2 Wafalme 9 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Yehu anawekwa kuwa mufalme wa Israeli

1Wakati uleule nabii Elisha alimwita mumoja wa wanafunzi wa nabii, akamwambia: “Ujitayarishe kusafiri, twaa chupa hii ya mafuta, na kwenda Ramoti katika Gileadi.

2Utakapofika kule, umutafute Yehu mwana wa Yosafati, mujukuu wa Nimusi. Umupeleke pembeni ndani ya chumba mbali na wenzake,

3kisha utwae chupa hii ya mafuta, umumiminie juu ya kichwa na kumwambia: ‘Yawe anasema hivi: Ninakupakaa mafuta ukuwe mufalme wa Israeli.’ Kisha fungua mulango na kuondoka upesi utakavyoweza.”

4Basi, nabii huyo kijana akaenda Ramoti-Gileadi.

5Alipofika, aliwakuta wakubwa wa waaskari katika mukutano. Akasema: “Nina ujumbe wako, mukubwa.”

Yehu akamwuliza: “Ni nani kati yetu unayemwambia?”

Akamujibu: “Wewe, mukubwa.”

6Halafu wote wawili wakaingia ndani ya chumba cha ndani na kule nabii akamutia Yehu mafuta juu ya kichwa na kumwambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Ninakupakaa mafuta ukuwe mufalme juu ya watu wangu Israeli.

7Nawe utaipiga jamaa ya bwana wako Ahabu kusudi nimulipize Yezebeli kisasi kwa damu ya watumishi wangu manabii na ya watumishi wangu wote.

8Utafanya hivyo kwa sababu jamaa yote ya Ahabu itaangamia. Tena nitamwua kila mwanaume wa jamaa ya Ahabu akuwe mutumwa au mutu huru.

9Jamaa yake itakuwa kama jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati na ya Basha mwana wa Ahiya.

10Yezebeli hatazikwa na mutu. Maiti yake itakuliwa na imbwa katika inchi ya Yezereheli.’ ” Kisha kusema hayo, nabii akaondoka ndani ya chumba na kukimbia.

11Yehu aliporudi kwa wenzake, mumoja wao alimwuliza: “Kuna shida yoyote? Mwenda-wazimu huyu alitaka nini kwako?”

Yehu akawajibu: “Si munamujua yeye na namna yake ya kusema?”

12Nao wakamwambia: “Hiyo si kweli! Utuambie alilosema!”

Akawaambia: “Aliniambia kwamba ‘Yawe anasema hivi: Ninakupakaa mafuta ukuwe mufalme wa Israeli.’ ”

13Mara moja wakubwa wenzake wakavua nguo zao, wakazilundika pamoja kwenye ngazi kusudi asimame juu yake, wakapiga baragumu na kulalamika kwa sauti: “Yehu ni mufalme!”

Mufalme Yoramu wa Israeli anauawa

14Yehu mwana wa Yosafati, ambaye vilevile alikuwa mujukuu wa Nimusi, alifanya mupango wa kuasi Yoramu. Yoramu na watu wote wa Israeli walikuwa Ramoti-Gileadi kwa kulinda zamu juu ya mufalme Hazaeli wa Aramu.

15Lakini mufalme Yoramu alikuwa amerudi Yezereheli kusudi apate kutunzwa vidonda alivyopata wakati wa kupigana katika vita na mufalme Hazaeli wa Aramu. Yehu aliwaambia wakubwa wenzake: “Ikiwa mutakubaliana nami, mutu yeyote asitoke Ramoti kwenda Yezereheli kwa kupeleka habari hizi.”

16Halafu akapanda ndani ya gari lake na kuelekea Yezereheli. Yoramu alikuwa bado hajapona, na Ahazia mufalme wa Yuda alikuwa amemutembelea.

17Mulinzi aliyekuwa kwenye zamu juu ya munara wa Yezereheli akasema: “Ninaona watu wakikuja na gari!”

Yoramu akajibu: “Chagua askari mupanda-farasi mumoja, umutume kusudi akutane nao, awaulize: ‘Munakuja kwa amani?’ ”

18Basi, mujumbe huyo alipokwenda alikutana na Yehu na kumwambia: “Mufalme anauliza: unakuja kwa amani?”

Yehu akajibu: “Kwa nini unauliza juu ya amani? Wewe geuka ufuatane nami!”

Mulinzi juu ya munara akasema: “Mujumbe amewafikia, lakini harudi.”

