2 Samweli 20 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Uasi wa Seba

1Sasa ilitokea kwamba kule Gilgali kulikuwa mutu mumoja wa ovyoovyo anayeitwa Seba mwana wa Bikiri, wa kabila la Benjamina. Basi Seba alipiga baragumu, na kusema: “Hatuna ushirika wowote na Daudi; hatuna sehemu yetu katika huyo mwana wa Yese. Enyi watu wa Israeli, kila mumoja ajiendee katika hema yake!”

2Kwa hiyo, watu wote wa Israeli wakamwacha Daudi, wakamufuata Seba mwana wa Bikiri. Lakini watu wa Yuda walimufuata mufalme Daudi kwa uaminifu toka muto Yordani mpaka Yerusalema.

3Nyuma, Daudi alifika katika nyumba yake kule Yerusalema. Mufalme aliwatwaa wahabara wake kumi ambao alikuwa amewaacha kwa kuangalia nyumba yake, akawaweka kwenye nyumba moja wapate kulindwa, akawatunza vizuri, lakini hakulala nao. Kwa hiyo wahabara hao wakakuwa wakifungwa mpaka siku za kufa kwao, wakaishi kama vile walikuwa wajane.

4Kisha, mufalme akamwambia Amasa: “Unikusanyie watu wote wa Yuda katika siku tatu, na wewe mwenyewe ukuwe pale.”

5Basi, Amasa akaenda kuwaita watu wa Yuda. Lakini akachelewa kurudi katika wakati ule aliopangiwa na mufalme.

6Daudi akamwambia Abisayi: “Sasa, Seba mwana wa Bikiri, atatuletea taabu kuliko Abusaloma. Twaa watumishi wangu, umufuate Seba kusudi asiingie kwenye miji yenye kuta na kuponyoka tusimwone tena.”

7Abisayi akatoka akiwa pamoja na Yoabu, Wakereti na Wapeleti pamoja na mashujaa wote. Hao wote waliondoka Yerusalema kwenda kumufuata Seba mwana wa Bikiri.

8Walipofika kwenye jiwe kubwa linalokuwa kule Gibeoni, Amasa akatoka kwenda kuwapokea. Yoabu alikuwa akivaa nguo ya kiaskari, na ndani ya nguo ile kulikuwa mukaba ulioshikilia upanga kwenye kiuno chake ukiwa kwenye mufuko wake. Yoabu alipokuwa anakaribia, upanga wake ulichomoka ndani ya mufuko ukaanguka chini.

9Yoabu akamwambia Amasa: “Habari gani ndugu yangu?” Yoabu akamushika Amasa kwenye kidevu kwa mukono wa kuume sawa vile anataka kumubusu.

10Lakini Amasa hakuona upanga uliokuwa katika mukono wa Yoabu. Basi, Yoabu akamuchoma Amasa upanga ndani ya tumbo, matumbotumbo yake yakatoka inje, akakufa. Yoabu hakumuchoma upanga mara mbili.

Kisha, Yoabu na ndugu yake Abisayi wakaendelea kumufuatilia Seba mwana wa Bikiri.

11Mutu mumoja wa Yoabu akakuja akasimama karibu na mwili wa Amasa, akasema: “Yeyote anayemupenda Yoabu na yeyote anayemupenda Daudi, amufuate Yoabu!”

12Amasa alikuwa bado anagaagaa ndani ya damu yake katikati ya barabara kubwa. Kwa hiyo, kila mutu aliyepita pale, alipomwona, alisimama. Lakini yule mutu alipoona kwamba watu wote walikuja na kusimama pale, aliuondoa mwili wa Amasa ndani ya barabara, akaupeleka katika shamba na kuufunika kwa nguo.

13Amasa alipoondolewa kwenye barabara kubwa, watu wote sasa waliendelea kumufuata Yoabu kwa kumufuatilia Seba mwana wa Bikiri.

14Seba alipita katika makabila yote ya Israeli mpaka katika muji wa Abeli wa Beti-Maka. Watu wote wa ukoo wa Bikiri wakakusanyika na kumufuata.

15Watu wote waliokuwa pamoja na Yoabu wakaenda kumuzunguka Seba akiwa katika muji ule wa Abeli wa Beti-Maka. Walilundika udongo kwa kuzunguka muji, na makimbilio. Halafu wakaanza kuubomoa ukuta kwa kuuangusha chini.

16Kisha, mwanamuke mumoja mwenye hekima alisikilika kutoka muji akisema: “Musikie! Musikie! Mumwambie Yoabu akuje nizungumuze naye.”

17Yoabu akaenda karibu naye, huyo mwanamuke akamwambia: “Wewe ndiwe Yoabu?”

Yoabu akasema: “Ndiyo! Ni mimi.”

Yule mwanamuke akamwambia: “Unisikilize mimi mujakazi wako.”

Yoabu akamwambia: “Ninasikiliza.”

18Yule mwanamuke akamwambia: “Zamani watu walikuwa wakisema: ‘Muache waombe shauri kutoka muji wa Abeli’. Ndivyo watu walivyoweza kutatua matatizo.

19Mimi ni mumoja wa wale wanaopenda amani na uaminifu katika Israeli. Sasa wewe unakusudia kuuharibu muji ambao ni sawa vile katika Israeli. Kwa nini sasa unataka kuuangamiza muji unaokuwa mali ya Yawe?”

20Yoabu akamujibu: “Hata kidogo katika maisha yangu! Sina nia ya kuangamiza wala kuharibu.

21Ulivyosema si kweli! Lakini mutu mumoja kutoka sehemu ya milima ya Efuraimu anayeitwa Seba mwana wa Bikiri anataka kumwasi mufalme Daudi. Mumutoe kwangu nami nitaondoka katika muji wenu.”

Yule mwanamuke akamwambia Yoabu: “Kichwa chake kitarushwa kwako kupitia juu ya ukuta.”

22Kisha, huyo mwanamuke akaenda kwa watu wote katika muji kwa hekima yake. Wakamukata Seba mwana wa Bikiri kichwa, wakakitupa inje kwa Yoabu. Kwa hiyo, Yoabu akapiga baragumu na kuwatawanya watu wake kutoka muji ule wa Abeli. Kila mutu akaenda kwake. Yoabu akarudi kwa mufalme Daudi, kule Yerusalema.

Majina ya wasaidizi wa Daudi

23Sasa Yoabu alikuwa jemadari wa waaskari wote wa Waisraeli. Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa jemadari wa Wakereti na Wapeleti.

24Adoramu alikuwa musimamizi wa kazi za kulazimishwa. Yeosafati alikuwa mwandishi wa habari za kifalme.

25Sewa alikuwa katibu. Zadoki na Abiatari walikuwa makuhani.

26Ira wa muji Yairi alikuwa vilevile kuhani wa Daudi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help