Yeremia 44 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Ujumbe wa Mungu kwa Waisraeli katika inchi ya Misri

1Yawe akamutolea Yeremia ujumbe juu ya Wayuda waliokuwa wanakaa katika inchi ya Misri katika miji ya Migidoli, Tapanesi, Nofi na sehemu ya Patro:

2Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Ninyi mumeona hasara yote niliyouletea Yerusalema na miji yote ya Yuda. Miji hii ni mabomoko mpaka leo wala hakuna mutu anayeishi humo.

3Imekuwa hivyo kwa sababu ya uovu walioufanya, wakanikasirikisha kwa kuifukizia ubani na kuitumikia miungu mingine ambayo wao wenyewe hawakuifahamu, wala ninyi, wala babu zenu.

4Hata hivyo, mimi niliwatuma kwenu siku zote watumishi wangu manabii nikisema: Musifanye jambo hili baya ninalolichukia!

5Lakini hakuna aliyenisikiliza wala kunitegea sikio. Ninyi mulikataa kuacha uovu wenu na kuacha kuifukizia miungu mingine ubani.

6Kwa hiyo, kasirani yangu na hasira yangu iliwaka na kumwangika juu ya miji ya Yuda na barabara za Yerusalema, hata kukakuwa jangwa na mabomoko kama inavyokuwa mpaka leo.

7Sasa, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Mbona munajiletea maovu makubwa namna hii, na kujiangamiza ninyi wenyewe, wanaume kama vile wanawake, watoto wadogo na wachanga, hata kusibaki mutu katika inchi ya Yuda?

8Kwa nini munanichochea nikasirike kwa kuabudu sanamu mulizojitengenezea wenyewe na kuifukizia ubani miungu mingine katika inchi ya Misri ambamo mumekuja kuishi? Munataka kuangamizwa na kuwa laana na kuchekelewa mbele ya mataifa yote katika dunia?

9Mumesahau uovu wa babu zenu, uovu wa wafalme wa Yuda, uovu wa wake wao na uovu wenu ninyi wenyewe na wa wake wenu, ambao muliufanya katika inchi ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalema?

10Mpaka hivi leo hamujajinyenyekeza wala kuogopa wala kuzifuata sheria zangu na masharti yangu nilizowawekea ninyi na babu zenu.

11Kwa hiyo, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Basi, nitawageukia na kuwaletea hasara na kuiangamiza Yuda yote.

12Nitawaondoa Wayuda waliobaki ambao wanaokazania kwenda kukaa Misri, na kuwaangamiza wote, wakubwa kama vile wadogo; watakufa kwa upanga au kwa njaa. Watakuwa takataka, kitu cha kutisha, cha laana na kuchekelewa.

13Nitawaazibu wale wanaokaa katika inchi ya Misri kama nilivyouazibu Yerusalema, kwa vita, njaa, na ugonjwa mukali.

14Kwa hiyo hakutakuwa mutu hata mumoja kati ya watu wa Yuda waliobaki na kwenda kukaa katika inchi ya Misri ambaye ataponyoka au kuishi au kurudi katika inchi ya Yuda ambayo wanatamani kurudi na kuishi humo. Hawatarudi, isipokuwa tu wakimbizi wachache.

15Kisha, wanaume wote waliojua kwamba wake wao walikuwa wameifukizia miungu mingine ubani, na wanawake wote waliokuwa hapo, kusanyiko kubwa la watu pamoja na Waisraeli waliokuwa wanakaa Patro katika inchi ya Misri walimujibu Yeremia:

16Juu ya neno ulilotuambia kwa jina la Yawe, hatutakusikiliza.

17Lakini kila kitu tulichoapa kufanya tutafanya: Tutamufukizia ubani malkia wa mbinguni na kumutolea sadaka ya kinywaji kama tulivyokuwa tunafanya sisi wenyewe na babu zetu, wafalme wetu na wakubwa wetu, katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema. Kwa wakati huo tulikuwa na chakula tele, tulistawi na hatukuona hasara yoyote.

18Lakini tangu tulipoacha kumufukizia malkia wa mbinguni ubani na sadaka ya kinywaji, tumekosewa kila kitu, na tumeangamizwa kwa vita na njaa.

19Nao wanawake wakasema: Tulimufukizia malkia wa mbinguni ubani na kumutolea sadaka ya kinywaji. Tulifanya hivyo kwa ruhusa ya waume wetu. Tena tulimutengenezea mikate yenye sura yake na kumutolea sadaka ya kinywaji.

20Halafu Yeremia akawaambia watu wote, wanaume na wanawake, ni kusema watu wote waliomupa jibu hilo:

21Juu ya matambiko ambayo ninyi na babu zenu, wafalme wenu na wakubwa wenu, pamoja na wanainchi wote, mulitoa katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema, munazani Yawe amesahau au hakumbuki?

22Yawe hakuweza kuvumilia tena matendo yenu maovu na mambo ya kuchukiza muliyotenda; ndiyo maana inchi yenu imekuwa ukiwa, jangwa, laana na bila wakaaji, kama inavyokuwa mpaka leo.

23Hasara hizi zimewapata mpaka leo kwa sababu muliitolea miungu mingine sadaka za kuteketezwa na kumukosea Yawe, mukakataa kusikiliza sauti yake au kufuata sheria yake, masharti yake na maagizo yake.

24Yeremia aliwaambia watu wote na wanawake wote: Musikilize neno la Yawe, enyi Wayuda wote munaokuwa katika inchi ya Misri.

25Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Ninyi pamoja na wake wenu mumetimiza kwa vitendo yale muliyosema kwa vinywa vyenu, mukisema kwamba mumekusudia kutimiza viapo vyenu mulivyofanya vya kumutolea malkia wa mbinguni ubani na kumutolea sadaka ya kinywaji. Basi mushike viapo vyenu na kutoa sadaka za vinywaji!

26Lakini musikilize neno la Yawe, enyi watu wote wa Yuda munaokaa katika inchi ya Misri. Yawe anasema hivi: Ninaapa kwa jina langu kubwa kwamba hakuna mutu yeyote wa Yuda katika inchi yote ya Misri atakayelitumia jina langu kwa kuapa nalo akisema: Kama vile Bwana wangu Yawe anavyoishi.

27Mimi ninawachungulia hao si kwa mema lakini kwa mabaya. Watu wote wa Yuda katika inchi ya Misri wataangamizwa kwa upanga na njaa, hakutabaki hata mutu mumoja.

28Ni wachache tu ndio watakaoponyoka katika vita na kurudi kutoka inchi ya Misri na kwenda katika inchi ya Yuda. Halafu Wayuda wote waliobaki kati ya wale waliokwenda kukaa Misri watatambua ni neno la nani lenye nguvu: langu au lao!

29Nitawaazibu hapahapa mupate kujua kwamba maneno ya hasara niliyosema juu yenu yatatimia.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Na hiki kitakuwa kitambulisho chake:

30Nitamutia Hofura mufalme wa Misri katika mikono ya waadui zake, katika mikono ya wale wanaotaka kumwua kama vile nilivyomutia Zedekia mufalme wa Yuda, katika mikono ya waadui zake ni kusema Nebukadneza, mufalme wa Babeli, ambaye alitaka kumwua. Ni Yawe anayesema hivyo.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help