1 Samweli 11 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Saulo anawashinda Waamoni

1Mufalme Nahasi wa Waamoni, alikwenda na kuushambulia muji wa Yabesi-Gileadi. Wakaaji wa muji wa Yabesi-Gileadi wakamwambia Nahasi: “Fanya mapatano nasi, nasi tutakutumikia.”

2Lakini akawaambia: “Nitafanya mapatano nanyi kwa shurti hii moja: nitamwongoa kila mumoja wenu jicho lake la kuume. Hivyo nitawapatisha Waisraeli wote haya.”

3Wazee wa Yabesi wakamwambia: “Utupatie muda wa siku saba kusudi tuwatume wajumbe katika inchi yote ya Waisraeli. Kama hakuna mutu yeyote wa kutuokoa, tutajitoa sisi wenyewe kwako.”

4Wale wajumbe walipofika katika muji wa Gibea, ambako Saulo alikoishi, wakaeleza habari hizo na watu wote wakaanza kulia kwa sauti.

5Sasa, Saulo alikuwa anatoka kwenye shamba akiwa na ngombe dume wake, akauliza: “Watu wana nini? Kwa nini wanalia?” Wakamwambia habari wajumbe waliyoleta kutoka Yabesi.

6Mara moja, Saulo aliposikia maneno hayo, roho wa Mungu akamufikia kwa nguvu, naye akawaka hasira kali.

7Akatwaa ngombe dume wawili, akawakatakata vipande, akatuma wajumbe wapitishe vipande hivyo katika mipaka yote ya Waisraeli wakisema: “Mutu yeyote ambaye hatamufuata Saulo na Samweli katika vita, ngombe dume wake watafanyiwa hivyo.” Waisraeli waliingiwa na hofu juu ya kile ambacho Yawe angeweza kufanya. Kwa hiyo, wote walitoka pamoja.

8Saulo alipowapanga Waisraeli kule Bezeki akakuwa na watu elfu mia tatu kutoka inchi ya Israeli na elfu makumi tatu kutoka inchi ya Yuda.

9Wakawaambia wale wajumbe waliorudi kutoka Yabesi: “Muwaambie wakaaji wa Yabesi-Gileadi hivi: kesho, wakati jua linapokuwa kali, mutakuwa mumekombolewa.” Watu wa Yabesi walipopata habari hizo walifurahi sana.

10Hivyo, wakamuchekelea Nahasi wakimwambia: “Kesho tutajitoa wenyewe kwako, nawe utatutendea sawa unavyotaka.”

11Kesho yake, Saulo aliwagawanya watu katika vikundi vitatu. Wakati wa zamu ya asubui, wakaingia kwenye kambi ya adui, na kuwashambulia Waamoni. Kufikia saa sita za muchana waadui wengi walikuwa wameangamizwa. Wale waliobaki walitawanyika ovyo, hata hakukuwa kikundi chochote kati yao hata cha watu wawili tu pamoja.

12Halafu Waisraeli wakamwambia Samweli: “Wako wapi wale watu waliosema Saulo asikuwe mufalme juu yetu? Mutuletee watu hao, nasi tutawaua.”

13Lakini Saulo akawaambia: “Hakuna mutu yeyote atakayeuawa leo, kwa sababu katika siku hii, Yawe ameikomboa Israeli.”

14Samweli akawaambia: “Twende wote Gilgali na kwa mara ingine tutamutangaza Saulo kuwa mufalme.”

15Watu wote wakaenda Gilgali, na walipofika kule, wakamusimika Saulo kuwa mufalme mbele ya Yawe. Wakamutolea Yawe sadaka za amani pale. Na Saulo pamoja na watu wote wa Israeli wakafurahi sana.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help