2 Wafalme 15 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufalme Azaria wa Yuda(2 Sik 26.1-23)

1Katika mwaka wa makumi mbili na saba wa kutawala kwa Yeroboamu mufalme wa Israeli, Azaria mwana wa Amazia, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala.

2Alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka makumi tano na miwili akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalema.

3Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile baba yake Amazia alivyotenda.

4Hata hivyo, nafasi za kutambikia kwenye milima hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambika na kufukiza ubani pale.

5Yawe akamwazibu Azaria, akakuwa na ukoma mpaka alipokufa. Alikaa katika nyumba ya pekee na shuguli zake zote za utawala ziliendeshwa na mwana wake Yotamu.

6Mambo mengine ya Azaria na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda.

7Azaria akakufa na kuzikwa katika makaburi ya wafalme katika muji wa Daudi; na mwana wake Yotamu akatawala kwa pahali pake.

Mufalme Zakaria wa Israeli

8Katika mwaka wa makumi tatu na nane wa utawala wa Azaria mufalme wa Yuda, Zakaria mwana wa Yeroboamu akaanza kutawala Israeli. Akatawala kwa muda wa miezi sita.

9Naye, kama vile watangulizi wake, alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi zile za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi.

10Salumu mwana wa Yabesi alimwasi, akamupiga mbele ya watu na kumwua, kisha akatawala kwa pahali pake.

11Matendo mengine yote ya Zakaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli.

12Basi tukio hilo lilitokana na ahadi ya Yawe kwa mufalme Yehu, kusema: “Wazao wako watatawala Israeli mpaka kizazi cha ine.”

13Katika mwaka wa makumi tatu na tisa wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Salumu mwana wa Yabesi akaanza kutawala Israeli na akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa mwezi mumoja.

14Menahemu mwana wa Gadi aliondoka Tirza kwenda Samaria, na kule akamupiga Salumu mwana wa Yabesi, kisha akatawala kwa pahali pake.

15Matendo mengine yote ya Salumu na uasi wake, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli.

16Menahemu alipokuwa katika njia kutoka Tirza, aliuharibu kabisa muji wa Tapua na kuangamiza wakaaji wake pamoja na inchi yote iliyouzunguka kwa sababu hawakujitoa kwake. Vilevile akapasua tumbo za wanawake wenye mimba.

Mufalme Menahemu wa Israeli

17Katika mwaka wa makumi tatu na tisa wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Menahemu mwana wa Gadi akaanza kutawala Israeli. Akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka kumi.

18Alitenda maovu mbele ya Yawe. Hakuacha maovu ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi.

19Basi, Puli mufalme wa Asuria akashambulia inchi ya Israeli, naye Menahemu akamupa kilo elfu makumi tatu na ine za feza kusudi amusaidie kuimarisha mamlaka yake juu ya inchi ya Israeli.

20Menahemu alipata feza hiyo kwa kuwalazimisha watajiri wa Israeli kutoa muchango wa vikoroti makumi tano vya feza kila mumoja. Halafu Puli hakukaa Israeli lakini akarudi katika inchi yake.

21Mambo mengine ya Menahemu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli.

22Menahemu akakufa, naye mwana wake Pekahia akatawala kwa pahali pake.

Mufalme Pekahia wa Israeli

23Katika mwaka wa makumi tano wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Pekahia mwana wa Menahemu akaanza kutawala Israeli. Akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka miwili.

24Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi.

25Peka mwana wa Remalia, ambaye alikuwa mukubwa wa waaskari wa Pekahia, alishirikiana na watu wengine makumi tano kutoka Gileadi, akamwua Pekahia katika chumba cha ndani cha nyumba ya mufalme kule Samaria na kuwa mufalme kwa pahali pake.

26Mambo mengine ya Pekahia na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli.

Mufalme Peka wa Israeli

27Katika mwaka wa makumi tano na mbili wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Peka mwana wa Remalia akaanza kutawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka makumi mbili.

28Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi.

29Wakati wa utawala wa Peka mufalme wa Israeli, Tigilati-Pileseri, mufalme wa Asuria, aliteka miji ya Iyoni, Abeli-Beti-Maka, Yanoa, Kadesi na Hazori, pamoja na inchi za Gileadi, Galilaya na Nafutali na kuwahamisha wakaaji wake kwenda Asuria.

30Katika mwaka wa makumi mbili wa utawala wa Yotamu mwana wa Uzia mufalme wa Yuda, Hoshea mwana wa Ela alimwasi Peka mwana wa Remalia na kumwua, kisha akatawala kwa pahali pake.

31Mambo mengine ya Peka na yote aliyoyafanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli.

Mufalme Yotamu wa Yuda(2 Sik 27.1-9)

32Katika mwaka wa pili wa utawala wa Peka mwana wa Remalia katika inchi ya Israeli, Yotamu mwana wa Uzia, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala Yuda.

33Alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala akiwa kule Yerusalema kwa muda wa miaka kumi na sita. Mama yake aliitwa Yerusa, binti ya Zadoki.

34Yotamu alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile baba yake Uzia alivyotenda.

35Hata hivyo, nafasi za kutambikia miungu ya uongo hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambikia na kufukiza ubani kwenye nafasi za juu. Yotamu alijenga mulango wa kaskazini wa nyumba ya Yawe.

36Mambo mengine ya Yotamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda.

37Wakati wa utawala wa Yotamu, Yawe akaanza kutuma mufalme Resini wa Aramu na mufalme Peka wa Israeli kwa kushambulia inchi ya Yuda.

38Yotamu akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi. Mwana wake Ahazi akatawala kwa pahali pake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help