Yakobo 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Upendo usiokuwa na upendeleo

1Wandugu zangu, kufuatana na vile munavyomwamini Bwana wetu Yesu Kristo mwenye utukufu, musikuwe vilevile na upendeleo na watu.

2Kwa mufano: tajiri mumoja anayevaa pete ya zahabu na nguo nzuri anaingia katika nyumba yenu ya kuabudia. Na kisha kunaingia vilevile masikini anayevaa nguo zinazopasukapasuka.

3Halafu munaonyesha heshima kwa yule anayevaa vizuri na kumwambia: “Ikaa hapa kwenye nafasi nzuri.” Lakini munamwambia yule masikini: “We! Simama pale, au uikae hapa chini kwenye nafasi ya kuwekea miguu yangu.”

4Jambo hilo halionyeshi kwamba munafanya ubaguzi, na kwamba kwa kuamua vile munaongozwa na mawazo mabaya?

5Wandugu zangu wapenzi, musikilize: Mungu amewachagua wamasikini wa dunia hii kusudi wakuwe watajiri katika imani, nao wapokee Ufalme ule aliowaahidi wale wanaomupenda.

6Lakini ninyi munawazarau wamasikini! Watajiri si ndio wale wanaowagandamiza ninyi na kuwashitaki kwenye tribinali?

7Vilevile si wao ndio wanaotukana jina lile nzuri mulilopewa?

8Munafanya vizuri kama mukitimiza sheria hii ya kifalme inayopatikana katika Maandiko Matakatifu: “Umupende mwenzako kama unavyojipenda wewe mwenyewe.”

9Lakini kama mukifanya upendeleo, munafanya zambi, nanyi munahukumiwa na Sheria kwa sababu mumeivunja.

10Kwa maana mutu akivunja agizo moja tu la Sheria, yeye anavunja Sheria yote.

11Kwa maana yule aliyesema “Usizini”, ndiye aliyesema vilevile “Usiue”. Basi ikiwa wewe huzini lakini unaua, wewe unavunja Sheria.

12Basi museme na kutenda kama watu watakaohukumiwa kufuatana na sheria inayotuweka kuwa huru.

13Kwa sababu Mungu hatahurumia mutu yule asiyehurumia wengine. Lakini huruma ya Mungu itaishinda hukumu.

Imani na matendo

14Wandugu zangu, ni faida gani kama mutu akisema kwamba yuko na imani lakini haionyeshi kwa njia ya matendo mazuri? Ile imani itaweza kumwokoa?

15Kwa mufano: kaka au dada fulani akikosewa nguo au chakula,

16itakuwa na faida gani, kama mumoja wenu anamwambia: “Mwende vizuri, mukaote moto na kushiba,” lakini hamusaidii na kitu chochote?

17Ni hivi vilevile, imani peke yake pasipo matendo imekufa kabisa.

18Lakini mutu anaweza kusema: “Wewe uko na imani, na mimi niko na matendo.” Mimi nitajibu: “Unionyeshe imani yako pasipo matendo, na mimi nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu.”

19Si wewe unaamini kwamba kuna Mungu mumoja? Ni vizuri! Hata pepo wanaamini vile, nao wanatetemeka kwa woga.

20Wewe mujinga! Unataka kuhakikishwa kwamba imani pasipo matendo ni bure?

21Babu yetu Abrahamu alihesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya matendo yake. Yeye alimutoa mwana wake Isaka juu ya mazabahu.

22Basi unaona kwamba imani yake ilionekana kwa njia ya matendo yake na kwa njia hiyo ikapata kukamilishwa.

23Na maandiko haya yakatimia: “Abrahamu alimwamini Mungu na kwa hiyo akahesabiwa kuwa mwenye haki.” Na Mungu akamwita rafiki yake.

24Basi munaona kwamba mutu anahesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya matendo, wala si kwa njia ya imani peke yake.

25Ilikuwa hivi vilevile kwa yule kahaba Rahaba. Mungu alimuhesabia haki kwa njia ya matendo yake, wakati alipowakaribisha wapelelezi na kuwatorosha kwa njia nyingine.

26Kwa maana kama vile mwili usiokuwa na pumzi ndani yake umekufa, hivi vilevile imani pasipo matendo imekufa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help