1Solomono alipenda sana wanawake wa kigeni: binti ya mufalme wa Misri, wanawake wa Wamoabu, Waamoni, Waedomu, Wasidoni, na Wahiti,
2ni kusema wanawake wa mataifa ambayo Yawe alikuwa amewakataza Waisraeli akisema: “Musioe kwao wala wao wasioe kwenu kwa sababu wanawake hao watapotosha mioyo yenu kusudi muitumikie miungu yao.” Solomono aliwapenda sana wanawake hao.
3Solomono akakuwa na wanawake mia saba, wote wabinti wa kifalme, na wahabara mia tatu. Hao wanawake wakamupotosha.
4Maana, alipokuwa muzee, wake zake walimupotosha hata akaitumikia miungu mingine, wala hakukuwa mwaminifu kabisa kwa Yawe, Mungu wake, kama baba yake Daudi alivyokuwa mwaminifu.
5Solomono alimutumikia Astaroti aliyekuwa mungu wa Wasidoni, na alimufuata Milkomu, mungu wa chukizo wa Waamoni.
6Hivyo, Solomono alitenda maovu mbele ya Yawe, wala hakufuata kwa ukamilifu mapenzi ya Yawe kama baba yake Daudi alivyokuwa amefanya.
7Juu ya mulima unaokuwa upande wa mashariki wa Yerusalema, Solomono alijenga pahali pa kumutambikia Kemosi, mungu wa chukizo wa Wamoabu, na nafasi ya kumutambikia Milkomu, mungu wa chukizo wa Waamoni.
8Vilevile, aliwajengea wake zake wote wa kigeni nafasi ya kufukizia ubani na kuitambikia miungu yao.
9Basi, Yawe alimukasirikia Solomono, kwa sababu alikuwa amemwacha Yawe, Mungu wa Israeli, ingawa yeye alikuwa amemutokea mara mbili
10na kumwamuru asiiabudu miungu ya kigeni. Solomono hakutii amri ya Yawe.
11Kwa hiyo Yawe akamwambia Solomono: “Kwa kuwa umeamua kufanya hivyo, ukavunja agano langu nawe, na kuasi masharti yangu niliyokupa, hakika nitakunyanganya huo utawala na kumupa mutumishi wako.
12Hata hivyo, kwa ajili ya baba yako Daudi, sitafanya hivyo wakati ungali unaishi, lakini nitauondoa utawala huo katika mikono ya mwana wako.
13Hata yeye sitamunyanganya urizi wote, lakini nitamwachia mwana wako kabila moja, kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi, na kwa ajili ya Yerusalema ambao nimeuchagua kuwa wangu.”
14Halafu Yawe akamufanya Hadadi, aliyekuwa wa ukoo wa mufalme wa Edomu, kuwa adui ya Solomono.
15Wakati Daudi alipowaangamiza Waedomu, Yoabu, jemadari wa waaskari wa Daudi, alikwenda kule kuwazika waliouawa. Yoabu aliwaua wanaume wote wa Edomu.
16Yoabu alikaa kule na waaskari wake kwa muda wa miezi sita, apate kuwaangamiza kabisa wanaume wote wa Edomu.
17Lakini Hadadi ambaye wakati ule alikuwa kijana alitorokea Misri pamoja na Waedomu wamoja, watumishi wa baba yake.
18Hadadi na wenzake walisafiri kutoka Midiani, wakawakamata watu wengine kule Parani, wakaenda nao mpaka Misri, kwa mufalme wa Misri. Yeye akamupatia Hadadi nyumba, shamba, na chakula.
19Hadadi alipata kukubaliwa kabisa mbele ya mufalme wa Misri. Kwa hiyo mufalme wa Misri akamuruhusu shemeki yake, mudogo yake na malkia Tapanesi, aolewe na Hadadi.
20Huyo dada ya Tapanesi akamuzalia Hadadi mwana aliyeitwa Genubati. Genubati alilelewa na Tapanesi katika nyumba ya mufalme wa Misri, pamoja na wana wa mufalme.
21Lakini Hadadi aliposikia kule Misri kwamba Daudi na Yoabu jemadari wa waaskari walikuwa wamekufa, alimwambia mufalme wa Misri: “Uniruhusu niondoke nirudi katika inchi yangu.”
22Lakini mufalme wa Misri akamwuliza: “Nimekunyima nini hata uamue sasa kurudi katika inchi yako?”
Naye Hadadi akasema: “Uniache tu niende.”
23Vilevile, Mungu alimufanya Resoni mwana wa Eliada, akuwe adui ya Solomono. Resoni alikuwa amemutoroka bwana wake, mufalme Hadadezeri wa Zoba.
