1Wafalme wote waliokuwa ngambo ya muto Yordani katika inchi ya milima na kwenye mabonde na eneo lote la pembeni ya bahari ya Mediteranea kuelekea Lebanoni, Wahiti, Waamori, Wakanana, Waperizi, Wahivi na Wayebusi waliposikia habari za Waisraeli,
2wakakusanyika pamoja kwa nia moja kwa kupigana vita na Yoshua na Waisraeli.
3Lakini wakaaji wa Gibeoni walipopata habari juu ya jinsi Yoshua alivyoitendea miji ya Yeriko na Ai,
4waliamua kutumia werevu. Wakatayarisha vyakula, wakapakiza magunia yaliyochakaa juu ya punda wao, vibuyu vilivyochakaa na kushonwa.
5Wakavaa viatu, nguo zilizochakaa na vyakula vyao vyote vilikuwa vimekauka na kuota manyoya.
6Basi, wakamwendea Yoshua katika kambi kule Gilgali, wakamwambia yeye na Waisraeli: “Sisi tumetoka katika inchi ya mbali. Tafazali tunaomba mufanye agano nasi.”
7Lakini Waisraeli wakawajibu hao Wahivi: “Tunaweza namna gani kufanya agano nanyi? Labda ninyi munaishi karibu nasi.” Ang. Kut 23.32; 34.12; Kumb 7.2
8Nao wakamwambia Yoshua: “Sisi tuko watumishi wako.” Naye Yoshua akawauliza: “Ninyi ni nani, na munatoka wapi?”
9Wakamujibu: “Sisi, watumishi wako, tumetoka inchi ya mbali na tumekuja kwa maana tumesikia sifa za jina la Yawe, Mungu wenu. Tulipata habari za utukufu wake na yote aliyoyafanya katika inchi ya Misri.
10Tumesikia yote aliyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ngambo ya muto Yordani, mufalme Sihoni wa Hesiboni na mufalme Ogi wa Basani aliyekaa kule Astaroti. Ang. Hes 21.21-35
11Halafu wazee wetu na wanainchi wote wa inchi yetu, wakatuambia, tutayarishe posho ya safari, tukuje kukutana nanyi na kuwaambia kwamba sisi ni watumishi wenu. Tafazali mufanye agano nasi.
12Angalia mikate yetu ambayo ilikuwa bado moto tulipoibeba wakati tulipoondoka kwetu, lakini sasa imekauka na kuota manyoya.
13Vibuyu hivi tulivijaza maji vikiwa vipya, lakini sasa vimepasukapasuka. Hata nguo na viatu vyetu vimechakaa, maana safari ilikuwa ndefu sana.”
14Hivyo, Waisraeli wakatwaa vyakula vyao, bila kumwuliza Yawe shauri.
15Yoshua akafanya nao mapatano ya amani; akafanya agano kwamba atawaruhusu kuishi. Viongozi wa Waisraeli wakawaapia kutimiza mapatano hayo.
16Siku tatu nyuma ya kufanya agano nao, Waisraeli wakagundua kwamba watu hao walikuwa jirani zao na waliishi kati yao.
17Basi, Waisraeli wakafunga safari, nyuma ya siku ya tatu wakafika katika miji yao. Miji hiyo ilikuwa Gibeoni, Kefira, Beroti na Kiriati-Yearimu.
18Lakini Waisraeli hawakuwaua, maana viongozi wa Waisraeli walikuwa wamewaapia kwa jina la Yawe, Mungu wa Israeli. Hivyo basi, Waisraeli wote wakawanungunikia viongozi wao.
19Lakini viongozi wa Waisraeli wakawaambia watu wao: “Kwa vile tumewaapia kwa jina la Yawe, Mungu wa Israeli, sasa hatuwezi kuwazuru.
20Tutawaacha waishi, kusudi tusipate kuazibiwa kwa sababu ya kiapo tulichofanya.
21Muwaache waishi.” Hivyo Wagibeoni wakakuwa wanatumikia Waisraeli wakiwakatia kuni na kuwachotea maji, kama viongozi wa Waisraeli walivyosema.
22Yoshua akawaita Wagibeoni na kuwauliza: “Kwa nini mulitudanganya kwamba mulitoka inchi ya mbali na wakati ninyi munaishi kati yetu?
23Sasa, ninyi mumelaaniwa nanyi siku zote mutakuwa watumwa wa kukata kuni na kuchota maji kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu.”
24Wakamujibu Yoshua: “Tuliambiwa kwamba kwa hakika Yawe, Mungu wenu, alimwamuru mutumishi wake Musa awaangamize wakaaji wote wa inchi hii na kuwapa ninyi inchi hii ikuwe mali yenu. Kwa hivyo, tuliogopea maisha yetu na ndipo tukafanya jambo hili.
25Sasa sisi tuko katika mikono yako, ututendee kama unavyoona vema na haki.”
26Basi, jambo Yoshua alilowatendea ni kuwaokoa toka katika mikono ya Waisraeli kusudi wasiwaue.
27Lakini kutokea siku hiyo, Yoshua akawafanya hao kuwa wakata - kuni na wachota - maji kwa ajili ya Waisraeli wote na kwa ajili ya mazabahu ya Yawe, popote pale Yawe alipochagua mpaka hivi leo.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.