Marko 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yesu anatangaza uharibifu wa hekalu(Mat 24.1-2; Lk 21.5-6)

1Yesu alipokuwa akitoka katika hekalu, mumoja kati ya wanafunzi wake akamwambia: “Mwalimu, angalia mawe haya mazuri na majengo haya makubwa!”

2Yesu akamujibu: “Unaona majengo haya makubwa? Hakutabaki hata jiwe moja juu ya lingine; yote yatabomolewa.”

Mateso yatakayokuwa mbele ya kurudi kwa Yesu(Mat 24.3-14; Lk 21.7-19)

3Yesu alipokuwa akiikaa kwa mulima wa Mizeituni kuelekea upande wa hekalu, Petro, Yakobo, Yoane na Andrea walipokuwa peke yao pamoja naye, wakamwuliza:

4“Utuambie, mambo hayo uliyotoka kusema yatakuwa wakati gani? Na ni kitambulisho gani kitakachoonyesha kwamba mambo hayo yote yanataka kutimia?”

5Basi Yesu akaanza kuwaambia: “Muangalie vizuri mutu asiwadanganye.

6Watu wengi watakuja wakijiita kwa jina langu, wakisema: ‘Mimi ni Kristo!’ Nao watawadanganya wengi.

7Mutakaposikia habari za matokeo au utetezi wa vita musiogope. Sherti mambo hayo yatukie, lakini hayaonyeshi kama mwisho umefika.

8Kwa maana taifa litapigana na taifa, na ufalme utapigana na ufalme. Kutakuwa tetemeko la inchi pahali mbalimbali. Vilevile kutakuwa njaa. Na haya yote ni kama mwanzo wa maumivu ya kuzaa tu.

9“Mujiangalie vizuri ninyi wenyewe, kwa maana watawapeleka mbele ya tribinali kwa kuwahukumu na kuwapiga fimbo katika nyumba za kuabudia. Vilevile mutapelekwa mbele ya wakubwa na wafalme kwa ajili yangu, kusudi mutoe ushuhuda wangu mbele yao.

10Ni lazima Habari Njema ihubiriwe kwanza kwa watu wa kila taifa.

11Na mutakapokamatwa na kupelekwa kwa kuhukumiwa, musijihangaishe mbele ya wakati juu ya maneno mutakayosema, lakini museme maneno mutakayopewa saa ile ile. Kwa sababu hayatatoka kwenu wenyewe, lakini yatatoka kwa Roho Mutakatifu.

12Ndugu atamutoa ndugu, kusudi auawe, na baba atatoa mutoto wake, nao watoto watawageukia wazazi wao na kuwaua.

13Na watu wote watawachukia kwa ajili yangu. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho, ataokolewa.

Chukizo la uharibifu(Mat 24.15-28; Lk 21.20-24)

14“Lakini mutamwona yule anayeitwa ‘Chukizo Linaloleta Uharibifu,’ akisimamishwa pahali asipopaswa kuwa. (Anayesoma maneno haya aelewe maana yake). Basi watakaokuwa Yudea, wakimbilie kwa milima.

15Atakayekutiwa juu ya paa la nyumba asishuke na kuingia ndani ya nyumba kutwaa kitu.

16Na mutu atakayekutiwa katika shamba, asirudi kwake kwa kutwaa nguo yake.

17Wanawake wenye mimba na wenye kunyonyesha watapata hasara katika siku zile.

18Mumwombe Mungu kusudi mambo hayo yasitokee katika wakati wa mvua.

19Kwa maana katika siku zile kutakuwa mateso makubwa yasiyoonekana hata kidogo tangu siku ile Mungu alipoumba ulimwengu mpaka sasa, wala hakutatokea tena mateso kama yale.

20Na kama Bwana asingepunguza siku zile za mateso, hakuna hata mutu mumoja ambaye angeponyoka kufa. Lakini kwa ajili ya wachaguliwa aliowachagua amezipunguza.

21“Kwa hiyo mutu akiwaambia: ‘Kristo yuko hapa!’ au ‘Yuko kule!’ musimusadiki.

22Kwa maana kutatokea watu wanaojiita kwa uongo ‘Kristo’ pamoja na manabii wa uongo, nao watafanya vitambulisho na maajabu, kusudi ikiwezekana wawadanganye wachaguliwa wa Mungu.

23Lakini ninyi mujiangalie vizuri, kwa maana nimewaambia hayo yote mbele.

Kurudi kwa Mwana wa Mutu(Mat 24.29-31; Lk 21.25-28)

24“Lakini katika siku zile kisha mateso yale, jua litatiwa giza, mwezi hautaangaza,

25nyota zitaanza kuanguka toka mbinguni na vyote vyenye nguvu vinavyokuwa katika mbingu vitatikiswa.

26Na halafu wakati ule Mwana wa Mutu ataonekana akikuja katikati ya mawingu kwa uwezo mwingi na kwa utukufu.

27Halafu atawatuma wamalaika wake katika pande ine za dunia, naye atakusanya watu wake aliowachagua kutoka katika dunia nzima.

Mafundisho kutoka muti wa tini(Mat 24.32-35; Lk 21.29-33)

28“Muangalilie mufano juu ya muti wa tini. Wakati matawi yake yanapochipuka, nayo majani yao yanapochipuka, ninyi munatambua kwamba wakati wa jua kali unakaribia.

29Vilevile, wakati mutakapoona mambo hayo niliyotoka kutaja yanatokea, mujue kwamba yeye yuko karibu, na amekuwa kwa mulango.

30Kweli ninawaambia: hiki kizazi chenu hakitapita mbele ya kutimia kwa mambo haya yote.

31Mbingu na dunia vitatoweka, lakini maneno yangu hayatabadilika hata kidogo.

Mungu pekee anajua wakati wa mwisho(Mat 24.36-44)

32“Lakini hakuna mutu anayejua siku ile au saa, hata wamalaika wanaokuwa mbinguni, hata Mwana; isipokuwa Baba peke yake tu.

33Mujiangalie, mukeshe, kwa maana hamujui saa wakati ule utakapotimia.

34Itakuwa kama vile mutu anayefunga safari. Alipotoka kwake akawaachia watumishi madaraka yake, akimupa kila mutu kazi yake. Vilevile akamwagiza mulinzi wa mulango akeshe.

35Basi muangalie sababu hamujui wakati bwana wa nyumba atakaporudi: labda magaribi, au katikati ya usiku, au wakati jogoo anapowika, au asubui.

36Mujiangalie, asikuje kwa rafla na kuwakuta mumelala usingizi.

37Mambo ninayowaambia ninyi, ninayasema kwa wote: mukeshe.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help