24Nyuma ya Daudi kufanya mauaji kule Zoba, Resoni alikusanya watu, naye mwenyewe akakuwa kiongozi wao. Basi, wakaenda Damasiki, wakakaa kule na kumufanya Resoni mufalme wa Damasiki.
25Resoni alikuwa adui wa Waisraeli siku zote za utawala wa Solomono, akamusumbua sana Solomono kama naye Hadadi alivyomusumbua. Basi, Resoni aliizarau inchi ya Israeli, naye alitawala inchi ya Aramu.
26Yeroboamu mwana wa Nebati Mwefuraimu wa muji wa Zereda, mutumishi wa Solomono, ambaye mama yake mujane aliitwa Zerua, naye alimwasi mufalme.
27Kisa cha uasi huo ni hiki: Solomono alijenga uwanja wa Milo na kuimarisha kuta za muji wa baba yake Daudi.
28Yeroboamu alionekana kuwa kijana hodari na shujaa. Wakati Solomono alipoona kwamba huyo kijana alikuwa mwenye bidii, akamuweka akuwe musimamizi wa kazi za kulazimishwa zilizofanywa na watu wa ukoo wa Yosefu.
29Siku moja, Yeroboamu alipokuwa akisafiri kutoka Yerusalema, nabii Ahiya wa Shilo alikutana naye katika njia. Ahiya alikuwa akivaa nguo mupya. Wote wawili walikuwa peke yao katikati ya mashamba.
30Mara moja, Ahiya akavua nguo yake mupya, akaipasua kwa vipande kumi na viwili,
31halafu akamwambia Yeroboamu: “Ujitwalie vipande kumi maana Yawe, Mungu wa Israeli, anasema: ‘Sasa hivi nitaurarua ufalme na kuuondoa katika mikono ya Solomono, nami nitakupa wewe makabila kumi.
32Lakini yeye, nitamwachia kabila moja kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi, na kwa ajili ya Yerusalema ambao nimeuchagua kuwa wangu katika makabila yote ya Israeli.
33Nitafanya hivyo kwa sababu Solomono ameniacha, akaabudu miungu ya kigeni: Astaroti mungu wa Wasidoni, Kemosi mungu wa Wamoabu, na Milkomu mungu wa Waamoni. Solomono ameniasi, ametenda maovu mbele yangu. Hakutii masharti yangu na maagizo yangu kama Daudi baba yake alivyofanya.
34Hata hivyo, sitamunyanganya urizi wote, wala sitamwondolea mamlaka wakati angali anaishi, kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi ambaye nilimuchagua, na ambaye alifuata amri zangu na masharti yangu.
35Lakini, nitamunyanganya mwana wake ufalme ule, nami nitakupatia wewe Yeroboamu makabila kumi.
36Huyo mwana wa Solomono nitamwachia kabila moja, kusudi wakati wote mutu mumoja wa uzao wa mutumishi wangu Daudi akuwe anatawala Yerusalema, akuwe taa inayoangaza siku zote mbele yangu katika muji ambao nimeuchagua ukuwe pahali pa kuniabudia.
37Basi, wewe Yeroboamu, nitakufanya kuwa mufalme wa Israeli, nawe utatawala kama unavyopenda.
38Na kama utashika yote nitakayokuamuru, kama utaishi kulingana na mapenzi yangu, kama utatenda mema mbele yangu kwa kushika masharti yangu na amri zangu, kama vile mutumishi wangu Daudi alivyofanya, mimi nitakuwa pamoja nawe siku zote. Na nitakupatia inchi ya Israeli na kuufanya utawala wako ukuwe imara kama nilivyomufanyia Daudi.
39Kutokana na hayo, nitawaazibu wazao wa Daudi, lakini si siku zote.’ ”
40Kwa sababu hiyo, Solomono alijaribu kumwua Yeroboamu. Lakini Yeroboamu akakimbilia Misri kwa Sisaki mufalme wa Misri, akakaa kule mpaka Solomono alipokufa.
Kifo cha Solomono(2 Sik 9.29-31)41Mambo mengine ya Solomono, yote aliyofanya na hekima yake yameandikwa katika Kitabu cha Matendo ya Solomono.
42Kwa muda wa miaka makumi ine, Solomono aliitawala inchi yote ya Israeli, makao yake yakiwa Yerusalema.
43Kisha, Solomono alikufa, akazikwa katika muji wa baba yake Daudi. Rehoboamu mwana wa Solomono akatawala kwa pahali pake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.