2 Mambo ya Siku 22 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufalme Ahazia wa Yuda(2 Fal 8.25-29; 9.21-28)

1Wakaaji wa Yerusalema wakamupa Ahazia mwana mudogo wa Yoramu ufalme, atawale pahali pa baba yake kwa sababu wakubwa wake wote waliuawa na kikundi fulani kilichokuja katika kambi pamoja na Waarabu. Hivyo, Ahazia mwana wa Yoramu, mufalme wa Yuda, akatawala.

2Ahazia, alianza kutawala akiwa mwenye umri wa miaka makumi ine na miwili, akatawala kutoka Yerusalema kwa muda wa mwaka mumoja. Mama yake aliitwa Atalia, mujukuu wa Omuri.

3Kwa sababu mama yake alikuwa mushauri wake katika kutenda maovu, naye vilevile alifuata mienendo ya jamaa ya Ahabu.

4Alitenda maovu mbele ya Yawe kama vile jamaa ya Ahabu ilivyofanya maana hao ndio waliokuwa washauri wake nyuma ya kifo cha baba yake, mpaka kwa kuangamia kwake.

5Hata akafuata shauri lao, akaenda pamoja na mufalme Yoramu mwana wa Ahabu mufalme wa Israeli kupigana vita na Hazaeli mufalme wa Suria kule Ramoti-Gileadi. Nao Wasuria wakamwumiza Yoramu.

6Kisha akarudi Yezereheli kusudi apate kutunzwa vidonda alivyopata kule Rama, wakati alipopigana na Hazaeli mufalme wa Suria. Naye Ahazia mwana wa Yoramu mufalme wa Yuda akamutembelea Yoramu mwana wa Ahabu kule Yezereheli kwa sababu alikuwa mugonjwa.

7Lakini ilikuwa imepangwa na Mungu kwamba maangamizi yatendeke kwa Ahazia kwa njia hiyo ya kumutembelea Yoramu; kwa sababu alipofika kule, alitoka pamoja na Yoramu kwenda kupigana na Yehu mwana wa Nimusi ambaye Yawe alimuchagua kwa kuangamiza uzao wa Ahabu.

8Wakati Yehu alipokuwa akiwahukumu watu wa jamaa ya Ahabu alikutana na wakubwa wa Yuda pamoja na wana wa wandugu za Ahazia, waliomutumikia Ahazia, akawaua.

9Akamutafuta Ahazia, naye akakamatwa akiwa amejificha kule Samaria. Wakamuleta mpaka kwa Yehu, akauawa. Wakauzika mwili wake maana walisema: “Yeye ni mujukuu wa Yosafati, ambaye alimutafuta Yawe kwa moyo wake wote.”

Hapakubaki hata mutu mumoja wa jamaa ya Ahazia ambaye angeweza kushika ufalme.

Malkia Atalia wa Yuda(2 Fal 11.1-3)

10Lakini wakati Atalia mama ya Ahazia alipoona kwamba mwana wake ameuawa, alitoka akaangamiza jamii yote ya kifalme ya Yuda.

11Lakini Yoseba, binti ya mufalme Yoramu alimutwaa Yoasi, akamuchukua kwa siri kutoka kati ya wana wa mufalme waliokuwa karibu kuuawa. Akamuficha yeye pamoja na yaya wake, katika chumba cha kulala. Hivyo Yoseba, binti ya mufalme Yoramu, muke wa kuhani Yoyada, kwa sababu alikuwa dada ya Ahazia, akamuficha Yoasi kusudi Atalia asimwone na kumwua.

12Naye akakaa nao kwa muda wa miaka sita akiwa amefichwa ndani ya nyumba ya Mungu wakati Atalia alipokuwa akitawala inchi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help