1Yobu akamujibu Elifasi:
2Heri uchungu wangu ungepimwa,
nayo mateso yangu yote yangewekwa katika mizani!
3Yangekuwa mazito kuliko muchanga wa bahari.
Ni kwa hiyo maneno yangu hayana maana!
4Mishale ya Mungu Mwenye Uwezo imenichoma;
nafsi yangu imekunywa sumu yake.
Vitisho vya Mungu vimenipata.
5Punda wa pori analia akiwa na majani,
au ngombe akiwa na malisho?
6Kitu kisichokuwa na onjo kinaweza kuliwa bila chumvi?
Sehemu nyeupe ya yai ina utamu wowote?
7Sina hamu ya kuvigusa vyakula hivyo,
hivyo ni vyakula vinavyonichukiza.
8Heri ningejibiwa kwa ombi langu,
Mungu angenipatia kile ninachotamani,
9angependezwa kunipondaponda,
angenyoosha mukono wake juu yangu na kuniua!
10Hiyo ingekuwa faraja yangu,
ningefurahi katika maumivu yasiyokuwa na huruma,
kwa sababu sikukataa maagizo ya Mungu Mutakatifu.
11Sina nguvu ya kuweza kuendelea.
Sijui mwisho wangu utakuwa namna gani, nipate kuvumilia.
12Nguvu zangu ni kama za mawe?
Au mwili wangu kama shaba?
13Kweli kwangu hakuna kitu cha kunisaidia;
musaada wowote ni mbali nami.
14Anayekataa kutendea mema rafiki yake,
anakataa kumwogopa Mungu Mwenye Uwezo.
15Warafiki zangu wamenidanganya kama kijito,
wamenidanganya kama mifereji isiyokuwa na maji,
16ambayo imejaa barafu,
na teluji imejificha ndani yake.
17Wakati wa kipwa inatoweka,
wakati wa jua kali inakauka.
18Wasafiri wanapotea njia zao wakitafuta maji,
wanapanda katika jangwa na kukufia kule.
19Wasafiri toka Tema wanatafutatafuta,
wasafiri toka Sheba wanatumainia.
20Wanachukizwa kwa kutumainia bure,
wanafika kwenye vijito hivyo na kuuzika.
21Ninyi mumekuwa kama vijito hivyo,
munaona hasara yangu na kuogopa.
22Nimesema munipe zawadi?
Au munitolee sehemu ya mali zenu?
23Au muniokoe toka katika mikono ya adui?
Au munikomboe toka katika mukono wa watesaji?
24Munifundishe, nami nitanyamaza.
Munieleweshe jinsi nilivyokosa.
25Maneno ya kweli yana nguvu kubwa!
Lakini makaripio yenu yanafaa kwa nini?
26Munazani kwamba munaweza kuchunguza maneno?
Maneno ya mutu aliyekata tamaa ni upepo tu.
27Ninyi munasubutu hata kuwapigia wayatima kura;
munauzisha hata rafiki yenu!
28Lakini sasa muniangalie tafazali.
Mimi sitasema uongo mbele yenu.
29Tafazali mugeuke, kusikuwe uovu;
muache sasa, kwa ajili ya haki yangu.
30Munazani kwamba nimesema uovu?
Munafikiri kwamba mimi siyatambui machungu?
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.