo hicho asikifanye yeye mwenyewe.

18Daudi akamwambia Saulo: “Mimi ni nani hata mufalme akuwe baba mukwe wangu? Ukoo wangu wenyewe na hata jamaa ya baba yangu si kitu katika Israeli.”

19Lakini, wakati ule ambapo Merabu binti ya Saulo angeoeshwa kwa Daudi, alioeshwa kwa Adrieli kutoka muji wa Mehola.

20Hata hivyo, Mikali binti mwingine wa Saulo alimupenda Daudi. Saulo alipoambiwa habari ile alifurahi sana.

21Saulo alifikiri: “Ngoja nitamutoa Mikali kusudi akuwe mutego kwake. Na bila shaka Wafilistini watamwua.” Hivyo Saulo akamwambia Daudi kwa mara ya pili: “Sasa nitakuwa baba mukwe wako.”

22Halafu Saulo aliwaamuru watumishi wake akisema: “Museme na Daudi kwa siri na kumwambia: ‘Mufalme anapendezwa sana nawe, hata watumishi wake vilevile wote wanakupenda’. Hivyo, sasa ukubali kuwa mukwe wa mufalme.”

23Basi, watumishi hao wa Saulo walimwambia Daudi maneno hayo kwa siri, naye akawaambia: “Munazani mufalme kuwa baba mukwe wangu ni jambo dogo? Mimi ni mutu masikini na wa hali ya chini.”

24Wale watumishi walimwelezea Saulo kama vile Daudi alivyosema.

25Saulo akawaambia: “Mumwambie Daudi hivi: ‘Kile ambacho mufalme anataka kama vile mali kwa binti yake ni magovi mia moja ya Wafilistini, kusudi ajilipize kisasi kwa waadui zake.’ ” Hivi ndivyo Saulo alivyopanga kusudi Daudi auawe na Wafilistini.

26Wale watumishi walipomwelezea Daudi yale mapenzi ya Saulo, Daudi alifurahi kwamba mufalme atakuwa baba mukwe wake. Mbele ya siku ya arusi,

27Daudi na watu wake walikwenda, wakawaua Wafilistini mia mbili na kuyatwaa magovi yao mpaka kwa mufalme Saulo. Hapo akamuhesabilia hesabu kamili kusudi mufalme akuwe baba mukwe wa Daudi. Hivyo, Saulo akamupatia Daudi binti yake Mikali akuwe muke wake.

28Lakini Saulo alipoona wazi kwamba Yawe alikuwa pamoja na Daudi, na kwamba Mikali binti yake alimupenda sana Daudi,

29alizidi kumwogopa Daudi. Saulo akakuwa adui wa Daudi siku zote.

30Waaskari wa Wafilistini walikwenda kupigana na Waisraeli, lakini kila mara walipopigana vita, Daudi alipata ushindi kuliko watumishi wa Saulo. Hivyo jina la Daudi likazidi kusifiwa sana.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help