Yeremia 14 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Ukosefu mukali wa maji

1Yawe akanitolea mimi Yeremia ujumbe juu ya ule ukosefu wa maji, akisema:

2Watu wa Yuda wanaomboleza,

miji yake inateketea.

Watu wake wanaomboleza wakiikaa katika udongo

na kilio cha Yerusalema kinapanda mpaka juu.

3Wakubwa wake wanawatuma watumishi wao maji;

watumishi wanakwenda kwenye visima,

lakini hawapati maji;

wanarudi na vyombo vitupu.

Kwa ajili ya haya na mahangaiko wanaangalia chini.

4Walimaji wanahuzunika

kwa kuona jinsi udongo unavyokauka

kwa ajili ya ukosefu wa mvua.

5Hata kulungu anazaa katika pori na kuacha kitoto chake,

kwa sababu hakuna majani.

6Punda wa pori wanasimama kwenye vichwa vya vilima vyenye kukauka,

wakivuta hewa kama mbweha;

macho yao yanafifia kwa ukosefu wa majani.

7Nao watu wanasema:

Ingawa zambi zetu zinatoa ushuhuda juu yetu,

utusaidie ee Yawe kwa ajili ya heshima ya jina lako.

Maasi yetu ni mengi,

tumetenda zambi mbele yako.

8Wewe unayekuwa tumaini la Waisraeli,

wewe unayetuokoa wakati wa taabu,

namna gani unajifanya kama mugeni katika inchi,

kama musafiri anayelala kwa usiku mumoja tu?

9Namna gani unakuwa kama mutu aliyechanganyikiwa,

kama shujaa asiyeweza kusaidia mutu?

Ingawa hivyo wewe ee Yawe unakaa katikati yetu;

nasi tunajulikana kwa jina lako, usituache.

10Yawe anasema hivi juu ya watu hawa:

Kweli wamependa sana kutangatanga,

wala hawakujizuia;

kwa hiyo mimi Yawe sipendezwi nao.

Sasa nitayakumbuka makosa yao,

na kuwaazibu kwa ajili ya zambi zao.

11Yawe akaniambia hivi: Usiwaombee watu hawa uheri.

12Hata wakifunga, sitayasikiliza maombi yao, na hata wakinitolea sadaka za kuteketeza kwa moto na sadaka zingine, mimi sitazikubali. Lakini nitawaangamiza kwa vita, njaa na ugonjwa mukali.

13Kisha mimi nikasema: Ee Bwana wangu Yawe! Manabii wanawaambia watu hawa kwamba hakutakuwa vita wala njaa, kwa sababu umeahidi kwamba kutakuwa tu amani katika inchi hii.

14Naye Yawe akaniambia: Hao manabii wanatoa unabii wa uongo kwa jina langu. Mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao. Wanawatabiria maono ya uongo, maaguzi yao hayana maana yoyote, wao wanajitungia uongo wenyewe.

15Kwa hiyo, Yawe anasema hivi juu ya hao manabii: Wanatabiri kwa jina langu, ingawa mimi sikuwatuma. Wanasema kwamba hakutakuwa vita wala njaa katika inchi hii: Manabii hao wataangamia kwa vita na kwa njaa.

16Na hao ambao waliowatabiria mambo hayo, maiti zao zitatupwa katika barabara za Yerusalema wakiuawa kwa njaa na vita, wala hakutakuwa mutu wa kuwazika wao wenyewe, wake zao, wabinti zao na wana wao. Mimi nitawabebesha lazima ya uovu wao wenyewe.

17Hivi ndivyo utakavyowaambia:

Heri macho yangetoa machozi usiku na muchana,

wala yasikome kutiririka,

maana, watu wangu wamepata hasara kubwa,

wameumizwa kidonda kikubwa sana.

18Nikienda inje katika mbuga,

ninaiona maiti ya waliouawa kwa vita;

nikiingia ndani katika muji,

ninaona tu maiti ya waliokufa kwa njaa!

Manabii na makuhani wanashugulikia mambo yao katika inchi,

lakini hawajui wanalofanya.

19Ee Yawe, umekataa Yuda kabisa?

Moyo wako umechukizwa na Sayuni?

Kwa nini umetupiga vibaya kama hivi,

hata hatuwezi kupona tena?

Tulitazamia kupata amani,

lakini hakuna kitu kizuri.

Tulitazamia kupona,

lakini tumepatwa na vitisho.

20Tunakubali uovu wetu, ee Yawe,

tunakubali uovu wa babu zetu,

maana, tumekukosea wewe.

21Usitutupe, kwa ajili ya heshima ya jina lako;

usikizarau kiti chako cha kifalme chenye utukufu.

Ukumbuke agano ulilofanya nasi, wala usilivunje.

22Katikati ya miungu ya uongo ya mataifa

nani anayeweza kunyesha mvua?

Au, ni mbingu ndiyo inaweza kutoa manyunyu?

Si ni wewe ee Yawe, Mungu wetu?

Tunakuwekea wewe tumaini letu,

maana ni wewe unayefanya haya yote.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help