2 Wafalme 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Elisha anamusaidia mujane masikini

1Basi, mwanamuke mumoja kati ya wake za wanafunzi wa manabii akamwendea Elisha, akamwambia: “Mutumishi wako, mume wangu amekufa, na kama vile unavyojua, alikuwa mwenye kumwogopa Mungu. Lakini mutu aliyemukopesha feza amekuja kuwatwaa wana wangu wawili wakuwe watumwa wake.”

2Elisha akamwuliza: “Sasa nikusaidie namna gani? Uniambie kile unachokuwa nacho kwako.”

Mama yule mujane akamujibu: “Mimi mutumishi wako sina kitu chochote lakini chupa ndogo ya mafuta.”

3Elisha akamwambia: “Kwenda kwa jirani zako, uazime vyombo vitupu vingi vya kutosha.

4Kisha uende, wewe pamoja na wana wako, mujifungie ndani ya nyumba, na muanze kujaza mafuta. Kila chombo munachojaza, mukiweke pembeni.”

5Akaenda na kujifungia ndani ya nyumba na wana wake na kuanza kumimia mafuta ndani ya vyombo.

6Vilipojaa vyote, akamwambia mwana wake mumoja: “Uniletee chombo kingine.”

Mwana wake akamujibu: “Vyote vimejaa!”

Hapo mafuta yakakoma kutiririka.

7Akarudi kwa mutu wa Mungu na kumweleza habari hiyo. Naye mutu wa Mungu akamwambia: “Kwenda uuzishe hayo mafuta na kulipa madeni yako, ndipo wewe na wana wako mutaishi kwa kutumia hayo yatakayobaki.”

Elisha na mama tajiri Musunami

8Siku moja Elisha alikwenda Sunemu, ambako kulikuwa mama mumoja tajiri. Mama yule akamwalika Elisha kwa chakula, na toka siku hiyo ikakuwa kawaida Elisha kula chakula kwake kila mara alipopitia kule.

9Mama yule akamwambia mume wake: “Sina shaka kwamba mutu huyu anayefika kwetu kila mara ni mutakatifu wa Mungu.

10Ninakuomba basi tumujengee chumba na kule tumwekee kitanda, meza, kiti na taa, kusudi akitumie kila mara anapotutembelea.”

11Siku moja Elisha akafika kule na kuingia ndani ya chumba chake kusudi apumzike.

12Akamwambia mutumishi wake Gehazi: “Umwite yule mama Musunami.” Alipomwita akakuja na kusimama mbele yake.

13Naye Elisha akamwambia Gehazi: “Umwambie, tumeona jinsi alivyotushugulikia; sasa anataka tumutendee jambo gani? Angependa aombewe lolote kwa mufalme au kwa jemadari wa waaskari?”

Mama Musunami akamujibu: “Mimi ninaishi kati ya watu wangu.”

14Elisha akasema: “Tumufanyie nini basi?”

Gehazi akamujibu: “Hakika hana mutoto, na mume wake amekuwa muzee.”

15Elisha akamwambia: “Umwite.” Naye akamwita. Akakuja na kusimama kwenye mulango.

16Elisha akamwambia: “Mwaka kesho, kwa wakati kama huu, utakuwa na mutoto katika mikono yako.”

Mama akamujibu: “Hapana, Bwana wangu! Wewe ni mutu wa Mungu; usinidanganye mimi mutumishi wako!”

17Lakini yule mwanamuke akapata mimba na kuzaa mutoto wakati kama ule mwaka uliofuata, kama vile Elisha alivyokuwa amemwambia.

18Mutoto yule alipokomaa, alitoka siku moja pamoja na baba yake akafuatana na wavunaji,

19naye akamwambia baba yake: “Ole, kichwa changu! Ninaumwa na kichwa!”

Baba yake akamwambia mutumishi wake mumoja: “Umupeleke kwa mama yake.”

20Alipofikishwa kwa mama yake, aliikaa juu ya magoti ya mama yake mpaka saa sita za muchana, halafu akakufa.

21Mama yake akamupeleka na kumulalisha kwenye kitanda cha mutu wa Mungu, akaufunga mulango na kuondoka.

22Akamwita mume wake na kumwambia: “Unipe mutumishi mumoja na punda mumoja, kusudi nimwendee mara moja yule mutu wa Mungu, kisha nitarudi.”

23Mume wake akamwuliza: “Kwa nini unataka kumwona leo? Leo si sikukuu ya mwandamo wa mwezi wala Sabato.”

