Hesabu 32 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Makabila ya upande wa mashariki wa Yordani(Kumb 3.12-22)

1Makabila ya Rubeni na Gadi yalikuwa na mifugo mingi sana. Basi, walipoona kwamba eneo la Yazeri na Gileadi lilifaa kwa mifugo,

2wakawaendea Musa, kuhani Eleazari na viongozi wa Waisraeli, wakawaambia:

3Miji ya Ataroti, Diboni, Yazeri, Nimura, Hesiboni, Eleale, Sebamu, Nebo na Beoni,

4inchi ambayo Yawe alishinda kwa ajili ya Waisraeli, ni inchi nzuri kwa mifugo, nasi tuko na mifugo mingi sana.

5Basi, kama tumepata kukubaliwa mbele yako, wewe Musa, tunakuomba utupatie inchi hii ikuwe mali yetu; usituvukishe ngambo ya muto Yordani.

6Musa akawajibu watu wa makabila ya Gadi na Rubeni: Munataka kubaki hapa wakati wandugu zenu Waisraeli wanakwenda kwa vita?

7Mbona munawavunja moyo Waisraeli wasiende katika inchi ambayo Yawe amewapa?

8Hivi ndivyo walivyofanya babu zenu nilipowatuma kutoka Kadesi-Barnea kwa kupeleleza inchi. Ang. Hes 13.17-33

9Wao walikwenda mpaka bonde la Eskoli, wakaiona inchi, lakini waliporudi, wakavunja Waisraeli moyo kusudi wasiingie katika inchi Yawe aliyowapa.

10Yawe akawaka hasira siku hiyo, akaapa akisema: Ang. Hes 14.26-35

11Hakika hakuna mutu yeyote kati ya watu waliotoka Misri mwenye umri wa miaka makumi mbili na zaidi atakayeona inchi niliyoapa kuwapa Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwa sababu hawakunitii kwa ukamilifu.

12Wote hawataiona, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune wa ukoo wa Kenizi na Yoshua mwana wa Nuni, maana wao wamenitii kwa ukamilifu.

13Yawe akawaka hasira juu ya Waisraeli, akawafanya watangetange katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine; kizazi kizima kilichokuwa kimefanya maovu mbele yake kikakufa.

14Na sasa, enyi kizazi cha wenye zambi, mumesimama kwa pahali pa wazee wenu, kuongeza tena hasira kali ya Yawe juu ya Waisraeli.

15Kama ninyi mukikataa kumufuata, yeye atawaachilia tena katika jangwa, nanyi mutasababisha watu hawa wote waangamie.

16Basi, wakamwendea Musa, wakamwambia: Kwanza uturuhusu tuwajengee kondoo wetu mazizi, na watoto wetu miji hapa.

17Lakini sisi wenyewe tutatwaa silaha zetu tayari kwenda kwa vita pamoja na wandugu zetu Waisraeli, na tutakuwa kwa mustari wa mbele katika vita mpaka tuwafikishe pahali watakapokaa. Wakati huo watoto wetu watakaa kwenye miji yenye kuta, kwa kujilinda na wenyeji wa inchi hii.

18Hatutarudi kwenye nyumba mpaka pale Waisraeli wengine wote watakaporizi maeneo yao waliyogawanyiwa.

19Hatutarizi mali yoyote kati yao ngambo ya muto Yordani, kwa sababu sisi tumepata maeneo yetu ngambo hii, upande wa mashariki wa muto Yordani.

20Musa akawaambia: Kama kweli mutafanya kama vile mulivyosema, basi hapahapa mbele ya Yawe, mutwae silaha zenu kwenda kwa vita.

21Kila mupiganaji wenu atavuka muto Yordani na mukiwa chini ya uongozi wa Yawe, mutawashambulia waadui zetu mpaka Yawe awashinde,

22na kurizi inchi. Mukisha kufanya hayo, mutarudi, maana mutakuwa bila kosa mbele ya Yawe na wandugu zenu Waisraeli. Kisha Yawe atakubali inchi hii ya upande wa mashariki wa Yordani kuwa mali yenu.

23Lakini ninawaonya kwamba musipotimiza ahadi yenu, mutakuwa mumemutendea Yawe zambi; mujue kwa hakika kwamba mutaazibiwa.

24Muwajengee watoto wenu miji na kondoo wenu mazizi; lakini mufanye kama vile mulivyoahidi.

25Kisha, watu wa Gadi na wa Rubeni wakamwambia Musa: Sisi watumishi wako tutafanya kama vile ulivyotuamuru.

26Wake zetu, watoto wetu na kondoo na ngombe, watabaki hapa katika miji ya Gileadi.

27Lakini sisi watumishi wako tuko tayari kwenda kwa vita chini ya uongozi wa Yawe. Tutavuka muto Yordani na kupigana, kama vile ulivyosema.

28Basi, Musa akatoa amri hizi kwa kuhani Eleazari, kwa Yoshua mwana wa Nuni, na kwa viongozi wa jamaa za makabila ya Waisraeli:

29Ikiwa watu wa Gadi na wa Rubeni watavuka muto Yordani pamoja nanyi wakiwa na silaha zao chini ya uongozi wa Yawe, mukishinda na kuitwaa inchi hiyo, basi mutawapa inchi ya Gileadi ikuwe mali yao.

30Lakini kama hawatavuka muto Yordani pamoja nanyi na silaha zao, basi watarizi sehemu ya inchi ya Kanana pamoja nanyi.

31Watu wa Gadi na wa Rubeni wakajibu: Bwana, sisi tutafanya kama vile Yawe alivyotuambia sisi watumishi wako.

32Chini ya uongozi wa Yawe, tutavuka na silaha zetu mpaka katika inchi ya Kanana, lakini inchi tuliyopewa hapa upande wa mashariki wa Yordani itakuwa mali yetu.

33Basi, Musa akawapa watu wa makabila ya Gadi na Rubeni na nusu ya kabila la Manase mwana wa Yosefu, inchi yote ya mufalme Sihoni wa Waamori na inchi ya mufalme Ogi wa Basani pamoja na miji na maeneo yaliyokuwa kandokando ya miji hiyo.

34Kabila la Rubeni likaijenga miji ya Diboni, Ataroti, Aroeri,

35Aturoti-Sofani, Yazeri, Yogibeha,

36Beti-Nimira na Beti-Harani, miji yenye kuta na mazizi ya kondoo.

37Kabila la Gadi likajenga miji ya Hesiboni, Eleale, Kiriataimu,

38Nebo na Bali-Meoni (majina ya hiyo miji yalibadilishwa), na Sibuma. Miji waliyoijenga wakaipa majina mengine.

39Wazao wa Makiri mwana wa Manase wakashambulia inchi ya Gileadi, wakaiteka na kuwafukuza Waamori waliokuwa wanakaa mule.

40Kwa hiyo, Musa akawapa watu wa ukoo wa Makiri mwana wa Manase, inchi ya Gileadi, nao wakakaa mule.

41Yairi, wa kabila la Manase, akashambulia vijiji vya Gileadi na kuviteka, akavipa jina “Vijiji vya Yairi”.

42Naye Noba akashambulia na kuteka Kenati na vijiji vyake, akauita Noba, jina lake mwenyewe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help