1Watu waliotembea katika giza
wameona mwangaza mukubwa.
Watu walioishi katika inchi ya giza kubwa,
sasa mwangaza umewaangazia.
2Wewe, ee Mungu, umeongoza taifa,
umezidisha furaha yake.
Watu wanafurahi mbele yako
wana furaha kama kwa wakati wa mavuno,
kama vile wanaogawanya vitu walivyonyanganya wanavyofurahi.
3Maana miti mizito waliyobeba,
nira walizokuwa wamefungwa,
na fimbo ya wasimamizi,
umezivunjavunja kama wakati wa Wamidiani.
4Viatu vyote vya washambulizi katika vita
na nguo zote zenye kujaa damu
vitateketezwa kama kuni za kuwasha moto.
5Maana mutoto amezaliwa kwa ajili yetu,
tumepewa mutoto mwanaume.
Naye atapewa mamlaka ya kutawala.
Ataitwa: “Mushauri wa Ajabu”,
“Mungu Mwenye Nguvu”,
“Baba wa Milele”,
“Mufalme wa Amani”.
6Utawala wake utastawi siku zote,
amani ya ufalme wake haitakoma.
Atakamata madaraka ya mufalme Daudi
na kutawala juu ya ufalme wake;
ataustawisha na kuuimarisha
kwa kufuata sheria ya Mungu na kutenda kwa haki
tangu sasa na hata milele.
Yawe wa majeshi atafanya mambo hayo. Azabu ya Waisraeli
7Yawe ametoa neno juu ya Yakobo
nalo litamupata Israeli.
8Watu wote watatambua,
ukoo wote wa Efuraimu
na wakaaji wa Samaria.
Kwa kiburi na majivuno wanasema:
9Kuta za matofali zimeanguka
lakini sisi tutazijenga kwa mawe yaliyochongwa!
Nyumba za nguzo za mikuyu zimeharibiwa
lakini pahali pake tutajenga za mierezi.
10Basi, Yawe atawaletea wapinzani
na kuwachochea waadui zao.
11Waasuria kwa upande wa mashariki,
Wafilistini kwa upande wa magaribi,
wamepanua vinywa vyao kwa kuimeza Israeli.
Hata hivyo, hasira yake haijatulia,
angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu.
12Ingawa aliwaazibu watu,
hawakumurudilia Yawe wa majeshi.
13Yawe atakata katika Israeli kichwa na mukia,
tawi la mingazi na nyasi,
kwa muda wa siku moja tu.
14Kichwa ni wazee na waheshimiwa,
mukia ni manabii wanaofundisha uongo.
15Wale wanaoongoza watu hawa wamewapotosha,
na hao wanaoongozwa nao wamepotoka.
16Kwa hiyo, Yawe hawahurumii vijana wao,
hana huruma juu ya wayatima na wajane wao;
maana hakuna hata mumoja anayemufuata,
kila mutu anasema upumbafu.
Hata hivyo, hasira yake haijatulia,
angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu.
17Uovu unawaka kama moto
unaoteketeza michongoma na miiba;
unawaka kama moto katika pori,
na kutoa moshi muzito unaopanda juu katika anga.
18Kwa kasirani ya Yawe wa majeshi
inchi imechomwa moto,
na watu ni kama kuni za kuuwasha.
Hakuna mutu anayemuhurumia ndugu yake;
19wananyanganya upande mumoja na hawatosheki;
wanakula upande mwingine lakini hawashibi.
Kila mumoja anamushambulia mwenzake.
20Manase anashambulia Efuraimu,
Efuraimu anashambulia Manase
na wote wawili wanashambulia Yuda.
Hata hivyo, hasira ya Yawe haijatulia,
angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.