1Nyuma ya hayo, Daudi aliwashinda Wafilistini. Akawanyenyekeza na kunyanganya utawala wa Wafilistini.
2Kisha aliwashinda Wamoabu. Aliwapanga katika mistari mateka hao, na kuwalalisha chini. Aliamuru wale waliokuwa katika mistari miwili wauawe na wale wa mustari wa tatu waachwe wazima. Hivyo, Wamoabu wakakuwa watumishi wa Daudi na wakakuwa wanamulipa kodi.
3Daudi vilevile alimushinda Hadadezeri mwana wa Rehobu, mufalme wa Zoba. Daudi alipata ushindi huu wakati Hadadezeri alipokuwa katika njia kwenda kulirudisha eneo la muto Furati kuwa chini ya utawala wake.
4Daudi aliteka waaskari wapanda-farasi elfu moja na mia saba, na waaskari wa miguu elfu makumi mbili. Kisha Daudi alikata mishipa ya miguu ya nyuma ya farasi wote wa magari ya vita, lakini aliacha farasi wa kutoshelea kwa magari mia moja.
5Nao Waaramu wa Damasiki walipokwenda kumusaidia Hadadezeri, mufalme wa Zoba, Daudi aliwashambulia na kuwaua watu elfu makumi mbili na mbili.
6Halafu Daudi aliweka kambi za waaskari katika muji wa Waaramu wa Damasiki. Basi, Waaramu wakakuwa watumishi wake na wakakuwa wanamulipa kodi. Yawe alimupa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
7Daudi alitwaa ngao za zahabu waaskari wa Hadadezeri walizobeba na kuzipeleka Yerusalema.
8Vilevile alitwaa shaba nyingi sana kutoka miji ya Beta na Berotayi, iliyokuwa miji ya Hadadezeri.
9Wakati Toi, mufalme wa Hamati, aliposikia kwamba Daudi amewashinda waaskari wote wa Hadadezeri,
10alimutuma mwana wake Yoramu kwa mufalme Daudi kwa kumupelekea salamu na shukrani kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumushinda. Maana Hadadezeri alipigana na Toi mara nyingi. Yoramu alimupelekea Daudi zawadi za vyombo vya feza, zahabu na shaba.
11Kwa ajili ya Yawe, Daudi akatakasa zawadi zile, pamoja na feza na zahabu ambazo alikuwa ameziteka kwa mataifa yote aliyoyashinda,
12ni kusema Aramu, Moabu, Amoni, Filistini, Amaleki. Aliteka vilevile vitu vya mufalme Hadadezeri mwana wa Rehobu mufalme wa Zoba.
13Daudi alijiongezea sifa yake. Alipokuwa anarudi kisha kumushinda Hadadezeri, aliwaua Waedomu elfu kumi na nane, katika Bonde la Chumvi.
14Akaweka kambi za waaskari katika inchi ya Edomu yote. Nao Waedomu wote wa kule wakakuwa watumishi wake. Yawe alimupa Daudi ushindi kokote alikokwenda.
15Kwa hiyo, Daudi akatawala juu ya Israeli yote, naye akawahukumu watu wake wote kufuatana na haki na sheria.
16Yoabu mwana wa Zeruya alikuwa jemadari wa makundi yake ya waaskari. Yosafati mwana wa Ahiludi alikuwa mwandishi wa habari za kifalme.
17Zadoki mwana wa Ahitubu na Ahimeleki mwana wa Abiatari walikuwa makuhani. Seraya alikuwa katibu.
18Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa kiongozi wa Wakereti na Wapeleti. Wana wa Daudi wakakuwa makuhani.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.