Zaburi 109 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Malalamiko ya mutu anayekuwa katika taabu

1Kwa mukubwa wa waimbaji. Wimbo wa Daudi.

Usinyamaze, ee Mungu, ninayekusifu!

2Watu waovu na wadanganyifu wananishambulia,

wanasema uongo juu yangu.

3Wanasema maovu juu yangu,

na kunishambulia bila sababu.

4Ingawa niliwapenda, walinishitaki.

Hata hivyo, niliwaombea.

5Wananilipa mabaya kwa mazuri yangu,

na chuki kwa mapendo yangu.

6Umuweke mwamuzi mubaya juu ya adui yangu;

na anayemushitaki amupeleke mbele ya baraza.

7Anapohukumiwa apatikane na kosa;

malalamiko yake yahesabiwe kuwa kosa lingine.

8Siku za maisha yake zikuwe chache,

mutu mwingine akamate kazi yake!

9Watoto wake wakuwe wayatima,

na muke wake akuwe mujane!

10Watoto wake watangetange na kuombaomba;

wafukuzwe katika mabaki ya nyumba zao!

11Anayemudai kitu amunyanganye mali yake yote,

na wageni wakule mapato ya jasho lake!

12Kusikuwe mutu wa kumutendea mema,

au kuwatunza watoto wake wayatima!

13Wazao wake wote wakufe;

jina lake lisahauliwe katika kizazi kinachokuja!

14Yawe akumbuke uovu wa babu zake,

zambi za mama yake zisifutwe hata kidogo!

15Yawe akumbuke zambi zao siku zote;

lakini wao wenyewe wasahauliwe katika dunia.

16Mwovu huyo hajali kabisa kutenda mema,

lakini anatesa

wamasikini, wakosefu, na wenye moyo wenye kuvunjika

mpaka kufa.

17Yeye alipenda kulaani watu;

laana imupate yeye mwenyewe.

Hakuwatakia wengine baraka;

basi, asipate baraka yeye mwenyewe.

18Kwake kulaani ni kama kuvaa nguo;

basi, laana hizo zimulowanishe kama maji,

zimwingie katika mifupa yake kama mafuta.

19Laana zimufunike kama nguo,

zimuzunguke siku zote kama mukaba.

20Yawe awalipe hayo hao watu wanaonishitaki,

hao wanaosema mabaya juu yangu.

21Lakini, ee Yawe, Bwana wangu,

unitendee kwa heshima ya jina lako.

Wema wako ni muzuri.

Basi, uniokoe!

22Mimi ni masikini na mukosefu;

ninaumizwa mpaka ndani ya moyo wangu.

23Ninatoweka kama kivuli cha magaribi;

nimepeperushwa kama nzige.

24Magoti yangu yanaregea kwa ajili ya kufunga kula chakula;

nimebaki mifupa na ngozi.

25Watu wananichekelea;

wanaponiona wanatikisa vichwa vyao kwa kunizarau.

26Unisaidie, ee Yawe, Mungu wangu;

uniokoe kufuatana na wema wako.

27Uwaonyeshe watu kuwa wewe ndiwe uliyetenda hayo.

Wewe, ee Yawe, ndiwe uliyefanya hivyo.

28Uwaache walaani, lakini wewe unibariki;

wanaonishambulia wafezeheke, nami mutumishi wako nifurahi.

29Waadui zangu wazungukwe na mazarau;

wajifunike haya yao kama vile nguo.

30Nitamushukuru sana Yawe kwa sauti;

nitamusifu kati ya kundi kubwa la watu,

31kwa maana yeye anamutetea mukosefu,

kwa kumwokoa kutoka kwa wale wanaomuhukumu kufa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help