Akamujibu: “Si neno.”

24Akatandika punda na kumwambia mutumishi: “Sasa kaza mwendo, wala usipunguze mpaka nitakapokuambia.”

25Basi, akaondoka, akaenda mpaka kwenye mulima Karmeli kule mutu wa Mungu alipokuwa.

Mutu wa Mungu alipomwona akikuja, akamwambia Gehazi mutumishi wake: “Angalia, ninamwona Musunami akikuja.

26Kimbia mara moja kumupokea na kumwuliza: ‘Uko muzima? Mume wako ni muzima? Mutoto ni muzima?’ ”

Naye Musunami akamujibu: “Tuko wazima.”

27Alipofika kwenye mulima kwa mutu wa Mungu, akamushika miguu, naye Gehazi akakaribia kusudi amwondoe. Lakini mutu wa Mungu akamwambia: “Umwache, maana ana uchungu mukali, naye Yawe hakunijulisha jambo hilo.”

28Huyo mama akamwambia: “Bwana wangu, mimi nilikuomba mutoto? Sikukusihi kwamba usinipatie matumaini ya uongo?”

29Elisha akamwambia Gehazi: “Ujitayarishe kusafiri, twaa fimbo yangu, na uende mara moja. Usisimame katika njia kwa kumusalimia mutu yeyote, na mutu yeyote akikusalimia katika njia, usipoteze wakati kwa kumurudishia salamu. Kwenda moja kwa moja mpaka katika nyumba na kuweka fimbo yangu juu ya uso wa mutoto.”

30Mwanamuke akamwambia Elisha: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.”

Basi Elisha akaondoka na kufuatana naye.

31Gehazi akatangulia mbele, na alipofika akaweka fimbo ya Elisha juu ya uso wa mutoto, lakini hakukuonekana kitambulisho chochote cha uzima. Akarudi na kukutana na Elisha, akamwambia: “Kijana hakuamuka.”

32Elisha alipofika, akaingia peke yake ndani ya chumba na kuona maiti ya kijana kwenye kitanda.

33Basi, akafunga mulango na kumwomba Yawe.

34Halafu akajilaza juu ya mutoto, kinywa chake juu ya kinywa cha mutoto, na macho yake juu ya macho ya mutoto na mikono yake juu ya mikono ya mutoto. Na alipokuwa amekaa hivyo, mwili wa mutoto ukaanza kupata joto.

35Elisha akasimama na kutembeatembea ndani ya chumba, kisha akarudi na kujilaza tena juu ya mutoto. Mutoto akapiga chafya mara saba, halafu akafungua macho.

36Elisha akamwita Gehazi na kumwambia: “Umwite yule Musunami.” Alipoitwa Elisha akamwambia: “Kamata mwana wako.”

37Akainama kwenye miguu ya Elisha kwa shukrani na kumukamata mwana wake.

Miujiza mingine miwili ya Elisha

38Elisha akarudi Gilgali wakati katika inchi kulikuwa njaa. Siku moja, alipokuwa akifundisha wanafunzi wa manabii alimwambia mutumishi wake: “Weka chungu kikubwa juu ya moto, uwapikie manabii chakula.”

39Mumoja wao akaenda katika shamba na kuchuma mboga. Kule akaona mboga za pori, akachuma mboga nyingi kwa kadiri alivyoweza kubeba. Akakuja nazo, akazikatakata na kuzitia ndani ya chungu bila kuzijua.

40Chakula kikapakuliwa. Lakini walipokionja wakamulilia Elisha wakisema: “Ee mutu wa Mungu, chakula hiki kitatuua!” Nao hawakuweza kukikula.

41Elisha akaagiza aletewe unga. Akaletewa unga, naye akautia ndani ya chungu na kusema: “Sasa uwape chakula wakule.” Wakakikula, na hapo hakikuwazuru.

42Mutu mumoja akatoka Bali-Salisa, akamuletea Elisha mikate makumi mbili iliyotengenezwa kwa shayiri ya malimbuko ya mavuno ya mwaka ule na masuke mabichi ya ngano katika gunia. Elisha akamwagiza Gehazi awape watu wakule.

43Mutumishi wake akasema: “Sitawapa kwa sababu hakitawatosha watu mia moja”.

Elisha akasema: “Uwape wakule, kwa sababu Yawe amesema kwamba watakula na kushiba na kingine kitabaki.”

44Mutumishi wake akawatayarishia chakula, wakakula na kushiba, na kingine kikabaki, kama vile Yawe alivyosema.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help