19Halafu mujumbe wa pili akatumwa na kumwuliza Yehu: “Mufalme anauliza: unakuja kwa amani?”

Yehu akajibu: “Kwa nini unauliza juu ya amani? Wewe geuka ufuatane nami!”

20Kwa mara ingine tena mulinzi akasema: “Mujumbe amewafikia lakini harudi.” Halafu akaongeza: “Uendeshaji wa gari ni kama wa Yehu mwana wa Nimusi, kwa sababu yeye anaendesha mbiombio.”

21Basi, Yoramu mufalme wa Israeli akaamuru akisema: “Tayarisha gari.”

Nao walitayarisha gari lake. Kisha Yoramu mufalme wa Israeli na Ahazia mufalme wa Yuda waliondoka kila mumoja akipanda ndani ya gari lake, wakaenda kukutana na Yehu. Walimukuta katika uwanja wa Naboti wa Yezereheli.

22Wakati Yoramu alipomwona Yehu, alimwuliza: “Yehu, unakuja kwa amani?”

Yehu akamujibu: “Amani gani, wakati makahaba na wachawi wa Yezebeli ni wengi?”

23Yoramu aligeuza gari lake na kuondoka, naye akimwambia Ahazia: “Ahazia, huu ni uasi!”

24Yehu akatwaa upinde wake na kutupa mushale ambao ulipenya mabega ya Yoramu na kuchoma moyo wake, naye akakufa palepale ndani ya gari lake.

25Yehu akamwambia musaidizi wake Bidikari: “Kamata hiyo maiti yake uitupe katika shamba hilo la Naboti wa Yezereheli. Kwa maana, kumbuka wewe na mimi tulipokuwa tumepanda juu ya farasi wetu nyuma ya baba ya Ahabu, jinsi Yawe alivyosema maneno haya juu yake.

26Yawe alisema: ‘Kwa ile damu ya Naboti na kwa damu ya wana wake niliyoona jana, nitakulipiza kisasi katika shamba hilo.’ Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo, kamata maiti ya Yoramu uitupe katika shamba la Naboti kama vile Yawe alivyosema.”

Mufalme Ahazia wa Yuda anauawa

27Ahazia mufalme wa Yuda alipoona yaliyotukia alikimbia akielekea Nyumba ya Bustani, naye akifuatwa na Yehu. Yehu akawaamuru watu wake: “Mumwue naye vilevile!”

Nao wakamupiga mushale akiwa ndani ya gari kwenye njia ya kupandia Guri karibu na muji wa Ibuleamu. Halafu alikimbilia Megido na kufia kule.

28Wakubwa wake wakaitwaa maiti yake ndani ya gari lake na kuipeleka Yerusalema. Kule akazikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi.

29Ahazia alianza kutawala juu ya Yuda katika mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu.

Malkia Yezebeli anauawa

30Yehu alipofika Yezereheli, Yezebeli alikuwa amekwisha kupata habari ya mambo yaliyotokea. Alijipakaa rangi kwenye macho na kuchanua nywele zake, kisha akaenda kwenye dirisha na kuangalia chini.

31Yehu alipokuwa akiingia kwenye mulango, Yezebeli alisema: “Unakuja kwa amani, ewe Zimuri, wewe unayemwua bwana wako?”

32Yehu akaangalia juu na kusema: “Ni nani anayekuwa upande wangu?”

Wakubwa wawili au watatu wakatokeza vichwa vyao kwa kumwangalia kutoka kwenye dirisha,

33naye Yehu akawaambia: “Mumutupe chini!”

Wakamutupa chini na damu yake ikasambaa juu ya ukuta na kwenye farasi. Yehu akapitisha farasi na gari lake juu ya maiti yake

34na kuingia katika nyumba ya kifalme, na huko akakula na kunywa. Halafu akaamuru: “Muzike mwanamuke yule aliyelaaniwa kwa sababu ni binti ya mufalme.”

35Halafu walikwenda kumuzika lakini hawakuona chochote isipokuwa mufupa wa kichwa na mifupa ya mikono na miguu.

36Kisha walirudi na kumupasha Yehu habari hii, naye akasema: “Hivi ndivyo Yawe alivyotabiri kwa njia ya mutumishi wake Elia wa muji wa Tisibe akisema: ‘Imbwa wataukula mwili wa Yezebeli katika shamba la Yezereheli.

37Maiti ya Yezebeli itakuwa kama mboleo ndani ya shamba katika inchi ya Yezereheli, hata hakuna atakayeweza kumutambua.’ ”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help