Matendo ya Mitume 20 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Safari ya Paulo katika inchi ya Makedonia na ya Ugriki

1Fujo ilipokwisha, Paulo akawakusanya wanafunzi na kuwatia moyo. Kisha akaagana nao, akasafiri kwenda Makedonia.

2Alipita katika inchi ile akiwaambia wanafunzi maneno mengi ya kuwatia moyo. Kisha akaenda Ugriki,

3na kukaa kule kwa muda wa miezi mitatu. Alipokuwa tayari kuvuka na chombo kwenda katika inchi ya Suria, akapata habari kwamba Wayuda walimufanyia shauri baya. Kwa hiyo akakusudia kurudia, akipitia Makedonia.

4Na hawa ndio watu waliokwenda pamoja naye: Sopateri mwana wa Piro, wa muji Beroya; Aristarko na Sekundo, wa muji Tesalonika; Gayo, wa muji Derbe; nao Timoteo, Tikiko na Trofimo, wa jimbo la Azia.

5Watu hawa wakatutangulia kwenda Troa, nao wakatungojea kule.

6Lakini nyuma ya sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu, sisi tukaondoka katika muji Filipi kwa njia ya chombo. Na kisha safari ya siku tano tukawakuta Troa, nasi tukakaa kule kwa muda wa siku saba.

Paulo anamufufua Eutiko

7Siku ya kwanza ya juma, tulikuwa tunakusanyika kwa kumega mukate. Paulo akasemezana na watu na kuendelea kuwahubiria mpaka katikati ya usiku, kwa sababu alikusudia kuondoka kesho yake.

8Na kulikuwa taa nyingi katika chumba cha gorofi tulichokusanyika ndani yake.

9Kijana mumoja, aliyeitwa Eutiko, alikuwa akiikaa kwenye dirisha. Na kwa muda ule murefu Paulo alipofundisha, Eutiko akaanza kusinziasinzia na kwa mwisho akawezwa na usingizi na akaanguka chini toka kwenye gorofi ya tatu. Walipomunyanyua alikuwa amekwisha kufa.

10Paulo akashuka chini, akajilaza juu yake na kumukumbatia akasema: “Musilie kwa maana angali muzima!”

11Kisha Paulo akapanda juu tena kwenye gorofi, akamega mukate na kuukula. Akaendelea kuhubiri kwa muda murefu mpaka saa za mapambazuko, na kisha akaondoka.

12Watu wakarudi na yule kijana, akiwa muzima nao wakafarijiwa sana.

Paulo anasafiri kwenda Mileto

13Sisi tulitangulia tukaingia ndani ya chombo na kusafiri kwenda Asosi. Kule tulipaswa kumutwaa Paulo sawa alivyotuagiza, kwa maana alikuwa amekusudia kwenda kule kwa miguu.

14Alipokuwa Asosi, tukamwingiza ndani ya chombo na kwenda pamoja naye mpaka Mitilene.

15Kesho yake tukaondoka kule kwa njia ya chombo na kufika kwenye kisanga cha Kio, na kesho kutwa tukafika kwenye kisanga cha Samosi. Na siku iliyofuata tukafika Mileto.

16Paulo alikuwa amekusudia kupita Efeso kwa chombo pasipo kuezeka kule, kusudi asikawie katika jimbo la Azia. Kwa maana alikuwa na haraka ya kufika Yerusalema mbele ya siku ya Pentekoste kama ikiwezekana.

Paulo anaagana na wazee wa kanisa la Efeso

17Toka Mileto, akatuma ujumbe Efeso kwa kuwaita wazee wa kanisa.

18Nao walipofika, akawaambia: “Ninyi munajua namna nilivyoishi wakati wote nilipokuwa pamoja nanyi, tangia siku ile ya kwanza nilipofika katika jimbo la Azia.

19Nilimutumikia Bwana kwa unyenyekevu wote na kwa machozi na katika majaribu niliyopata kwa ajili ya mashauri mabaya Wayuda waliyonifanyia.

20Munajua kwamba sikuwaficha hata neno moja lenye kuwafalia ninyi, lakini niliwahubiri na kuwafundisha katika mikutano na katika nyumba zenu.

21Nimewaonya Wayuda wa mataifa mengine kwamba wanapaswa kumugeukia Mungu na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo.

22Basi sasa kwa kuwa ninalazimishwa na Roho Mutakatifu, nitakwenda Yerusalema pasipo kujua mambo yatakayonitokea kule.

23Lakini kitu kimoja ninachojua tu, ni kwamba katika kila muji Roho Mutakatifu ananihakikishia kwamba vifungo na mateso vinaningojea.

24Lakini sihesabu maisha yangu kuwa kitu cha bei kali kwangu. Shabaha moja ninayokuwa nayo ni kufikia mwisho wa utumishi wangu na kutimiza kazi ile niliyopewa na Bwana Yesu; maana yake kushuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu.

25“Nilikuwa nikizungukazunguka kati yenu ninyi wote nikitangaza Ufalme wa Mungu. Lakini sasa, ninajua kwamba hakuna hata mumoja atakayeniona tena.

26Ndiyo maana ninahakikisha mbele yenu leo kwamba mimi sitabeba lazima ya damu ya hata mumoja wenu atakayepotea.

27Ni vile kwa sababu niliwatangazia mupango wote wa Mungu pasipo kuwaficha kitu.

28Mujichunge ninyi wenyewe na muchunge vilevile lile kundi lote Roho Mutakatifu alilowapatia kusudi mukuwe wasimamizi wao. Hivi mutaweza kuchunga kanisa la Mungu ambalo alijipatia kwa damu ya Mwana wake.

29Ninajua kwamba nyuma ya kuondoka kwangu, imbwa wakali wa pori wataingia katikati yenu, nao hawatahurumia kundi lile.

30Na hata kati yenu kutatokea watu watakaotoa mafundisho ya kupotosha wengine kusudi wawavute waamini kuwafuata.

31Kwa sababu hii mujiangalie, mukikumbuka kwamba kwa muda wa miaka mitatu, usiku na muchana, sikuchoka kumwonya kila mumoja wenu kwa machozi.

32“Basi sasa ninawaweka chini ya ulinzi wa Mungu na wa neno lake la neema linaloweza kuwajenga katika imani na kuwapa urizi pamoja na watu wake wote watakatifu.

33Mimi sikutamani feza, zahabu, wala nguo ya mutu yeyote.

34Ninyi wenyewe munajua namna nilivyotumika kwa mikono yangu mimi peke kwa kupata vitu vyote ambavyo mimi pamoja na wenzangu tulihitaji.

35Katika mambo hayo yote niliyofanya, nimewaonyesha mufano kwamba tunapaswa kusumbuka vile na kazi kwa kuwasaidia wasiojiweza, tukikumbuka maneno haya Bwana Yesu mwenyewe aliyosema: ‘Ni heri kutoa kuliko kupewa.’ ”

36Paulo alipokwisha kusema maneno haya, akapiga magoti pamoja nao wote na kuomba.

37Na wote walilia sana wakimukumbatia na kumubusu.

38Walihuzunika zaidi kwa sababu aliwaambia kwamba hawatamwona tena. Wakamusindikiza mpaka kwenye chombo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help